Uislamu
 ni dini ambayo imekamilika kwa namna ambayo yeyote aweza kuifuata na 
kuisimamisha. Sio dini ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa 
sallam) wala Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘Anhum) pekee. Bali ni dini ya 
Ulimwengu mzima. Historia yaonesha kwamba Uislamu ulikuwa na nguvu kubwa
 enzi za nyuma kuliko hali tuliyokuwa nayo sasa. Hivyo, kama misingi hii
 inaweza kufuatwa na wasiokuwa Waislamu, kwanini Waislamu wenyewe 
washindwe kuzifuata?
Yaonesha
 dhaahir kwamba hila zinabuniwa, kutekelezwa na kufanikiwa katika 
kuangusha mila na desturi za Kiislamu kwani hakuna taifa wala Kiongozi 
mmoja wa kuwaunganisha Waislamu. Uislamu ni dini yenye Shahadah moja, 
Qiblah kimoja, Mfungo wa Swawm mmoja na Hijjah moja tu. Hivyo yaonesha 
wazi wazi kuwa ni dini ya mshikamano, lakini bado haitendewi haki namna 
inavyotakiwa. Kilio kikubwa ni kwamba, juu ya kuwepo nguzo hizi za 
kutuunganisha lakini hatuna kauli moja wala vitendo vyenye muelekeo 
mmoja katika mila na desturi zetu. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa 
aalihi wa sallam) amesema kwamba Waumini ni wamoja na wanafanana na 
jengo:
((Hakika Muumini Kwa Muumini ni kama jengo, wanashikamana pamoja)) Akafungamisha Vidole vyake pamoja [Al-Bukhaariy na Muslim]
Badala yake, tunaiendea kinyume Hadiyth hiyo na kuwa pamoja na hila za Magharibi katika kuupiga vita Uislamu.
Tunashuhudia
 kuwepo mlolongo mkubwa wa shughuli za kuwadumaza Waislamu ili wasiwe ni
 wenye kuona mbali na kuweza kutoa mawazo ambayo yatakwenda kinyume na 
misingi ya kibepari. Misingi hii ya kibepari ni ile ambayo inamtoa 
thamani mwanamke, kuwadhalilisha viumbe kwa neno la demokrasia na uhuru.
 Imekuwa hii dunia ni uwanja wa fujo tu, mpate mpatae, mshike mshike. Hajulikani nani muadilifu wala mtenda madhambi.
Waislamu
 tumefanana na mbu kukosa kumbukumbu. Kwani hatukumbuki namna 
walivyopigwa vita, kubakwa, kuuawa na kuteswa Waislamu waliopo 
Afghanistan kwa neno la ‘ugaidi’, Iraaq kwa neno la ‘dikteta’ na 
Chechnya kwa neno la ‘usalama’. Yote haya yanafanywa kwa nani na kwa 
ajili ya kupata nini? Hakuna chengine kinachogombaniwa hapa ila kuhodhi 
mamlaka chini ya mkono mmoja wenye nguvu za kushika na kuachia.
Utawala
 huu wa kimabavu duniani bado unaendelea, na unalenga zaidi kunufaisha 
nchi za Magharibi. Mfano mzuri tu ni namna Waislamu wanavyoshughulishwa 
mno na mambo ya anasa na kupoteza muda.
Mechi za mpira ni moja kati ya zana kuu zinazotumiwa kuupiga vita Uislamu. Kama
 hatutakuwa makini, daima tutakuwa wapofu kwa kuhifadhi majina ya 
wachezaji pamoja na historia ya klabu za mpira. Huku tukiacha nyuma Siyrah
 tukufu ya Uislamu pamoja na matendo sahihi ya Uislamu. Hatukai 
kufikiria namna mzunguko wa mechi hizi zinavyopokezana, mechi zisizokuwa
 na mwisho kana kwamba wanaoshuhudia pia ni wenye kufanya mazoezi ya 
mpira. 
Kuna
 mechi za ligi kuu ndani ya mikoa, nchi nzima, nchi jirani pamoja na 
Afrika nzima. Ukipiga hesabu utapata takriban sio chini ya mechi 100 kwa
 mwaka mzima. Tukitoka Afrika, tunakwenda chimbuko la ukoloni duniani na
 kupata mashindano ya kombe la Uingereza, carling cup na FA 
yanayoshindaniwa kila mwaka. Kabla yake kuna mechi za Uingereza, Spain na Ujerumani. Kama
 hizo hazitoshi, kuna kombe la dunia la kila baada ya miaka minne. Huku 
mechi zikichuja hatua kwa hatua kupata mataifa yatakayoshiriki kombe la 
dunia.
Huko
 ndiko akili zilipoelekezwa. Ni kutokana na mechi hizi, Waislamu 
wanaswali kwa kudonoa donoa namna kuku anavyodonoa mtama. Akili 
hazijajikomboa kuona namna Uislamu unavyoangushwa na kutengenezewa hila 
mpya kila siku. Iblisi na kundi lake la Magharibi hawalali wakitafakari 
njia mbadala za kuwapotosha Waislamu bila ya kuwabatiza.
Mechi hizi ndizo zinazowafanya Waislamu kushindwa kusoma fiqhi na kuelewa taratibu za ndoa, mirathi na kadhalika. Mtandao wa Alhidaaya   umejaa masuala kede kede yenye kuonesha dhaahir mmommonyoko wa maadili. Inafikia hatua Muislamu anauliza kama uzinifu (kuwa na girlfriend au boyfriend) ni halali au haramu? Yote hayo yanatokana na kukosa elimu kwa kufuata mdundiko wa pumbazo kama hizi.
Jee
 hatujafikia hatua ya kuamini namna hizi akili zilivyotekwa nyara? Bila 
ya shaka yoyote hazitakuwa ni akili zenye kuona mbali isipokuwa kuweka 
mbele mazungumzo ya mpira badala ya kupanga mikakati ya kukuza Uislamu, 
kuchangia miradi ya Uislamu pamoja na kuhisabu Waislamu wanaouawa kila 
leo na kudhulumiwa kila sekunde. Mechi hizi ndizo zinazotengeneza njia 
ya kuendeleza biashara za ulevi kwa matangazo ya pombe kwenye viwanja na
 fulana za wachezaji, kukuza uchumi wa Magharibi na kuwadumaza Waislamu.
Tuanze leo, tusisubiri zaidi kubadilika na kuishi Kiislamu katika kila hatua. Kama
 kweli tunahitaji mpira, tusiwe ni wenye kufuata tu kila kitu. Tutumie 
muda muafaka kufanya mazoezi ya kweli kweli kusakata kandakanda huku 
tukitumia muda mwingi zaidi kutafakari juu ya Uislamu wetu. Kuwa bwana 
wa nafsi yako na wala usiwe mtumwa kwa nafsi yako kufuata kila 
kipendacho nafsi.
No comments:
Post a Comment