Jibriyl
 (‘Alayhis Salaam) aliposhuka kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa 
aalihi wa sallam) alimtikisha na kumbana barabara akimuamuru kusoma kwa 
jina la Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala). Mola Ambaye Amemuumba mwanadamu 
kwa tone la damu na kumfunza kwa kutumia kalamu.
	Iwapo
 kipenzi cha Mola Mlezi asiyejua kusoma wala kuandika ametikishwa namna 
hiyo, je sisi tutarajie nini katika kutafuta elimu? Wengi wa Waislamu ni
 wenye kwenda na kurudi bila ya kutilia mkazo elimu ya Kiislamu. Na kama
 Waislamu watasimama kihaki liLlaahi kuitafuta elimu, basi ndio itakuwa 
sababu ya kuondoka udhalilifu walionao Waislamu hivi sasa. 
	Katika
 baadhi ya miji ya Waislamu, utakuta kuna Misikiti chungu nzima lakini 
Madrasah zikiwa kidogo kweli kweli. Sasa hiyo Misikiti ikaswalishwe na 
kusomeshwa darsa na nani? Ingawa hizo Madrasah pia zipo na zimejaa taa 
na mazulia mazuri mazuri, lakini wanafunzi wake ni wachache kabisa. 
Kwanza Waislamu watilie mkazo kusoma na kusomesha, badaye ndio 
wasambazwe hao waliosoma ndani ya Misikiti. Na kwa bahati mbaya, hivi 
sasa Misikiti na Madrasah ni vitu viwili tofauti. Misikiti mingi 
inajengwa kwa ajili ya kuswalia tu, na Madrasah kwa ajili ya kusoma tu. 
Tumesahau ya kwamba Mtume aliujenga Msikiti ambao ndio kiini cha elimu 
ya Kiislamu na hivi sasa unatoa shahada za juu kabisa kwa wanafunzi.
	Mtume
 (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipewa utume kwa kauli ya
 "Iqraa" iliyomo ndani ya Suratul-'Alaq na akaamrishwa kulingania 
kupitia aya za mwanzo za Suratul-Muddathir. Tunachojifunza hapa ni 
kwamba amri ya kusoma imekuja mwanzo kabla ya kulingania. Na bila ya 
shaka Mola Amemuamuru mwanaadamu kutafuta elimu kabla ya kumuamuru 
kumuelewa Mola Mwenyezi (elimu ya tawhiyd). Kwani kupitia elimu ndio 
atapata wepesi wa kumpwekesha Mwenyezi Mungu. Allaah (Subhaanahu wa 
Ta’ala) Anasema ndani ya Qur-aan:
	{{Jua ya kwamba hakuna aabudiwaye kwa haki ila Mwenyezi Mungu.}} [Suratu-Muhammad: 19]
	Amri
 ya Mola inayosema "jua" ina maana sawa na "soma". Kilichopo hapo ni 
kwamba kwanza tusome na ndani ya hiyo elimu tutaelewa kuwa hakuna 
aabudiwaye kwa haki ila Mwenyezi Mungu. Hii inatutambulisha kwamba amri 
ya kumtambua Mola ipo chini kulinganisha na amri ya kutafuta elimu.
	Tuzingatie na tuelewe ule msemo wa Waarabu unaosema: "العلم من المعهد إلى العهد"
	wenye
 maana kwamba elimu ni ya kutafutwa milele kuanzia chuoni hadi mwisho wa
 maisha yake mtu. Tusikate tamaa katika kutafuta elimu. Kwani elimu ni 
ngumu kuipata na ndio silaha yako hapa duniani na kesho Akhera iwapo 
utaitumia vyema. Hata unapofariki, warithi wako hawataipata kwani 
unaondoka nayo kama vile unavyoondoka na ‘amali zako. Watabaki kurithi 
hizo pumbao za dunia. Na kama umeisoma kisha ukaisomesha na kuwapatia manufaa watu, basi thawabu zake utaendelea kuzichuma hadi kaburini insha Allaah.
	Tunamuomba
 Mola Atupatie fahamu ya Manabii na nyoyo zenye kuelewa mambo kwa wepesi
 kabisa. Atufunulie akili zetu kwa mambo yenye manufaa na kuzifunga 
akili zetu zisifahamu wala kuelewa hata kidogo yale yasiyo na manufaa. 
Aamiyn!
No comments:
Post a Comment