Nani Aliyepanga Surah, Aayah Na Nani Aliyetoa Majina ya Surah?
	SWALI:
	Swali La Kwanza:  
	Asslaam aleykum,
	Ni 
nani aliezipanga sura za Qur-an katika mpango tunaouona sasa. Ni kwa 
nini na kuna hikma gani. Ikiwa Suratul Baqra imeteremshwa Madina kwa 
nini iwe ya pili katika msahafu na isiwe ya 86, kwani za mwanzo zilianza
 kuteremshwa Makkah?
	Swali La Pili: 
	Shekh,
 naomba tafadhali maelezo nani aliyetoa majina ya sura za qurani?  Vipi 
zimepangwa aya ikiwa Qurani imeteremshwa kidogo kidogo kuanzia iqra hadi
 aya za mwisho kabla kufa Mtume maana naona imeanza Alhamdu na 
kumalizikia Qul-audhu. 
	JIBU:
	Sifa 
zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, 
Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 
‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.
	Shukrani
 zetu za dhati kwa swali lako kuhusu upangaji wa surah za Qur-aan. Ni 
jambo linaloeleweka kuwa hakuna jambo lolote la Uislamu isipokuwa lina 
hekima kubwa ni sawa tunazijua hizo hekima au la.
	Mpangilio
 wa Qur-aan na majina yake yamepangwa na Yeye Mwenyewe Allaah Mwenye 
hekima na busara kubwa. Tufahamu kuwa Qur-aan yote ilikuwa imehifadhiwa 
na Allaah Aliyetukuka katika sehemu inayoitwa Lawhul Mahfuudh na kisha 
kuteremshwa yote usiku wa al-Qadr katika mwezi wa Ramadhaan hadi wingu 
wa duniani. Kutoka hapo Jibriyl ('Alayhis Salaam) akawa ni mwenye 
kupatiwa amri na Aliyetukuka kumteremshia Mtume wa Allaah (Swalla 
Allaahu 'Alayhi wa aalihi wa sallam) kidogo kidogo kwa miaka 23 
kulingana na mahitajio. 
	Kila 
ilipokuwa inateremshwa Surah au baadhi ya Aayah Jibriyl ('Alayhis 
Salaam) kwa maagizo kutoka kwa Allaah Aliyetukuka alikuwa akimuamuru 
Mtume (Swalla Allaahu 'Alayhi wa aalihi wa sallam) aiweke mahali kadhaa 
na jina la Surah liwe kadhaa. Baada ya kuhama Madiynah, Jibriyl alikuwa 
akija kila Ramadhaan kumsikiliza Mtume (Swalla Allaahu 'Alayhi wa aalihi
 wa sallam) kisomo cha Qur-aan. Na ule mwaka aliokufa, Jibriyl alikuja 
mara mbili na mara ya mwisho Zayd bin Thaabit (Radhiya Allaahu 'anhu) 
alikuwepo.
	Hivyo, alivyoaga dunia (Swalla Allaahu 'Alayhi wa aalihi wa sallam), Maswahaba (Radhiya Allaahu 'anhum) waliandika Qur-aan kama
 walivyofundishwa na kuagiziwa na Mtume (Swalla Allaahu 'Alayhi wa 
aalihi wa sallam). Hata wale waandishi wa Mtume (Swalla Allaahu 'Alayhi 
wa aalihi wa sallam) walikuwa wakipatiwa maagizo hayo.
	Ama kuhusu Suratul Baqarah kuwa ni ya 86 si kweli na huenda kuwa ndugu yetu akawa amekosea katika ubinaadamu wake. Na hilo
 si la ajabu. Hakika ni kuwa Suratul Baqarah ni Surah ya 87 kuteremshwa 
na ya kwanza kuteremka Madiynah. Surah ya mwisho kuteremshwa Makkah 
ilikuwa ni ya 86 nayo ni Suratul Mutwaffifiyn (83).
	Na Allaah Anajua zaidi
No comments:
Post a Comment