Toa Swadaqah Kwa Ajili Ya Allaah
 Naaswir Haamid
 Ihsaan
 ni kinyume cha ufisadi, na miongoni mwa Ihsaan ni kufanya wema bila ya 
kujali mipaka ya Kaskazi wala Kusi, na kutoa kwa ajili ya Allaah ni wema
 na Ihsaan kwa mwanaadamu.
 Hakuna
 shaka yoyote kwamba Swadaqah ni katika tabia njema, na iwapo tutafungua
 kurasa za Siyrah za wema waliotangulia, tutaona kwamba walikuwa 
wakikithiri mno kwenye kutoa Swadaqah. Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) 
Anasema: 
 {{Chukua Swadaqah katika mali zao, uwasafishe na kuwatakasa kwa ajili ya hizo (Swadaqah zao).}} [At-Tawbah: 103]
 Kupitia
 Tamko hilo hapo juu, tunafahamu kwamba kumbe kuisafisha nafsi kutokana 
na takataka za upungufu na kuiinua jamii mpaka kuifikisha kwenye daraja 
tukufu kabisa, ndio hekima ya juu. Ni kwa ajili hii ndio Mtume (Swalla 
Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipanua wigo katika kuelezea maana
 ya neno “Swadaqah” ambayo Muislamu anatakiwa kuitoa, akasema: 
 ((Tabasamu
 lako usoni kwa nduguyo (Muislamu mwenzio) ni Swadaqah, kuamrisha kwako 
mema na kukataza kwako maovu ni Swadaqah. Na kumuongoza kwako njia mtu 
katika ardhi (nchi) ya upotevu, hilo kwako ni Swadaqah. Na kuondosha 
kwako njiani udhia, mwiba na mfupa, hilo kwako (nalo) ni Swadaqah. Na 
kumtekea kwako maji nduguyo, kwako ni Swadaqah na kumsaidia kwako mtu 
dhaifu wa uoni kuongoza njia, (hilo nalo) kwako ni Swadaqah)). [Al-Bukhaariy]
 Swadaqah
 huanza kwa kuuzoesha mkono kutoa kila mara bila ya kinyongo wala 
manuuniko. Mkono una dhima kuu ya kukulingania kutoa Swadaqah katika 
vile ulivyoruzukiwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kama Alivyosema:
 {{Yule
 anayetoa (Zakaah, Swadaqah na vinginevyo) na kumcha Allaah. Na kusadiki
 jambo jema (akalifuata). Tutamsahilishia njia ya kwenda Peponi.}} [Al-Layl: 5-7] 
 Hiyo
 ndio faida na jazaa ya aliyeutumia vyema mkono wake katika kutoa 
Swadaqah. Akautumia mkono wake katika kutoa vile Alivyoruzukiwa na 
Allaah Ar-Razzaaq, katika kuisadia jamii na kuupeleka mbele Uislamu.
 Ni vyema ukakumbuka kwamba kutoa katika mambo ya khayr ni katika kuishukuru neema ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala). Ambako hakumaanishi ila kuzidishiwa neema, tusome kwa mazingatio: 
 {{Na
 (kumbukeni) Alipotangaza Mola wenu (kuwa): "Kama mkishukuru, 
Nitakuzidishieni; na kama mkikufuru, (jueni) kuwa adhabu Yangu ni kali 
sana.}} [Ibraahiym: 7]
 "Mtenda wema hutendea nafsi yake na mtenda ovu humrejea mwenyewe". Hivyo
 elewa kamba kuishukuru neema kikweli kweli na kuitumia vile 
inavyostahiki sio tu kusema au kuandika kwenye milango kwa mbwembwe: ‘AlhamduliLlaah’ au ‘Hadha Min Fadhli Rabiy’! Na ni ubaya ulioje kuzitumia neema hizi kinyume na vile Alivyoamrisha Ar-Razzaaq.
No comments:
Post a Comment