Mashairi


Muhammad Faraj Saalim As-Sa’ay

Bwana Mwenye Kumilki
Mayahudi wahiliki
Watoweke wasibaki
Penye uso wa duniya


Hawa wasio na haya
Waovu tena wabaya
Adui wa insaniya
Na adui wako piya


Nchi wanaiunguza
Roho wanaangamiza
Nyumba wanateketeza
Ghaza inaangamiya


Vijana wapukutika
Vizuka waongezeka
Watu wanamahanika
Mayatima wanaliya


Wanapiga kwa roketi
Skuli na marikiti
Kila pahali maiti
Kote wameshaenya


Waisilamu jasiri
Wapigwa na makafiri
Hapana alofikiri
Kwenda kuwasaidiya


Watu wote wamegoma
Wengine wapiga ngoma
Na wengine wakoroma
Hawataki kusikiya


Damu hii ni nzito
Inakwenda kama mito
Wazee hata watoto
Wanawake nao piya


Hawana wanachojali
Hawana hata muhali
Hata mahospitali
Pia wanashambuliya


Ya Ilahi ya Manani
Irudishe yetu shani
Turudi kama zamani
uma ulotanguliya


Neno letu liwe moja
Pasiwepo na kungoja
Tuwapige kwa pamoja
Kwa uwezo wa Jaliya


Kama yule mwanamama
Alotekwa na waroma
Waa Muutasima
Kwa sauti aliliya


Muutasima akasema
Ewe mbwa wa Waroma
Umuache huyo mama
Ama utajijutiya


Jeshi akasimamisha
Tena kubwa la kutisha
Warumi hawakubisha
Wakaikunja mikiya


Mola wetu ya Manani
Turudishie imani
Turudi kama zamani
Wakati wa Salafiya


Tuungane kwa pamoja
Neno letu liwe moja
Sote tuwe nguvu moja
Enzi zetu kurudiya


Adui atuhofiye
Iondoke miye miye
Kila kitu kiwe siye
Uma wa Muhamadiya


Aridhi tuwashe moto
Wakubwa pia watoto
Kwa risasi na kokoto
Tuanze kushambuliya


Tulikuwa maamiri
Kwao hawa makafiri
Wakifuata amri
Kila tunachowambiya


Hata hivyo hatukuwa
Tukichinja na kuua
Kila mtu alikuwa
Na haki ilotimiya


Sasa wao wanatamba
Wanajifanya mamwamba
Wamesahau yakwamba
Inazunguka duniya


Khaybari ya Yahudi
Tulikulaza kifudi
Jeshi letu litarudi
La Muhamadi Nabiya


Hamadi alishasema
Naye mkweli daima
Hakisimami Qiyaama
Aridhi itarejeya


Hiyo ni ahadi yake
Kutoka kwa Mola wake
Mkitaka msitake
WaLlaahi mtakimbiya


Mti wa gharqadi
Ni mti wa Mayahudi
Nyuma yake itabidi
Mjifiche na kuliya


Kisha humo mtatoka
Huku mukipapatika
Hamuwezi kutoroka
Wala hata kukimbiya


Watu hawa maluuni
Mungu Ameshawalani
Ndani ya Quruani
Na hadithi za Nabiya


WaLlaahi ninaandika
Huku jasho lanitoka
Na moyo kuungulika
Kwa haya yanotokeya
**************Siku ya Qiyama*******

Hodi mlango nabisha, salaam zangu pokeeni,
Wajibu kukaribisha, akiwasili mgeni,
Sikuja kuwafundisha, bali natoa maoni,
QIYAAMA kipo njiani, siku hiyo inatisha.

Siku hiyo inatisha, Kiyama kipo njiani,
Ni nani ataebisha, wote kimya hadharani,
Siku ya kusikitisha, na siku yenye huzuni,
QIYAAMA kipo njiani, siku hiyo inatisha.

Ndio mwanzo wa maisha, ya pepo na ya motoni,
Yote Atarekebisha, Rabuka kwenye mizani,
Ukweli kubainisha, na haki itabaini,
QIYAAMA kipo njiani, siku hiyo inatisha.

Mitume Watasimama, na wao pia foleni,
Hakuna ataesema, mpaka Aje Rahmani,
Hapo watu hutetema, ataepasi ni nani?
QIYAAMA kipo njiani, ongezeni yenu mema.

Ikipigwa baragumu, sijuwi niseme nini,
Siku hiyo siku ngumu, kwa viumbe ardhini,
Siku ya kujilaumu, majuto tupu usoni,
QIYAAMA kipo njiani, tuwe tayari kaumu.

Majabali kuvunjika, kupeperuka angani,
Ardhi kutetemeka, kuja juu yalo chini,
Bahari moto kuwaka, Ya Ilahi Ya Manani,
QIYAAMA kipo njiani, tukae tukikumbuka.

Nyota zitapukutika, hazitabaki mbinguni,
Na jua litakunjika, imesema Qur-aani,
Na mimba kuharibika, mwana kutoka tumboni,
QIYAAMA kipo njiani, na tuzidishe sadaka.

Watoto huota mvi, nywele zote za kichwani,
Na watu kama walevi, hivyo wewe utadhani,
Na kumbe sio walevi, adhabu kali jamani,
QIYAAMA kipo njiani, fanya wema sasa hivi.

Allah Atakunja mbingu, kwa Mkono ni yakini,
Watafufuliwa wafu, watoke makaburini,
Tusimame kwenye safu, bila ya nguo mwilini,
QIYAAMA kipo njiani, tushike dini tukufu.

Kila mtu nafsi nafsi, na ndugu hawajuani,
Baba na mwana ni basi, umeshakwisha ubini,
Hakuna tena nafasi, mapenzi hufa moyoni,
QIYAAMA kipo njiani, tenda mazuri upesi.

Tuwe tayari kabisa, kwa ibada na imani,
Tuanze kutoka sasa, tuiizingatie dini,
Tuache zote anasa, na michezo ya kihuni,
QIYAAMA kipo njiani, tabia piga msasa.

Hapa nimefika mwisho, kuandika natamani,
Lakini natokwa jasho, nimechoka samahani,
Tufikirie ya kesho, Kiyama sio utani,
QIYAAMA kipo njiani, Siku Hiyo Ya Vitisho.************************************
*****

Salaam zangu natuma, ziwafike Afrika,
Mungu Awape hekima, mzidi kuneemeka,
Naomba Zake rehema, zivuke zote mipaka,
Omba Toba kwa haraka, madhambi unapotenda.

Madhambi unapotenda, omba toba kwa haraka,
Mungu sana Anapenda, Aombwe kila dakika,
Hujuwi unapokwenda, lini roho itatoka,
Omba Toba kwa haraka, madhambi unapotenda.

Yupo macho Maulana, Halali na Kuzeeka,
Kila kitu Anaona, yote yanayotendeka,
Si usiku si mchana, Yupo macho Mtukuka,
Omba Toba kwa haraka, madhambi unapotenda.

Yupo karibu na sisi, dua Kwake zinafika,
Ili zifike upesi, tuzidi Kumkumbuka,
Tuache yote maasi, ili Apate ridhika,
Omba Toba kwa haraka, madhambi unapotenda.

Wakati unatoroka, tupo kwenye hekaheka,
Mauti yatatufika, ghafla tutaanguka,
Hapo tunapodondoka, toba imeshafungika,
Omba Toba kwa haraka, madhambi unapotenda.

Shetani yupo mbioni, humuoni akichoka,
Hutupambia machoni, baya sawa huliweka,
Atutie mtegoni, halafu anatucheka,
Omba Toba kwa haraka, madhambi unapotenda.

Alipokua peponi, Adamu kahadaika,
Kadanganywa na shetani, balaa ikamfika,
Akatubu Kwa Manani, mwishowe akaokoka,
Omba Toba kwa haraka, madhambi unapotenda.

Kuomba toba ni nzuri, kosa linapofanyika,
Unajiweka tayari, ajali inapofika,
Kumbuka mbele kaburi, na moto usozimika,
Omba Toba kwa haraka, madhambi unapotenda.

Omba toba kila mara, huku ukisikitika,
Omba sana maghfira, toa kidogo sadaka,
Kumbuka sana akhera, na siku ya kufufuka,
Omba Toba kwa haraka, madhambi unapotenda.

Mungu Atupe uzima, hapa mwisho kuandika,
Atupe nguvu na hima, radhi Zake tunataka,
Atupe nzuri hatima, na madhambi kufutika,
Omba Toba kwa haraka, madhambi unapotenda.************kudra na imaan

             ‘Abdallaah Bin Eifan
           (Jeddah, Saudi Arabia)


Salaam waheshimiwa, nawaombea baraka,
tunaomba kujaliwa, kila kheri na fanaka,
tupate kuokolewa, tutoke kwenye mashaka,
Lazima kitakufika, kile kilichoandikwa.

Kile kilicho andikwa, lazima kitakufika,
nahodha anaposhindwa, bahari ikichafuka,
na rubani kwenye hewa, ndege ikipeperuka,
Lazima kitakufika, kile kilichoandikwa.

Mvuvi anapovua, samaki kukusanyika,
akikosa anajua, leo Mungu Hakutaka,
hawezi kujisumbua, kununa kukasirika
Lazima kitakufika, kile kilichoandikwa.

Mkulima hushtushwa, shamba moto likiwaka,
ajue akiulizwa, kama ametoa zaka,
asiseme kasakamwa, au mkosi umefika,
Lazima kitakufika, kile kilichoandikwa.

Biashara  ikifanywa, na ukifungua duka,
kama hukufanikiwa, uache kunung'unika,
pengine hudhulumiwa, watu kwako hupunjika,
Lazima kitakufika, kile kilichoandikwa.

Yote yamesajiliwa, Mungu Ameshaandika,
kalamu kuinuliwa, wino umeshakauka,
kudura imeshapangwa, hakuna kubadilika,
Lazima kitakufika, kile kilicho andikwa.

Tangu bado kuzaliwa, vyote vimeandikika,
riziki imegawiwa, na ajali kadhalika,
utajiri ukipewa, usisahau sadaka,
Lazima kitakufika, kile kilicho andikwa.

Utajiri ukinyimwa, halafu ukasumbuka,
usidhani umetupwa, Kakusahau Rabuka,
mwisho wake utalipwa, ukisubiri hakika,
Lazima kitakufika, kile kilicho andikwa.

Na mitihani mikubwa, kama inamiminika,
tumshukuru MKUBWA, subira kulazimika,
tuzidi kuomba dua, hapana kulalamika,
Lazima kitakufika, kile kilicho andikwa.

Imani yako hupimwa, ovyo hapana ropoka,
yote hayo majaliwa, kukupima Anataka,
imani kuzingatiwa, rehema itateremka,
Lazima kitakufika, kile kilicho andikwa.

Msiba unapokuwa, dhaifu hutetemeka,
kama mwehu anakuwa, imani inamtoka,
anasahau ya kuwa, Mungu hivyo Ameweka,
Lazima kitakufika, kile kilicho andikwa.

Na makelele kupigwa, maafa yakimfika,
na yote yamekatazwa, Mungu Ataghadhibika,
Apenda  kushukuriwa, Mola wetu Mtukuka,
Lazima kitakufika, kile kilichoandikwa.

Kuvumilia ni sawa, na imani kuiweka,
hadhulumiwi muumbwa, kwa haki kinatendeka,
hakuna cha kuonewa, imani ya nguvu shika,
Lazima kitakufika, kile kilichoandikwa.

Usiseme umerogwa, sababu ya kuteseka,
yote hayo yanapingwa, imani kudhoofika,
huo ndio ni ugonjwa, wa shirki usotibika,
Lazima kitakufika, kile kilichoandikwa.

Kumbuka unavyozikwa, kaburini kukuweka,
watu wote sawasawa, sanda wanawafunika,
na wote wanasaliwa, hakuna kubagulika,
Lazima kitakufika, kile kilichoandikwa.

Usikubali kushindwa, shetani akakucheka,
utageuka mfungwa, wa shetani ni mateka,
hapo ndio umekumbwa, na imani kutoweka,
Lazima kitakufika, kile kilichoandikwa.

Hirizi ukivalishwa, shingoni kuipachika,
ujuwe umedanganywa, huwezi kunufaika,
madhambi utabebeshwa, hapo umehadaika,
Lazima kitakufika, kile kilichoandikwa.

Hapa nafunga baruwa, pengine mmeshachoka,
tunaomba maridhawa, Mola Apate Ridhika,
tunaomba kuepushwa, na madhambi kufutika,
LAZIMA KITAKUFIKA, KILE KILICHOANDIKWA.***********************toa swadaqa****************

                      ‘Abdallah Bin Eifan
                   (Jeddah, Saudi Arabia)

Salaamu kwa mahabubu, zivuke yote mipaka,
Walo mbali na karibu, nawaombea fanaka,  
Nimefungua kitabu, na kalamu nimeshika,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Hapo siku ya hesabu, hukuokoa Sadaka,
Utakusanya thawabu, marundo hujirundika,
Inapunguza ghadhabu, ya Mwenyezi Mtukuka,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Inakua ni kivuli, ona inakufunika,
Utamkuta Jalali, na wewe Ameridhika,
Umetoa kwa halali, radhi za Mungu kutaka,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Khasa Sadaka ya siri, hakika imetajika,
Ina baraka na kheri, kwa Mungu hukubalika,
Huitoi kwa fakhari, ili upate sifika,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Akhera na duniani, mambo yanasahilika,
Utaona mitihani, kwa wepesi unavuka,
Nuru yazidi nyumbani, riziki huongezeka,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Toa Sadaka upesi, kabla kufilisika,
Utoe hata kiasi, kwa jina la Msifika,
Utoe kwa ikhlasi, huku umefurahika,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Usifanye kusimanga, thawabu itafutika,
Wala hapana kuringa, kudharau na kufoka,
Dini yetu inapinga, masikini kumcheka,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Kwa maiti ndio nzuri, Sadaka inamfika,
Mpaka ndani ya kaburi, thawabu humiminika,
Tena inakusitiri, siku ya kujumuika,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Duniani kwenye mali, inazidisha baraka,
Usifanye ubakhili, mwisho utahangaika,
Utakwenda na amali, mali yote hukatika,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Kwanza waliokaribu, lazima kuwakumbuka,
Kina bibi kina babu, kina dada kina kaka,
Hawa wote ni wajibu, wapate kunufaika,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Halafu ni mafakiri, kwa shida wanasumbuka,
Amewanyima Qahari, hivyo Allah Ametaka,
Kagawa rizki Jabari, yote Ameshaandika.
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Usisahau yatima, ona wanavyoleleka,
Mapenzi yale ya mama, wamekosa kwa hakika,
Kwa macho ukitazama, kweli utasikitika,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Toa kwa mambo ya kheri, yote Mola Anaweka,
Utazikuta tayari, thawabu kukusanyika,
Akhera wewe tajiri, hapo utafaidika,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Nawasihi ndugu zangu, ipate kueleweka,
Haipotei kwa Mungu, Kwake inahifadhika,
Iwe ndogo kama chungu, kwa Mola husajilika,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Sote tuwe Wakarimu, kabla ya kuondoka,
Tumridhishe Rahimu, mwisho tutapumzika,
Tuepushwe jahanamu, moto unaolipuka,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Ona Sadaka si Zakaa, Zakaa imefaridhika,
Usipoitoa Zakaa, mengi yataharibika,
Madhambi yatakufika, nguzo tano kupunguka,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.
                                                                  
Amma Sadaka khiari, hapo hukulazimika,
Ukitoa ni vizuri, akiba yako kuweka,
Mbele itakunawiri, kama taa itawaka,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

Hapa nafunga shairi, mwisho sasa nimefika,
Atuepushe na shari, Mola wetu Mtajika,
Tupo ndani ya safari, toa Sadaka haraka,
Hukuokoa Sadaka, hapo siku ya hesabu.

 

No comments: