Wednesday 24 December 2014

mambo atakayoulizwa mja siku ya qiyama

Mambo manne utayoulizwa siku ya Qiyama

Yawmul QiyaamahKutoka kwa Abu Barzah Al-Aslamiyy ambaye amesema: Mtume wa Allaah (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: ((Nyayo za mja hazitoondoka [Siku ya Qiyaamah] mpaka aulizwe juu ya umri wake alivyoumaliza, elimu yake alivyoifanyia, mali yake ameichuma kutoka wapi na ameitumia kwa mambo gani, na mwili wake aliutumia kwa kazi gani)).
  Mafunzo Na Hidaaya:
  1. Hima ya Muislamu kutumia umri wake katika yale yanayomridhisha Allaah (سبحانه وتعالى).
  1. Mambo manne hayo ni miongoni mwa neema nyingi za Allaah (سبحانه وتعالى) kwa mja, anapaswa kushukuru kwa yakini, kauli na vitendo, na ataulizwa kuhusu neema hizo.
ثُمَّ لَتُسْأَلُنَّ يَوْمَئِذٍ عَنِ النَّعِيمِ ﴿٨﴾
Kisha bila shaka mtaulizwa siku hiyo kuhusu (kila) neema (mmezitumiaje duniani?)
  1. Kuwa na ikhlaasw katika ‘amali azitendazo Muislamu. [Al-Kahf 18: 110].
  1. Himizo la kuchuma mali kutoka njia za halali na kuitumia katika yanayomridhisha Allaah (سبحانه وتعالى) pamoja na kuitolea Zakaah na sadaka na tahadharisho la chumo la haramu. [Al-Baqarah 2: 168, Twaahaa 20: 81].
  1. Kuuhifadhi mwili usitende yaliyo haramu na kuutiisha pamoja na kuutumikia katika utiifu wa Allaah (سبحانه وتعالى), na kufanya ‘Ibaadah kwa wingi.
  1. Kujifunza elimu iliyo na manufaa na aifanyie kazi kwa ikhlaasw anufaike nayo na anufaishe wengineo.
  1. Mambo manne hayo ni majukumu ya kila mtu Siku ya Qiyaamah. Hakuna atakayeondoka mbele ya Allaah (سبحانه وتعالى) bila kuulizwa.
  1. Hadiyth hii ni tahadharisho la kujirekebisha kwa mtu anayekwenda kinyume na yanayomridhisha Allaah (سبحانه وتعالى) duniani.
  1. Uhai na maisha ya dunia ni kama madrasa anayosoma mtu na kufanya juhudi, kisha mtihani wake na malipo ni Siku ya Qiyaamah. Atakayefanya kinyume chake, atapata khasara Aakhirah kwenye maisha ya milele [Ash-Shuwraa 42: 20].
مَّن كَانَ يُرِيدُ الْعَاجِلَةَ عَجَّلْنَا لَهُ فِيهَا مَا نَشَاءُ لِمَن نُّرِيدُ ثُمَّ جَعَلْنَا لَهُ جَهَنَّمَ يَصْلَاهَا مَذْمُومًا مَّدْحُورًا ﴿١٨﴾ وَمَنْ أَرَادَ الْآخِرَةَ وَسَعَىٰ لَهَا سَعْيَهَا وَهُوَ مُؤْمِنٌ فَأُولَـٰئِكَ كَانَ سَعْيُهُم مَّشْكُورًا ﴿١٩﴾ كُلًّا نُّمِدُّ هَـٰؤُلَاءِ وَهَـٰؤُلَاءِ مِنْ عَطَاءِ رَبِّكَ ۚ وَمَا كَانَ عَطَاءُ رَبِّكَ مَحْظُورًا ﴿٢٠
Anayetaka ‘aajilah (starehe za kupita kwa haraka za dunia) Tunamharakizia humo Tuyatakayo, na kwa Tumtakaye. Kisha Tutamjaalia (Moto wa) Jahannam auingie (na) kuungua hali ya kuwa mwenye kushutumiwa na kufukuziliwa mbali (kuwekwa mbali na Rahmah ya Allaah). . Na anayetaka Aakhirah na akaifanyia juhudi inayostahiki kufanyiwa, naye ni Muumin, basi hao juhudi zao ni za kushukuriwa (na kulipwa thawabu na Allaah). Wote (wanaotaka dunia na Aakhirah) Tunawakunjulia – hawa na hawa- katika neema za Mola wako. Na hazikuwa neema za Mola wako zenye kuzuiliwa (zisimfike Amtakaye Allaah)
  1.  Umuhimu wa kufanya kazi, na mtu achunge sana kazi atakayofanya, kwa sababu chumo la haramu litampeleka mtu pabaya.
  1.  Muislamu anatakiwa na shari’ah achume chumo la halali na alitumie kwa njia za halali.
  1.  Katika riwaya nyengine ya at-Tirmidhiy badala ya mwili inataja ujana umetumiwa vipi kumaanisha kuwa kipindi hicho ni muhimu sana katika maisha ya mwanaadamu na ni wakati wa kuchuma mema mengi.
Kwa hisani ya Alhidaayah

Dalili za qiyama

Abdullah ibn Abbas (r.a.) amesema kuwa baada ya kumaliza Hajj ya mwisho (mwaka wa 10 Hijriyyah), Mtume Mtukufu s.a.w.w. alisimama mbele ya mlango wa Ka'aba Tukufu, akiwa ameshikilia komeo ya mlango, huku akiwauliza ma-Sahaba wake: "Je, nikuambieni dalili za siku ya QIYAMA?" Salman Farsi (r.a.) ambaye alikuwa karibu naye, alisema:"Ndiyo, Ewe Mtume wa Allah swt."

Mtume Mtukufu s.a.w.w. akasema, "Hakika,miongoni mwa dalili za saa, ni kuwa (1) watu watapuuza sala, (2) watafuata matamanio yao wenyewe (3) wataelekeza kujipendelea wao wenyewe, watawaheshimu matajiri, (4) na watauza Dini yao kwa manufaa ya kidunia (5) wakati huo roho na moyo wa Muumin itayayuka (kwa huzuni) kama chumvi inavyoyayuka katika maji, kwa sababu ataona mambo yaliyoharamishwa na hataweza kuyabadili."

Salman akasema: "Haya yatatokea, ewe Mtume wa Allah swt?"
Mtume Mtukufu s.a.w.w. akasema: "Ndiyo, naapa kwa Aliyonayo roho yangu mkononi mwake."

"Ewe Salman, (6) wakati huo watawala watakuwa wadhalimu (7) Mawaziri watakuwa waasi, (8) na wadhamini (wale waliopewa amana kwa kuaminiwa) watafanya hiana, (9) hakika wakati huo maovu yatakuwa mema na mema yatakuwa maovu, (10) wale wafanyao hiana wataaminiwa na waaminifu watafikiriwa kuwa si waaminifu;na mwongo atasadikiwa,na msema kweli atahesabiwa mwongo. (11) Wakati huo kutakuwapo na utawala wa wanawake, (12) Masuria watashauriwa, (13) na watoto watakaa juu ya mimbar, (14) udanganyifu utahesabiwa kuwa ni uerevu (15) na Zaka itakuwa ni kama kutozwa faini;na mateka ya vita (yaani mali ya ummah) yatakuwa kama ni mali ya mtu binafsi; na mtu atakuwa mjeuri kwa wazazi wake na atakuwa mwema kwa marafiki zake, (16) na wakati huo kutatokea na nyota zenye mikia (comets)."

Salman akasema: "Haya yatatokea, ewe Mtume wa Allah swt?"

Mtume Mtukufu s.a.w.w. akasema: "Ndiyo, naapa kwa Aliyonayo roho yangu mkononi mwake."

"Ewe Salman! (17) wakati huo mwanamke atakuwa mshiriki wa mumewe katika biashara, (18) na mvua itakuwa moto sana (19) na watu wema watabaki katika huzuni; na masikini hawata heshimiwa; na wakati huo masoko yatakaribiana, (20) Tena huyu atasema,"Mimi sikuuza chochote, na yule atasema, "Mimi sikupata faida yoyote." Kwa hivyo hutamkuta mtu yeyote asiyemlalamikia Allah swt.
"Ewe Salman! (21) tena itatokea iwapo watu watawazungumzia watawala wao, watawaua, na ikiwa watanyamaza kimya, watanyang'anywa mali yao, watanyimwa heshima zao, watamwaga damu yao na mioyo ya watu itajaa woga;kisha hutamwona mtu yeyote ila atakuwa mwoga,mwenye khofu, ametishika na ameshstushwa"

"Ewe Salman! (22) Bila shaka wakati huo mambo fulani yataletwa kutoka Mashariki (23) na mambo fulani yataletwa kutoka Magharibi, (24) Basi ole kwa watu walio dhaifu (wa imani) katika Ummah wangu kutokana na hayo; Ole ya Allah swt iwe kwa hayo. Wao hawatakuwa na huruma juu ya wadogo wao, wala hawatamsamehe yeyote aliyefanya kosa. Miili yao itakuwa ya wanadamu, lakini mioyo yao itakuwa ya mashetani."

"Ewe Salman! (25) Wakati huo wanaume watawaashiki wanaume, (26) na wanawake watawaashiki wanawake; (27) na watoto wa kiume watapambwa kama wanawake; (28) na wanaume watajifanya kama wanawake(29) na wanawake wataonekana kama wanaume; (30) na wanawake watapanda mipando (31) Hapo tena patakuwepo laana ya Allah swt juu ya wanawake wa Ummah wangu."

"Ewe Salman! (32) Bila shaka wakati huo Misikiti itapambwa (kwa dhahabu n.k.) kama inavyofanywa katika masinagogi na makanissa, (33) na Quran zitapambwa (kwa nakshi na rangi za kupendeza n.k.) (34) na minara (ya misikiti) itakuwa mirefu; na safu za watu wanaosimama katika sala zitazidi, lakini nyoyo zao zitachukiana na maneno yao yatatofautiana."

"Ewe Salman! (35) Wakati huo wanaume watatumia mapambo ya dhahabu; kisha watavaa hariri,na watatumia ngozi za chui."

"Ewe Salman! (36) Wakati huo riba itakuwako, (37) na watu wata-fanyia biashara kwa kusemana na rushwa (38) na dini itawekwa chini, na dunia itanyanyuliwa juu."

"Ewe Salman! (39) Wakati huo talaqa zitazidi (40) na mipaka ya Allah swt hayatasimamishwa (41) Lakini hayo hayatamdhuru Allah swt."

"Ewe Salman! (42) Wakati huo watatokea wanawake waimbaji, (43) na ala za muziki (44) na wabaya kabisa watawatawala Ummah wangu."

"Ewe Salman! (45) Wakati huo matajiri katika Ummah wangu watakwenda Kuhiji kwa matembezi, na walio wastani kwa biashara, na masikini kwa kujionyesha. (46) Hivyo basi wakati huo watakuwapo watu ambao watajifundisha Quran si kwa ajili ya Allah swt na wataifanya Quran kama ala ya muziki. (47) Na watakuwapo watu ambao watasoma dini si kwa ajili ya Allah swt (48) na idadi ya wanaharamu itazidi (49) watu wataiimba Quran, (50) na watu watavamiana kwa uroho wa kidunia."

"Ewe Salman! (51) Haya yatatokea wakati heshima zitakapo- ondoka,na madhambi yatatendwa (52) na watu waovu watakuwa na uwezo juu ya watu wema, (53) na uongo utaenea na mabishano (matusi) yatatokea (54) na umasikini utaenea, (55) na watu watajiona kwa mavazi yao (56) na itakuwepo mvua wakati si wake (57) na watu watacheza dama, kamari na Ala za muziki, (58) na hawatapenda kuhimizana mema wala kukatazana maovu (59) na kwa ajili hali itakavyokuwa hata itafikia wakati huo kuwa Muumin atakuwa na heshima ndogo kuliko hata mjakazi (60) na wanaosoma na wanaotumia wakati wao katika kumwabudu Allah swt watalaumiana. (61) Hao ndio watu watakaoitwa wachafu na wanajisi katika Ufalme wa mbinguni."

"Ewe Salman! (62) Wakati huo matajiri hawataogopa chochote isipokuwa mtu masikini; hadi kwamba masikini wataendelea kuomba kati ya ijumaa mbili, na hawatamwona mtu yeyote wa kutia chochote mikononi mwao."

"Ewe Salman! (63) Wakati huo itazungumzwa Ruwaibidhah."

Salman akauliza: "Ni nini Ruwaibidhah ? Ewe Mtume wa Allah swt, baba na mama yangu wawe fidia kwako."

Mtukufu Mtume s.a.w.w. akajibu: (64) "Watu fulani watazungumza kuhusu mambo ya watu ambayo hayakuwahi kuzungumzwa namna hii zamani. (65) Tena baada ya muda mchache machafuko yatatokea duniani, na kila nchi itafikiri kuwa machafuko yapo katika nchi yao tu."

(66) "Watabaki katika hali hiyo kwa muda ambao Allah swt atapenda wabaki; (67) kisha ardhi itatapika vipande vya moyo wake dhahabu, fedha na madini mengineyo; (Hapo Mtume s.a.w.w.) alinyosha kidole chake penye nguzo, na akasema:"Kama hizi (kwa ukubwa), lakini siku hiyo dhahabu wala fedha hazitamsaidia mtu yeyote. Na hii ndiyo maana ya maneno ya Allah swt 'Hakika dalili Zake zimekuja.'

Zipo habari zingine zilizoelezwa katika vitabu vinginevyo kwa kupitia Jabir Ibn Abdullah Ansari, ambavyo ninazitaja:
"Ewe Salman! Wakati huo (1) Wazee watajitumbukiza katika mambo ya ushirikina na uchawi, (2) ghiba ndiyo itakuwa mazungumzo yenye kupendeza, (3) mali iliyopatikana kwa njia za haramu, itachukuliwa kama ndiyo neema, (4) wazee hawatakuwa na mapenzi ya wadogo na vile vile wadogo hawatawajali wazee na kuwaheshimu (5) Islam itabakia kwa jina tu kwani wafuasi wake hawatakuwa wakifuata maadili na maamrisho yake, (6) Kimbunga kikubwa cha rangi nyekundu kitatokezea mbinguni na kutaanguka mawe kutoka mbinguni (7) nyuso zitakuwa za kuchukiza (8) kutakuwa na mitetemeko na kuporomoka kwa ardhi kila mara.

Hapo Sahaba walimwuliza Mtume s.a.w.w., "Ewe Mtume wa Allah swt, je lini yatakapotokea hayo yote?" (pamoja na nishani na dalili za hapo juu, baadhi zimeongezeka hapa chini)

Mtume s.a.w.w. aliwajibu: (1) "Watu watakuwa watumwa wa shahwa au matamanio yao, (2) watu watakuwa walevi wa kupindukia kwani matumizi ya ulevi utakithiri na utakuwa ukipatikana kwa udhahiri bila ya watu kuona aibu ya aina yoyote, (3) Wanaume watakuwa wakiwatii wake zao, (4) jirani atakuwa wakiwaudhi na kuwatesa majirani wenzake, (5) Wakubwa hawatakuwa watu wenye huruma, mioyo yao itakuwa imejaa kwa maonevu, (6) vijana hawatakuwa na heshima (7) watu watajenga majumba imara na marefu mno, (8) wafanyakazi watadhulumiwa haki zao, (9) ushahidi wa kiuongo utachukuliwa kuwa wa kawaida, (10) ndugu atakuwa akimwonea wivu ndugu yake halisi (11)watu watakaokuwa wakifanya biashara kwa ushirika, basi watakuwa daima wakifikiriana mbinu za kumdhulumu mwenzake, (12) mambo ya zinaa yatakuwa kama kawaida kwani yatatendeka na kusikika pia.(13) ile mioyo ya kutaka kusaidia watu wengine itakuwa imetoweka, (14) Maasi na dhuluma itaongezeka kupita kiasi, (15) matumbo ya watu itachukuliwa kuwa ndiyo miungu yao,kwani hawatajali kiwevyo, ilimradi wapate chochote kile, (16) wanawake watakuwa wakitawala akili za wanaume na watakuwa wakiwaendesha wanaume vile watakavyo wao, (17) kutatokea Maulamaa au wanazuoni waovu kabisa kwani watajionyesha kuwa ni wacha Mungu na wenye ilimu, ambapo kwa hakika watakuwa waroho wa mali ya dunia tu."

Hapo Mtume Mtukufu s.a.w.w.liwaonya: "Kumbukeni,wakati kama huo utakapokuja, basi Allah swt atatumbukiza watu katika balaa za aina nne, (1) kutawaliwa na watawala dhalimu (2) ukame na vitu vya matumizi ya kila siku kuwa bei ghali yaani kupanda kwa maisha, (3) dhuluma za watawala (4) kuabudu miungu."

Sahaba waliposikia hayo walishtushwa na kuuliza: "Ewe Mtume wa Allah swt! Je kweli kuwa Mwislamu atakuwa akiabudu miungu na masanamu?"

Mtume s.a.w.w. aliwajibu: "Naam! Kwao mapesa yatakuwa kama miungu kwani watakuwa wakiziabudu kupindukia kiasi."

Kwa hakika sisi tunayashuhudia haya yote yakitokea ambayo Mtume s.a.w.w. amekwisha bashiri karibu karne kumi na nne zilizokwishapita. Imam Ali a.s. katika khutba yake ijulikanayo kama Al-Bayan anaelezea ubashiri kwa undani zaidi. Wasomaji wenye kutaka kupata habari zaidi wanaweza kutazama (1) Yanabi-ul-Muwaddah (2) Basharat-ul-Islam, Sayyid Mustafa Ali-Sayyid Haider al-Kazami, chapa ya Baghdad.
.

Saturday 1 November 2014

Hukmu Ya Kufunga Ijumaa Ikiwa Ni Siku Ya 'Arafah Au 'Aashuraa


SWALI LA KWANZA:
Assalaam 'Alaykum,
Shukurani zetu kwa kutujuilisha muandamo wa mwezi,
Pia nilikuwa nina masuala machache kuhusu  mwezi huu.  Jee tunaweza kufunga Arafa Ijumaa peke yake? au ni vizuri tufunge na Alhamis ili tuepuka kufunga siku ya Ijumaa pekee na kupata fadhila za Alhamis??
Pia kuna ushahidi wowote wa kufunga siku tisa za mwanzo za mfungo tatu (Hijja) kama ilivyozoeleka na wengi
Jazaka Allah Khayra
SWALI LA PILI:
Je inafaa kufunga Ijumaa ikiwa itaangukia ni siku ya tarehe 10 Muharram (Ashura)?
 




JIBU:
Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu 'anhum)  na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.
Mas-ala ya kufunga siku ya Ijumaa pekee au Jumamosi pekee zinapoangukia siku zilizotajwa kuwa ni siku za kufunga kama 'Arafah na 'Ashuraa, yana ikhtilaaf baina ya Maulamaa. Kuna waliosema kuwa inafaa kutokana na fadhila zilizotajwa katika kufunga siku hizo na kuna waliopinga kabisa kutokana na Hadiyth za Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) 
Makatazo ya Kufunga siku ya Ijumaa:

 عن أَبِي هُرَيْرَةَ رَضِيَ اللَّهُ عَنْهُ قَالَ سَمِعْتُ النَّبِيَّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ يَقُولُ : (( لا يَصُومَنَّ أَحَدُكُمْ يَوْمَ الْجُمُعَةِ إِلا يَوْمًا قَبْلَهُ أَوْ بَعْدَهُ )) رواه البخاري   ومسلم
Kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allahu 'anhu) ambaye amesema: 'Nimemsikia Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: ((Asifunge yeyote siku ya Ijumaa ila ikiwa (akiunganisha) siku kabla yake au baada yake)) [Al-Bukhaariy na Muslim]
Vile vile,
  عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رَضِيَ اللَّهُ عَنْهُ عَنْ النَّبِيِّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ : (( لا تَخْتَصُّوا لَيْلَةَ الْجُمُعَةِ بِقِيَامٍ مِنْ بَيْنِ اللَّيَالِي وَلَا تَخُصُّوا يَوْمَ الْجُمُعَةِ بِصِيَامٍ مِنْ بَيْنِ الْأَيَّامِ إِلا أَنْ يَكُونَ فِي صَوْمٍ يَصُومُهُ أَحَدُكُمْ ))  مسلم
Kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allahu 'anhu) kwamba Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Msiufanye usiku wa Ijumaa kuwa ni mahsusi kwa Qiyaam (Kisimamcho cha kuswali usiku) baina ya nyusiku nyingine na wala msiifanye siku ya Ijumaa ni makhsusi kwa kufunga baina ya siku nyingine isipokuwa ikiwa ni miongoni mwa siku anazofunga mmoja wenu)) [Muslim]

عَنْ جُوَيْرِيَةَ بِنْتِ الْحَارِثِ رَضِيَ اللَّهُ عَنْهَا أَنَّ النَّبِيَّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ دَخَلَ عَلَيْهَا يَوْمَ الْجُمُعَةِ وَهِيَ صَائِمَةٌ فَقَالَ ((أَصُمْتِ أَمْسِ)) قَالَتْ لا قَالَ ((تُرِيدِينَ أَنْ تَصُومِي غَدًا)) قَالَتْ لا قَالَ ((فَأَفْطِرِي)) وَقَالَ حَمَّادُ بْنُ الْجَعْدِ سَمِعَ قَتَادَةَ حَدَّثَنِي أَبُو أَيُّوبَ أَنَّ جُوَيْرِيَةَ حَدَّثَتْهُ فَأَمَرَهَا فَأَفْطَرَتْ   رواه البخاري
Kutoka kwa Juwariyah bin Al-Haarith (Radhiya Allahu 'anhumaa) kwamba Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliingia kwake siku ya Ijumaa naye akiwa amefunga akasema: ((Je ulifunga jana?)) Akasema: "Hapana". Akasema: ((Je unataka kufunga kesho?)) Akasema: "Hapana". Akasema: ((Basi fungua)) [yaani usifunge] Na kasema Hammad bin Al-Ja'd 'Nimemsikia Qataadah akisema, Abu Ayyuub kaniambia kuwa  Juwayriyah alimhadithia  (alivyozungumza na Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ) akamuamrisha afungue . [Al-Bukhaariy]

Makatazo ya kufunga siku ya Jumamosi
عَنْ عَبْدِ اللَّهِ بْنِ بُسْرٍ عَنْ أُخْتِهِ أَنَّ رَسُولَ اللَّهِ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ : (( لا تَصُومُوا يَوْمَ السَّبْتِ إِلا فِيمَا افْتَرَضَ اللَّهُ عَلَيْكُمْ ، فَإِنْ لَمْ يَجِدْ أَحَدُكُمْ إِلا لِحَاءَ عِنَبَةٍ ، أَوْ عُودَ شَجَرَةٍ فَلْيَمْضُغْهُ))      وأبو داود  وابن ماجه صححه الألباني في "الإروا
Kutoka kwa 'Abdullahi bin Busr kutoka kwa kaka yake kwamba Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kasema: ((Msifunge siku ya Jumamosi isipokuwa ikiwa mmefaridhiwa na Allah kwenu. Ikiwa mtu hakupata chochote cha kula isipokuwa jani la zabibu au gome la mti, basi alitafune)) [Abu Daawuud na Ibn Maajah na kaipa daraja ya sahiyh Shaykh Al-Albaaniy katika Al-Irwaa]
Bonyeza katika kiungo kifuatacho chenye maelezo zaidi kuhusu hukmu ya funga ya Jumamosi:
 Hukumu Ya Kufunga Siku Ya Jumamosi Pekee

Kauli za Maulamaa kuhusu mas-ala haya:
Ibn Qudaamah kasema: "Ni makruuh kuipwekesha siku ya kufunga Ijumaa ila ikiwa imeangukia katika siku ambayo ni kawaida yake mtu kufunga kama vile Swawm ya siku moja na ya pili kuacha (Swawm ya Nabii Daawuud) ikaangukia Swawm kama hiyo katika siku ya Ijumaa, au kwa mwenye tabia ya kufunga siku ya mwanzo au ya mwisho au ya katikati katika mwezi" [Al-Mughni, Mjadala 3 Uk. 53]
An-Nawawy kasema: "Wafuasi wetu (yaani Mashaafi'iy) wamesema: Ni makruuh kuipwekesha siku ya Jumamosi kufunga. Lakini mtu anaweza kuunga siku kabla yake au baada yake. Au ikiwa imeangukia katika siku za kawaida yake kufunga, au kama kaweka nadhiri mfano; ni siku ambayo mpenzi wake amepona, au siku 'fulani' atakayorudi, na ikatokea kuwa siku hiyo ni Ijumaa basi sio makruuh kufunga" [Al-Majmuu-sharh al Muhadhadhab, Mjadala 6, Uk. 479]
Shaykhul-Islaam amesema: "Sunnah inasema kuwa ni makruuh kupwekesha (mwezi wa ) Rajab kwa kufunga na ni makruuh kuipwekesha Ijumaa (kwa kufunga)" [Al-Fataawa al-Kubra, Mjadala 6, Uk. 180]
Shaykh Ibn 'Uthaymiyn kasema: "Ama Ijumaa, sio Sunnah kufunga siku hii, na ni makruuh kuipwekesha kwa ajili ya kufunga" [Ash-Sharh al-Mumti', Mjadala 6, Uk.465]
Tukiacha makatazo hayo ya kuipwekesha siku ya Ijumaa kufunga, mtu anaweza kufunga ikiwa ni siku ya kawaida yake mtu kama mwenye kufunga Ayyaamul-Biydhw (tarehe 13, 14, 15 ya kila mwezi wa Kiislam) mwenye kutaka kufunga 'Arafah na ikaangukia kuwa ni Ijumaa.
Vile vile ikiwa mtu anataka kulipa deni lake la Ramadhaan anaweza kufunga Ijumaa peke yake. Hii ni kutokana na Fataawa inayosema: "Inaruhusiwa Muislamu afunge Ijumaa peke yake ikiwa ni funga ya deni la Ramadhaan" [Fatwa al-Lajnah ad-Daaimah, Mjadala 10, Uk. 347] 
Kwa hiyo ikiwa ni 'Arafah au 'Ashuraa imeangukia kuwa ni Ijumaa inaruhusiwa kufunga kwa sababu nia ni ya kufunga 'Arafah au 'Ashuraa na sio kufunga Ijumaa. Vilevile ikiwa mtu atafunga na siku ya Alkhamiys, itakuwa ni jambo jema zaidi kwani atakuwa amepata fadhila zaidi ya moja;
  1. Fadhila ya kutekeleza Sunnah ya kuifunga siku hiyo kama alivyokuwa akifanya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kufunga Jumatatu na Alkhamiys.
  2. Fadhila ya kufunga siku ya kabla ya siku ya Ijumaa, na hivyo ni kuondosha shaka yoyote inayohusiana na kuipwekesha Ijumaa kwa Swawm.
  3. Fadhila ya kutenda kitendo kizuri katika masiku kumi ya Dhul-Hijjah kama ilivyosisitizwa katika Sunnah. 
Alhidaaya inawasisitiza sana ndugu Waislam mfunge siku ya Alkhamiys na Ijumaa .
Ama kuhusu swali lako la pili kuhusu kufunga siku 9 za Dhul-Hijjah, jibu lake liko tayari kwenye kiungo kifuatacho:
Inafaa Kufunga Siku 9 Za Dhul-Hijjah?
Tunawakumbusha tena waulizaji, muwe mnatembelea kitengo cha maswali na majibu kwenye tovuti kabla hamjauliza maswali yenu. Kufanya hivyo kunawasaidia kupata majibu ya maswali mnayotaka kuuliza ambayo tayari yashajibiwa, na kadhalika kutatuwepesishia sisi na kazi za ziada In Shaa Allaah.
Yanayohusiana na Swawm ya Jumamosi yanapatikana katika kiungo kifuatacho:
Hukumu Ya Kufunga Siku Ya Jumamosi Pekee Na Inapoangukiwa Siku Ya 'Arafah Au 'Aashuraa

Na Allaah Anajua zaidi

Thursday 30 October 2014

Mambo Ya Kufanya Siku Ya Ijumaa


Ijumaa hii tunaelezea utukufu wa siku hii kwa kujulisha mambo yanayotupasa kuyafanya yenye fadhila  na thawabu nyingi.

Kukoga (Ghuslu) Ni Wajibu

حديث أَبِي سَعِيدٍ الْخُدْرِيِّ، عَنِ النَّبِيِّ صلى الله عليه وسلم قَالَ: الْغُسْلُ يَوْمَ الْجُمُعَةِ وَاجِبٌ عَلَى كُلِّ مُحْتَلِمٍ ( أخرجه البخاري)   
Kutoka kwa Abu Sa'iyd Al-Khudriy ambaye alisema: Mtume صلى الله عليه وسلم  kasema  Ghuslu ( kukoga kwa kujitia twahara) siku ya Ijumaa ni wajibu kwa kila Muislamu aliyebaleghe.  [Al-Bukhaariy]

Inapendekezwa kwa kila anayekwenda kuswali kujisafisha, kupiga mswaki, kujitia mafuta mazuri (isipokuwa mwanamke) na kuvaa nguo iliyo nzuri kabisa. Muislamu akitimiza adabu ya Swalah ya Ijumaa hufutiwa madhambi yake ya wiki.

عن سلمان رضي الله عنه قال: قال رسول الله  صلى الله عليه  وسلم  لا يغتسل رجل يوم الجمعة، ويتطهر ما إستطاع من طهر، ويدّهن من دهنه، أو يمس من طيب بيته، ثم يخرج فلا يفرق بين إثنين، ثم يصلي ما كتب له، ثم ينصت إذا تكلم الإمام، إلا غفر له ما بينه وبين الجمعة الأخرى) رواه البخاري(

Kutoka kwa Salmaan رضي الله عنه  ambaye alisema:  Kasema Mtume صلى الله عليه وسلم "Muislamu atakayekoga (Ghuslu)  siku ya Ijumaa, akajisafisha vizuri awezavyo, akatia rangi (nywele zake) (isiyo nyeusi),  au akajipaka mafuta mazuri  aliyonayo nyumbani kwake, kisha akaenda Msikitini bila ya kufarikisha (kuwapangua akipita) watu wawili (ambao wameshakaa kitako msikitini), akaswali aliyofaridhishwa, kisha akasikiliza  (khutbah) kimya, hufutiwa madhambi yake yaliyo baina ya Ijumaa hiyo na Ijumaa ijayo.  [Al-Bukhaariy na Ahmad]

Swalah Ya Ijumaa 

Allaah سبحانه وتعالى Ametuamrisha kwenda kuswali Swalah ya Ijumaa
يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا إِذَا نُودِي لِلصَّلَاةِ مِن يَوْمِ الْجُمُعَةِ فَاسْعَوْا إِلَى ذِكْرِ اللَّهِ وَذَرُوا الْبَيْعَ ذَلِكُمْ خَيْرٌ لَّكُمْ إِن كُنتُمْ تَعْلَمُونَ

“Enyi mlioamini! Ikiadhiniwa Swalah siku ya Ijumaa, nendeni upesi kwenye dhikri ya Allaah, na acheni biashara. Hayo ni bora kwenu, lau kama mnajua” [Al-Jumu’ah 62: 9]

Ni wajibu kwa kila mwanamme Muislamu kwenda kuswali Ijumaa, na hatari ya  kutokwenda kuswali bila ya kuwa na sababu iliyoruhusu shari’ah ni kuwa  Allaah سبحانه وتعالى  humpiga muhuri mtu  moyoni  mwake, kama katika Hadiyth sahihi ifuatayo:

 قال رسول الله صلى الله عليه وسلم قال: من ترك ثلاث جمع تهاونا طبع الله على قلبه (رواه أحمد وأصحاب السنن،)

Kasema Mtume صلى الله عليه وسلم : Atakayeacha (kuswali Swalah ya) Ijumaa mara tatu bila ya sababu yeyote, Allaah سبحانه وتعالى humpiga muhuri katika moyo wake.” [Ahmad na wapokezi wa Hadiyth wengine wenye vitabu vya ‘Sunnan’]

Kupigwa muhuri huo inamaanisha kwamba Allaah سبحانه وتعالى Ameshampa chapa huyu mtu kuwa ni 'Aasi na amekwishatumbukia katika makemeo ya Allaah سبحانه وتعالى  kwamba   ni katika walioghafilika  kama alivyotutahadharisha Mtume صلى الله عليه وسلم :

حديث ابن عمر وأبي هريرة رضي الله عنهما المخرج في صحيح مسلم من أنهما سمعا رسول الله صلى الله عليه وسلم يقول على أعواد منبره: لينتهين أقوام عن ودعهم الجمعات أو ليختمن الله على قلوبهم ثم ليكونن من الغافلين

Kutoka kwa Ibn 'Umar na Abu Hurayrah رضي الله عنهما kwamba wamemsikia Mtume صلى الله عليه وسلم akisema: “Wasiohudhuria  Swalah ya Ijumaa  wabadilishe  mtindo wao huo au sivyo Allaah سبحانه وتعالى Atawapiga mihuri katika nyoyo zao  na watakuwa  miongoni wa walioghafilika.” [Muslim]


Kufika Mapema Msikitini   

Kila atakapofika mtu mapema msikitini huwa amepata daraja Fulani na muhimu kabisa ni kufika kabla ya khutba kuanza, akichelewa mtu kufika akakosa khutba atakuwa amekosa Swala ya Ijumaa

حديث أَبِي هُرَيْرَةَ رضي الله عنه، أَنَّ رَسُولَ اللهِ صلى الله عليه وسلم قَالَ: مَنِ اغْتَسَلَ يَوْمَ الْجُمُعَةِ غُسْلَ الْجَنَابَةِ ثُمَّ رَاحَ فَكَأَنَّمَا قَرَّبَ بَدَنَةً، وَمَنْ رَاحَ فِي السَّاعَةِ الثَّانِيَةِ فَكَأَنَّمَا قَرَّبَ بَقَرَةً، وَمَنْ رَاحَ فِي السَّاعَةِ الثَّالِثَةِ فَكَأَنَّمَا قَرَّبَ كَبْشًا أَقْرَنَ، وَمَنْ رَاحَ فِي السَّاعَةِ الرَّابِعَةِ فَكَأَنَّمَا قَرَّبَ دَجَاجَةً، وَمَنْ رَاحَ فِي السَّاعَةِ الْخَامِسَةِ فَكَأَنَّما قَرَّبَ بَيْضَةً، فَإِذَا خَرَجَ الإِمَامُ حَضَرَتِ الْمَلاَئِكَةُ يَسْتَمِعُونَ الذِّكْرَ (أخرجه البخاري )

Kutoka kwa Abu Hurayrah رضي الله عنه ambaye alisema:  Mtume صلى الله عليه وسلم kasema: “Atakayekoga (Ghuslu) siku ya Ijumaa kisha akaenda Msikitini, itakuwa kama mfano ametoa (kafara ya) ngamia. Akienda  saa ya pili yake, itakuwa kama katoa (kafara ya) nġ’ombe.  Akienda saa ya tatu yake, itakuwa kama katoa (kafara ya) kondoo mwenye pembe. Akienda saa ya nne yake, itakuwa kama katoa   kuku. Akienda saa ya tano yake itakuwa kama katoa yai. Imaam akifika, Malaika watatoka kuja kusikiliza dhikr” [Al-Bukhaariy]


Surah Za Kusoma Siku Ya Ijumaa

·         Suratul Kahf

عن أبي سعيد الخدري رضي الله عنه أن النبي صلى الله عليه  وسلم  قال: من قرأ سورة الكهف يوم الجمعة أضاء له من النور ما بين الجمعتين ( رواه الترمذي)
Kutoka kwa Abu Sa'iyd Al-Khudriy رضي الله عنه ambae alisema: Kasema Mtume صلى الله عليه وسلم : “Atakayesoma Suratul-Kahf siku ya Ijumaa atakuwa katika mwangaza baina ya Ijumaa mbili.”  [At-Tirmidhiy]

Pamoja na kusemwa kuwa Hadiyth hiyo imetoka kwa Mtume صلى الله عليه وسلم, lakini Wanachuoni wa Hadiyth wengi wamesema ni Hadiyth 'Mawquuf' ambayo haijaelezwa na Mtume bali ni kutoka kwa Maswahaba, na kwa nyongeza ya neno 'atakayeisoma Ijumaa' haikuthibiti kwa Mtume, na maelezo hayo hapo juu ni ya kutoka kwa Abu Sa'iyd Al-Khudriy na yeye ndiye aliyekuwa akiisoma Surah hiyo katika siku ya Ijumaa, na Wanachuoni wanasema kuwa maadam Maswahaba walikuwa wakiisoma Surah hiyo siku ya Ijumaa, basi hakuna neno kuisoma Ijumaa, japo kuisoma siku yoyote ni sawa na mtu atapata fadhila zilizotajwa kwenye Hadiyth hiyo. Ama kutoka kwa Mtume صلى الله عليه وسلم, Wanachuoni wamesema haikuja na lafdhi ya 'kuisoma Ijumaa', bali imekuja kwa ujumla wake wa kuisoma Surah hiyo siku yoyote ile kama ilivyokuja hapa chini:

((وقال صلى الله عليه وسلم : من قرأ سورة الكهف كما أنزلت كانت له نورا يوم القيامة ، من مقامه إلى مكة ، و من قرأ عشر آيات من آخرها ثم خرج الدجال لم يضره ....))  صححه الألباني في سلسلة الأحاديث الصحيح 
((Kasema Mtume صلى الله عليه وسلم atakayesoma Suratul-Kahf kama ilivyoteremshwa, atakuwa na mwangaza siku ya Qiyaamah pale alipo mpaka Makkah, na atakayesoma Aya kumi za mwisho kisha akitokea Dajjaal hatomdhuru)) [Swahiyh kama alivyoeleza Shaykh Al-Albaaniy katika Silsilatul-Ahaadiyth As-Swahiyhah]

·         Swalah ya Alfajiri

حديث أَبِي هُرَيْرَةَ رضي الله عنه، قَالَ: كَانَ النَّبِيُّ صلى الله عليه وسلم يَقْرَأُ فِي الْجُمُعَةِ، فِي صَلاَةِ الْفَجْرِ، آلَم تَنْزيلُ، السَّجْدَةَ، وَ هَلْ أَتَى عَلَى الإِنْسَانِ ( أخرجه البخاري)

Kutoka kwa Abu Hurayrah رضي الله عنه ambaye alisema:  Alikuwa Mtume صلى الله عليه وسلم  akisoma surah ya Alif-Laam-Tanziylu (Suratus Sajdah) na Hal-Ataa 'Alal-Insaan (Suratul Insaan)”  [Al-Bukhaariy]

·         Kumswalia Mtume صلى الله عليه وسلم

عن أوس بن أوس رضي الله عنه قال: قال رسول الله  صلى الله عليه  وسلم  إن من أفضل أيامكم يوم الجمعة، فأكثروا علي من الصلاة فيه، فإن صلاتكم معروضة علي  ) رواه أبو داود)
Kutoka kwa Aws Ibn Aws رضي الله عنه ambaye alisema:  Kasema Mtume صلى الله عليه وسلم : “Siku bora kabisa kwenu ni siku ya Ijumaa, kwa hiyo zidisheni kuniswalia,  kwani Swalah (kuniombea) zenu zinaonyeshwa (zinaletwa mbele yangu) kwangu.” [Abu Daawuud]
 

Usimuombe Muhammad, Bali Muombe Allaah

 
Waislamu sote tunakiri na kutamka kwa ndimi zetu kwamba Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ni Mtume wa mwisho, naye ni mbora wa viumbe, mwenye tabia bora za kupigiwa mfano na sisi tunawajibika kuzifanyia kazi.
 
Hata hivyo, juu ya hikmah zake, cheo na daraja alichonacho, hatustahiki hata kidogo kumuomba Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) katika lolote tunalohitajia kuliomba. Wala hatuwajibiki kuamini kwamba du’aa isiyopita transit kwake, haikubaliwi. Hilo sio sahihi katu, kwani Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) hakuwa malaaikah wala jamii isiyokuwa yetu sisi. Ni mwenzetu, mwenye maumbile sawa na sisi, kilichobadilika kutoka kwake ni kupokea wahyi tu.
 
Mola wetu, Anasema kwamba tumuombe Yeye, kwani Ndiye Anayezisikia du’aa zetu na malalamiko yetu:
 
{{Na waja Wangu watakapokuuliza khabari Zangu, waambie kuwa Mimi Nipo karibu. Naitikia maombi ya mwombaji anaponiomba. Basi na waniitikie Mimi, na waniamini Mimi, ili wapate kuongoka.)) [Al-Baqarah:186]
 
Pia Amesema:
 
{{Na Mola wenu Anasema: Niombeni nitakuitikieni.}} [Suratul-Ghaafir: 60]
 
Kwa upande wake, Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema kwamba tusimtukuze kama walivyomtukuza Manasara kwa Nabii ‘Iysaa hadi kumpa daraja na cheo sawa cha Uungu:
 
((Msinitukuze (kwa kunipandisha cheo kama cha Allaah) kama walivyomtukuza Manasara ‘Iysaa mwana wa Maryam, hakika mimi ni mja, kwa hiyo semeni mja wa Allaah na Mjumbe Wake.)) [Imepokewa na Al-Bukhaariy na Muslim]
 
Wala hawa Manasara hawakuishia hapo, nao pia wakajitukuza na kujipachika vyeo vya Unabii na Utume, na kujidai kuweza kuombwa na wanaadamu wenzao pamoja na kusamehe madhambi. Hayo kwetu yatabakia ni uzushi mkubwa na ni shirki iliyo wazi.
 
Kwa hapa, tunaomba tuzingatie kwamba du’aa yoyote inatakiwa kuelekezwa moja kwa moja, kiroho na kimatamshi kwake Muumba wala sio kwa Mtume. Tunaona ndani ya jamii zetu za Kiswahili, mtu anapojitoka, anapotokewa na tatizo la ghafla au mfano wa hayo; basi kauli ya mwanzo linalomjia mdomoni ni la kishirikina: Mtume! na mfano wa hayo.
 
Ewe ndugu yangu Muislamu, umesahau ya kwamba Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) hivi sasa ni maiti. Naye Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) hivi sasa ni maiti, asiyeweza hata kusikia maombi yetu, seuze kuweza kutuombea kwa Mola. Sasa iweje leo neno lako la mwanzo unapotokezewa na shida liwe Mtume!?
 
Na wengine wapo waliochupa mipaka, wakawapatia vyeo wanaowaita masharifu, mashekhe, mamufti, maqadhi, mawalii na kadhalika, wakawatumia kuzipitisha du’aa zao kwao. Ni ushirikina na uzushi ulioje. Utakuta kwenye du’aa zao wakisema: Kwa kuhudhuria Sayyiduna Muhammad, mawlaana, sharful-anbiyaa, wa shuyukhina, al-faatihah! Ujahili ulioje huu, Mola wetu yupo karibu kuliko mapigo ya mioyo yetu, ya nini kupata taabu kuzipitisha du’aa kupitia kwa viumbe vinavyotegemea rahmah zake?
 
Tunamalizia kwa kuzinasihi nyoyo zetu na za Waislamu wote, kuachana na aina hii ya shirki, kwani tutakuwa tunamuomba kiumbe badala ya kumuomba Muumba.
 

Kutafuta Elimu Ni Wajibu

Jibriyl (‘Alayhis Salaam) aliposhuka kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimtikisha na kumbana barabara akimuamuru kusoma kwa jina la Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala). Mola Ambaye Amemuumba mwanadamu kwa tone la damu na kumfunza kwa kutumia kalamu.
 
Iwapo kipenzi cha Mola Mlezi asiyejua kusoma wala kuandika ametikishwa namna hiyo, je sisi tutarajie nini katika kutafuta elimu? Wengi wa Waislamu ni wenye kwenda na kurudi bila ya kutilia mkazo elimu ya Kiislamu. Na kama Waislamu watasimama kihaki liLlaahi kuitafuta elimu, basi ndio itakuwa sababu ya kuondoka udhalilifu walionao Waislamu hivi sasa.
 
Katika baadhi ya miji ya Waislamu, utakuta kuna Misikiti chungu nzima lakini Madrasah zikiwa kidogo kweli kweli. Sasa hiyo Misikiti ikaswalishwe na kusomeshwa darsa na nani? Ingawa hizo Madrasah pia zipo na zimejaa taa na mazulia mazuri mazuri, lakini wanafunzi wake ni wachache kabisa. Kwanza Waislamu watilie mkazo kusoma na kusomesha, badaye ndio wasambazwe hao waliosoma ndani ya Misikiti. Na kwa bahati mbaya, hivi sasa Misikiti na Madrasah ni vitu viwili tofauti. Misikiti mingi inajengwa kwa ajili ya kuswalia tu, na Madrasah kwa ajili ya kusoma tu. Tumesahau ya kwamba Mtume aliujenga Msikiti ambao ndio kiini cha elimu ya Kiislamu na hivi sasa unatoa shahada za juu kabisa kwa wanafunzi.
 
Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipewa utume kwa kauli ya "Iqraa" iliyomo ndani ya Suratul-'Alaq na akaamrishwa kulingania kupitia aya za mwanzo za Suratul-Muddathir. Tunachojifunza hapa ni kwamba amri ya kusoma imekuja mwanzo kabla ya kulingania. Na bila ya shaka Mola Amemuamuru mwanaadamu kutafuta elimu kabla ya kumuamuru kumuelewa Mola Mwenyezi (elimu ya tawhiyd). Kwani kupitia elimu ndio atapata wepesi wa kumpwekesha Mwenyezi Mungu. Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anasema ndani ya Qur-aan:
 
{{Jua ya kwamba hakuna aabudiwaye kwa haki ila Mwenyezi Mungu.}} [Suratu-Muhammad: 19]
 
Amri ya Mola inayosema "jua" ina maana sawa na "soma". Kilichopo hapo ni kwamba kwanza tusome na ndani ya hiyo elimu tutaelewa kuwa hakuna aabudiwaye kwa haki ila Mwenyezi Mungu. Hii inatutambulisha kwamba amri ya kumtambua Mola ipo chini kulinganisha na amri ya kutafuta elimu.
 
Tuzingatie na tuelewe ule msemo wa Waarabu unaosema: "العلم من المعهد إلى العهد"
wenye maana kwamba elimu ni ya kutafutwa milele kuanzia chuoni hadi mwisho wa maisha yake mtu. Tusikate tamaa katika kutafuta elimu. Kwani elimu ni ngumu kuipata na ndio silaha yako hapa duniani na kesho Akhera iwapo utaitumia vyema. Hata unapofariki, warithi wako hawataipata kwani unaondoka nayo kama vile unavyoondoka na ‘amali zako. Watabaki kurithi hizo pumbao za dunia. Na kama umeisoma kisha ukaisomesha na kuwapatia manufaa watu, basi thawabu zake utaendelea kuzichuma hadi kaburini insha Allaah.
 
Tunamuomba Mola Atupatie fahamu ya Manabii na nyoyo zenye kuelewa mambo kwa wepesi kabisa. Atufunulie akili zetu kwa mambo yenye manufaa na kuzifunga akili zetu zisifahamu wala kuelewa hata kidogo yale yasiyo na manufaa. Aamiyn!

Ibilisi Hakati Tamaa

 
Imesimuliwa ya kwamba kulikuwa na mcha Mungu aliyependwa sana na watu wa wakati wake akiitwa Wadd. Alipofariki, swahiba zake walilizunguka kaburi lake huko Babylon kwa masikitiko makubwa. Ibilisi alipoona hilo, aliwashauri kumtengenezea sanamu ili wapate kumkumbuka.
 
Walikubaliana na hilo, hivyo likatengenezwa na kuwekwa mbele ya umma wa watu. Kizazi kilipokuja kuona namna sanamu la Wadd linavyotukuzwa, wakaamua kuweka sanamu hilo ndani ya kila nyumba. Baada ya kupita muda mrefu na pia kuondoka elimu ya Dini, watoto wa hao watu walikuja kuabudia masanamu hayo.
 
Kisa cha Wadd kinatudhihirishia ya kwamba hawakuanza kuabudia masanamu kwa ghafla moja tu. Walianza kidogo kidogo hadi kuingia kwenye shirki moja kwa moja. Na kisa hichi kinadhihirisha Qawl ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kwamba Ibilisi ni adui aliye wazi kabisa:
 
{{Hakika Shaytwaan kwa mwanadamu ni adui aliye dhahiri}} [17:53]
 
Ibilisi hana haraka ya kuwavuta viumbe na wala hakati tamaa, huanza kidogo kidogo na hatimaye kuwatumbukiza ndani ya dimbwi la maasi bila ya kujijua. Mfano mwengine ni wa Muislamu mwenye kusimamisha Swalah tano. Ibilisi huanza kumuondoshea hamu ya kufika Masjid mapema, baadaye humshughulisha ili asipate kuswali, huendelea kwa kuswali nyumbani na hatimaye huacha kabisa.
 
Maandishi ya SW kusimama kwa Subhaanahu Wa Ta’ala na SAW kuelezea Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam ni mambo mengine ambayo hapana budi kuyafikiria vizuri. Kwa hali hii, haitokuwa ajabu kuona kizazi kinachofuata kikitamka: Allaah Ess Dabal Yuu (SW) au Mtume Ess Eee Dabal Yuu (SAW).
 
Halikadhalika, mambo ya kusherehekea birthday hayana mnasaba ndani ya Diyn hii tukufu. Wanaswara wanayo birthday ya Yesu (Krismasi), Waislamu nao wakaweka birthday ya Mtume! Laa hawla! Jina la birthday likabadilishwa ili lipate lafdhi zile za Kiarabu na kuitwa Mawlid. Kwa mtindo huu, ndio tunaona sasa hata Waislamu hawaelewi kufunga Jumatatu wala Alkhamisi, Sunnah za Swalah ya dhuhaa na witri zote kaachiwa mwenyewe Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Wanasubiri Mfunguo sita waende kusoma hayo Mawlidi wakielewa kuwa ndio kumtukuza kipenzi chetu.
 
Yeye Ibilisi hamuachi mtu hadi mauti yamfike. Hivyo, haifai kusema kwamba ‘nitatubu baadaye’ au ‘nitaanza kuvaa hijabu nikifika umri kadhaa’. Kwani tunashuhudia ndani ya jamii zetu kizee cha kupindukia miaka 85 kikiwa kinaimba kwa matusi ya juu na kunywa pombe mithili ya kijana wa miaka 20!
 
 
Vipi tutaepukana naye?
 
Kuna njia mbili kuu za kuepukana na Ibilisi ambazo ni:
 
Kwanza ni kufuata amri za Allaah. Hii ni pamoja na kukumbuka wasia wa Mola Mlezi wa kutomfuata Ibilisi na badala yake kumuabudia Yeye pekee kwani hii ndiyo njia iliyonyoka:
 
{{Je, Sikukuagizeni (Sikukuusieni) enyi wanaadamu kuwa msimuabudu Shaytwaan? Hakika yeye ni adui aliye dhahiri kwenu. Na ya kwamba niabuduni Mimi. Hii ndiyo njia iliyonyoka.}} [36:60-61]
 
Pili ni kushikamana kwa hali zote katika mwendo wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) pamoja na Makhalifa wake waadilifu:
 
"... Basi shikamaneni na Sunnah zangu na Sunnah za Makhalifa wangu waongofu, kamataneni nazo kwa magego (shikamaneni nazo kwa nguvu zote)" [Abu Daawuud 4607, At-Tirmidhy 2676 Nayo ni Hadiyth Nzuri Sahihi]
 
Huyo ndie Ibilisi ambaye Radhi za Allaah zipo mbali na yeye. Athari ya kumfuata Ibilisi ni mbaya mno, kwani hutuwekea kizuizi baina yetu na Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala). Na kila mwenye kumfuata yeye ataelekea kwenye njia potofu.
 

Akili Zinapotawaliwa...Daima Hazitofanikiwa


Uislamu ni dini ambayo imekamilika kwa namna ambayo yeyote aweza kuifuata na kuisimamisha. Sio dini ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) wala Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘Anhum) pekee. Bali ni dini ya Ulimwengu mzima. Historia yaonesha kwamba Uislamu ulikuwa na nguvu kubwa enzi za nyuma kuliko hali tuliyokuwa nayo sasa. Hivyo, kama misingi hii inaweza kufuatwa na wasiokuwa Waislamu, kwanini Waislamu wenyewe washindwe kuzifuata?

Yaonesha dhaahir kwamba hila zinabuniwa, kutekelezwa na kufanikiwa katika kuangusha mila na desturi za Kiislamu kwani hakuna taifa wala Kiongozi mmoja wa kuwaunganisha Waislamu. Uislamu ni dini yenye Shahadah moja, Qiblah kimoja, Mfungo wa Swawm mmoja na Hijjah moja tu. Hivyo yaonesha wazi wazi kuwa ni dini ya mshikamano, lakini bado haitendewi haki namna inavyotakiwa. Kilio kikubwa ni kwamba, juu ya kuwepo nguzo hizi za kutuunganisha lakini hatuna kauli moja wala vitendo vyenye muelekeo mmoja katika mila na desturi zetu. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema kwamba Waumini ni wamoja na wanafanana na jengo:
((Hakika Muumini Kwa Muumini ni kama jengo, wanashikamana pamoja)) Akafungamisha Vidole vyake pamoja [Al-Bukhaariy na Muslim]
Badala yake, tunaiendea kinyume Hadiyth hiyo na kuwa pamoja na hila za Magharibi katika kuupiga vita Uislamu.

Tunashuhudia kuwepo mlolongo mkubwa wa shughuli za kuwadumaza Waislamu ili wasiwe ni wenye kuona mbali na kuweza kutoa mawazo ambayo yatakwenda kinyume na misingi ya kibepari. Misingi hii ya kibepari ni ile ambayo inamtoa thamani mwanamke, kuwadhalilisha viumbe kwa neno la demokrasia na uhuru. Imekuwa hii dunia ni uwanja wa fujo tu, mpate mpatae, mshike mshike. Hajulikani nani muadilifu wala mtenda madhambi.

Waislamu tumefanana na mbu kukosa kumbukumbu. Kwani hatukumbuki namna walivyopigwa vita, kubakwa, kuuawa na kuteswa Waislamu waliopo Afghanistan kwa neno la ‘ugaidi’, Iraaq kwa neno la ‘dikteta’ na Chechnya kwa neno la ‘usalama’. Yote haya yanafanywa kwa nani na kwa ajili ya kupata nini? Hakuna chengine kinachogombaniwa hapa ila kuhodhi mamlaka chini ya mkono mmoja wenye nguvu za kushika na kuachia.

Utawala huu wa kimabavu duniani bado unaendelea, na unalenga zaidi kunufaisha nchi za Magharibi. Mfano mzuri tu ni namna Waislamu wanavyoshughulishwa mno na mambo ya anasa na kupoteza muda.

Mechi za mpira ni moja kati ya zana kuu zinazotumiwa kuupiga vita Uislamu. Kama hatutakuwa makini, daima tutakuwa wapofu kwa kuhifadhi majina ya wachezaji pamoja na historia ya klabu za mpira. Huku tukiacha nyuma Siyrah tukufu ya Uislamu pamoja na matendo sahihi ya Uislamu. Hatukai kufikiria namna mzunguko wa mechi hizi zinavyopokezana, mechi zisizokuwa na mwisho kana kwamba wanaoshuhudia pia ni wenye kufanya mazoezi ya mpira.

Kuna mechi za ligi kuu ndani ya mikoa, nchi nzima, nchi jirani pamoja na Afrika nzima. Ukipiga hesabu utapata takriban sio chini ya mechi 100 kwa mwaka mzima. Tukitoka Afrika, tunakwenda chimbuko la ukoloni duniani na kupata mashindano ya kombe la Uingereza, carling cup na FA yanayoshindaniwa kila mwaka. Kabla yake kuna mechi za Uingereza, Spain na Ujerumani. Kama hizo hazitoshi, kuna kombe la dunia la kila baada ya miaka minne. Huku mechi zikichuja hatua kwa hatua kupata mataifa yatakayoshiriki kombe la dunia.

Huko ndiko akili zilipoelekezwa. Ni kutokana na mechi hizi, Waislamu wanaswali kwa kudonoa donoa namna kuku anavyodonoa mtama. Akili hazijajikomboa kuona namna Uislamu unavyoangushwa na kutengenezewa hila mpya kila siku. Iblisi na kundi lake la Magharibi hawalali wakitafakari njia mbadala za kuwapotosha Waislamu bila ya kuwabatiza.

Mechi hizi ndizo zinazowafanya Waislamu kushindwa kusoma fiqhi na kuelewa taratibu za ndoa, mirathi na kadhalika. Mtandao wa Alhidaaya   umejaa masuala kede kede yenye kuonesha dhaahir mmommonyoko wa maadili. Inafikia hatua Muislamu anauliza kama uzinifu (kuwa na girlfriend au boyfriend) ni halali au haramu? Yote hayo yanatokana na kukosa elimu kwa kufuata mdundiko wa pumbazo kama hizi.

Jee hatujafikia hatua ya kuamini namna hizi akili zilivyotekwa nyara? Bila ya shaka yoyote hazitakuwa ni akili zenye kuona mbali isipokuwa kuweka mbele mazungumzo ya mpira badala ya kupanga mikakati ya kukuza Uislamu, kuchangia miradi ya Uislamu pamoja na kuhisabu Waislamu wanaouawa kila leo na kudhulumiwa kila sekunde. Mechi hizi ndizo zinazotengeneza njia ya kuendeleza biashara za ulevi kwa matangazo ya pombe kwenye viwanja na fulana za wachezaji, kukuza uchumi wa Magharibi na kuwadumaza Waislamu.

Tuanze leo, tusisubiri zaidi kubadilika na kuishi Kiislamu katika kila hatua. Kama kweli tunahitaji mpira, tusiwe ni wenye kufuata tu kila kitu. Tutumie muda muafaka kufanya mazoezi ya kweli kweli kusakata kandakanda huku tukitumia muda mwingi zaidi kutafakari juu ya Uislamu wetu. Kuwa bwana wa nafsi yako na wala usiwe mtumwa kwa nafsi yako kufuata kila kipendacho nafsi.