Hajj

Hajj: Hatua Kwa Hatua


1 – 7 Dhul-Hijjah – Makkah au Madiynah
Kuzuru Msikiti wa Mtume صلى الله عليه وآله وسلم  au kuweko Makkah kufanya 'Umrah (kwa Wanaofanya Hajjut-Tamattu'u) na kuendelea kuswali hapo Masjidul-Haraam.

Madiynah

Kuswali Masjidun-Nabawiy na wanaume kuzuru kaburi la Mtume صلى الله عليه وآله وسلم
  
Makkah


Kufanya Twawwaaf  Kuzunguka Ka'abah mara 7
Kuswali Raka'ah mbili Maqaam Ibraahiym



Sa'yi  -  Swafaa  Na Marwah
Kuanza Kilima cha Swafaa kwenda kilima cha Marwah mara saba.

Wakimaliza 'Umrah watabakia Makkah na kuswali katika Masjidul-Haraam kupata fadhila zake


8 Dhul-Hijjah – Mina


Asubuhi Wanaondoka Makkah kuelekea Minaa.

9  Dhul-Hijjah – Siku ya 'Arafah

Wanaondoka kutoka Minaa asubuhi kuelekea 'Arafah na kubaki hadi jua litakapozama. 
Ni siku ya kutekeleza fardhi kubwa miongoni mwa taratibu za Hajj. Siku ya kuomba Du'aa sana. Na ndiyo siku iliyokamilika Dini yetu tukufu aliposimama Mtume صلى الله عليه وآله وسلم katika mlima wa 'Arafah na kutoa khutbah yake ya mwisho. Na ni siku ambayo wengi wetu wataachiwa huru na moto.

Hapa wataswali Swalah ya Adhuhuri na Alasiri 'jam'an wa Qaswran' (kujumuisha na kufupisha Rakaah mbili mbili). Watasikiliza khutbah (watakaojaaliwa kuweko karibu na Masjidun-Namirah).  Wasiokuwepo huko siku hiyo watafunga Swawm ya 'Arafah ambayo Mtume صلى الله عليه وآله وسلم kasema inafuta madhambi ya mwaka uliopita na ujao.


Jua likizama, wataelekea Muzdalifah.

10  Dhul-Hijjah – Muzdalifah – Mina - Makkah
Watafika Muzdalifah usiku na wataswali Magharibi na 'Ishaa  'jam'an wa Qaswran' (kujumuisha na kufupisha Rakaah tatu Magharibi kawaida na kufupisha rakaa mbili 'Ishaa)
Watabakia Muzdalifah usiku mzima kwa kumkumbuka Allaah سبحانه وتعالى sana na kuokota vijiwe vya kurusha katika Jamaraat.
Asubuhi – Yawmun-Nahr (siku ya kuchinja) kwa Mahujaji, na kwa wasiokuwepo huko ni siku ya 'Iyd. Wataelekea kutekeleza vitendo vifuatavyo vya fardhi za Hajj:
1) Kurusha vijiwe katika Jamaraat
2) Kutufu Twaaful-Ifaadhwah
3) Kunyoa nywele  
4) Kuchinja
(vyovyote watakavyotanguliza  katika vitendo hivi inajuzu)
 

Kurusha mawe katika Jamaraat 
  
11 – 12 Dhul-Hijjah – Ayyaamut-Tashriyq
(Siku ya kwanza na ya pili ya Tashriyq)
Watarudi Minaa na kwa ajili ya kurusha mawe katika Jamaraat.
Ni siku za kula na kunywa na kumkumbuka sana Allaah سبحانه وتعالى  

13 Dhul-Hijjah  (Siku ya mwisho ya Tashriyq)
Wanaopenda kubakia Mina watabakia kisha watarudi Makkah na ikiwa safari imewadia watafanya Twawwaaful-Wida'a (Twawwaaf ya kuaga)

ALHIDAAYA inawaombea ndugu zetu Waislamu wote ulimwenguni wanaokwenda kutekeleza nguzo hii ya tano ya Dini, Hajjum-Mabruur, Wa Dhambum-Maghfuur na warudi salama kwa watu wao.
Na inawaombea wasiojaaliwa kutekeleza nguzo hii, Allaah سبحانه وتعالى Awajaalie uzima na afya mwakani wawe miongoni mwa Mahujaji. Aamiyn.******************************

Fadhila Za Hajj Na 'Umrah Na Adabu Zake



Imekusanywa Na: Ukht Muznah Faraj

Alhamdulillahi Rabbil Alaamiyn Was swalatu Wassalaamu Alaa Nabiyyinaa Waalaa Aalihi Waswahbihi Waman Tabiahum bi’ihsaani ilaa yaumid’diyn. Amma Ba’ad,
1- Amesema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):
((Na Allaah Amewawajibishia watu wafanye hajji katika nyumba hiyo; (Al-Ka’abah) Yule awezae kufunga safari kwenda huko. Na atakae kanusha (asende, hali kuwa anaweza) basi Allaah simuhitaji kuwahitajia walimwengu))
[Qur-aan: 3:97]

2- Na amesema Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):
((Kufanya umrah hadi umrah  hufutiwa madhambi baina yake, na Hajj (Mabruur) yenye kukubaliwa haina malipo isipokuwa pepo))
{Imepokewa na Al-Bukhaariy na Muslim}

3- Na amesema Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):
((Atakayehiji ikawa hakufanya maovu (kwa vitendo wala kwa maneno) na wala hakuvunja amri za Allaah (Subhaanahu Wata’ala) atasamehewa madhambi yake yote atakuwa kama siku aliyozaliwa na Mama yake))
[Imepokewa na Al-Bukhaariy na Muslim]

4- Na amesema Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):
((Chukueni Hajj kutoka kwangu))
[Imepokewa na Muslim]
- Ni wajibu wa kila mwenye kuhiji na kufanya umrah awe mali anayofanyia ibada hizo iwe ni ya halali ili Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) aikubali, kwa kauli ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):
((Hakika Allaah Mtukufu ni mzuri na hakubali isipokawa kizuri))
[Imepokewa na Muslim]

6- Kwa hakika hajji ni kongamano kubwa kwa waislamu linalo wakutanisha waislamu, kwa sababu kunapatikana ndani yake kujuana, kupendana, na kusaidiana katika kutatua matatizo juu ya kila hali, na pia kushuhudia manufaa yanayopatikana humo ya dini na dunia. SubhaanAllaah!!!  Ametukuka Aliye Mbora wa viumbe.
Na Amesema Allaah Mtukufu:
((Na saidianeni kwa wema na uchaji Allaah wala msisaidaene katika madhambi na uadui))
[Qur-aan: 5:2]

7- Inajuzu kufanya umrah katika wakati wowote, lakini kufanya umrah katika mwezi wa Ramadhaan ni bora,  kwa kauli aliyosema Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):
((Kufanya 'Umrah katika mwezi wa Ramadhaan ni kama Hajj))
[Al-Bukhaariy na Muslim]

8- Swalah katika Msikiti mtukufu wa Makkah ni bora mara  laki moja kuliko Swalah katika Misikiti mingine. Kwa kauli aliyosema Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):
((Swalah katika Msikiti wangu huu ni bora katika Swalah elfu moja kuliko misikiti mingine iispokuwa Msikiti  mtukufu wa Makkah)) [Imepokewa na Muslim]
Swalah moja katika Msikiti wa Mtume Madiynah ni sawa malipo yake na Swalah elfu moja (1000).
Na amesema Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):
((Swalah katika Msikiti mtukufu wa Makkah ni bora kuliko Swalah katika Msikiti wangu huu kwa Swalah mia))
[Imepokewa na Ahmad]
Akimaanisha mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kuwa swala moja ni sawa na swala mia, yaani 100*1000 = 100,000 .
Hii ni kuonyesha kuna fadhila kubwa sana na yoyote ambae amejaaliwa kufika huko basi na ajitahidi swala zake zote aziswali msikitini ili asikose thawabu hizi.

KWA UFUPI:
Hajj ni nguzo miongoni mwa nguzo za Kiislamu na ndani yake kuna fadhila nyingi ambazo nimezitaja kwa ufupi na manufaa  ya kidunia na Akhera.  Kwa mfano, unaweza kufanya biashara pindi umalizapo hajji na mengineyo ambayo tuliyataja hapo juu. Na manufaa ya akhera ambayo ni bora zaidi kuliko ya dunia.
Allaah Amesema:
((Na maisha (bora zaidi kabisa) ni ya Aakhirah yenye kudumu))
[Qur-aan: 87:17]

Basi ni juu ya kila muislamu ajitahidi kuendea njia hiyo pale atapo kuwa na uwezo wa kuifikia njia hiyo kabla hayajamfikia mauti hali yuko katika maaswi. Basi na ajihadhari kutokana na maovu, kuvunja amri za Allaah, mijadala isiyo ya hakki wala faida ndani yake na maaswi yote kwa ujumla.

ADABU ZA HAJJ NA UMRAH:
1- Itakase hajji yako iwe kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu Wata’ala) na sema kama alivyosema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)
((Ee Mola ifanye Hajj yangu isiwe ya kujionyesha wala kusifiwa))
[Swahiyh Al-Bayhaqiy]
Kwani kuna baadhi ya watu matendo yao wanayafanya ili waonekane na wao wamekwenda au wamefanya hajji au wamesikilikana kwa kusifiwa kama Fulani pia amekwenda iwe ni matendo ya hajji au hata ibada zozote ilihali si kwa ajili ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) hao matendo yao yatakuwa hayana malipo yoyote mbele ya Allaah Mtukufu.

2- Iwe hajji  imewafikiana na hajji aliohijji Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kama alivyo sema mwenyewe Bwana Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema:
((Chukueni Hajj kutoka kwangu))
[Imepokewa na Muslim]

3- Jihadhari na  kutokufanya maovu na yaliyo katazwa, na maaswi, na mijadala iliyo baatili (iliyokatazwa) mpaka hijjah yako iwe ni maqbuul ( yenye kukubalika).

4- Jihadhari na kuomba duaa kwa asie kuwa Allaah Mtukufu. kuomba maiti mfano kwenye makaburi wakati unapo zuru makaburi ni kwa ajili ya kujikumbusha na mauti na kuwatakia rehma na maghfira sikuwaomba au kutaka msaada au kuokolewa  hiyo itakuwa ni shirki ambayo itabatilisha hajji na amali zako zote. Kama alivyo sema Allaah Mtukufu:
((Ikiwa utamshirikisha (Allaah ) bila shaka matendo yako yote yataruka patupu (hutazipatia thawabu japo ni matendo mazuri ) na lazima utakuwa miongoni mwa wenye khasara))
[Qur-aan 39:65]

5- Unatakiwa uwe mpole kwa walio karibu yako yaani walioko pembezoni mwako  wakati unapokuwa unafanya twawafu (kuizunguka al ka’abah) na unapo fanya saa’yi (kutembea kilima cha saffa na mar’wah) na wakati wa kutupa mawe katika minara ya jamaraati, wala msinyanyuwe sauti wakati wa kumtaja Allaah wala wakati wa Duaa na khasa pale mnapokuwa kwenye kundi kwani kunyanyuwa sauti kunawachanganya wengine kwakufanya hivyo hakuna dalili na hivyo kunyanyuwa sauti ni Bid’aa iliyozushwa.

6- Haifai kufanya zahma yaani kusukumana wakati wa kuliendea jiwe jeusi wala kusimama hapo kuwazulia wengine wakati unapo fanya tawaafu. Inavotakiwa ni kuligusa, kulibusu na huku unaomba nakuondoka si kusukumana.

7- Kusimama wakati wa Sa’yi kati ya Swaffa na Marwah pindi inapo nadiwa swala ya Jama'ah mpaka itapomalizika Swalah utatimiza palipobaki.

8- Kuhifadhi Swalah ya Jama'ah katika msikiti na khasa unapokuwa katika Msikiti wa Makkah, Kwani kuna fadhila kubwa kama tulivyotangulia kusema.

9- Usiwapitepite wenye kuswali ukawaudhi, kaa palipo karibu yako penye nafasi.

10- Jihadhari na kuwapita watu wanapo kuwa kwenye safu ya Swalah kati yako na mwenye kuswali hata kama ni katika msikiti mtukufu wa Makkah ili upite safu ya mbele ikiwa unataka kukaa mbele basi inakubidi uwahi na sio kuwakunja watu shingo ili upite mbele, kwani hayo ni matendo ya shaitwani, isipokuwa iwe kwa  dharura.
11- Kuzidisha kuizunguka al ka’abah kwani kufanya hivyo kuna malipo makubwa  kama alivyosema Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam):
((Mwenye kuizunguka Al-Ka’abah mara saba atakuwa kama aliyemuacha huru Mtumwa))
[Imepokewa na Ibn Maajah]

12- Haifai kuchinja  kabla ya kufikia siku ya kuchinja wala haifai kutoa sadaka  kwa thamani yake.

13- Na katika alama za kukubaliwa hajji ni kubadilika katika hali iliyo nzuri ya aqidah yako (kutokumshirikisha Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) katika ibaada zako kushirikiana na Waislamu wenzio kwa wema na tabia njema na ni juu yako kumuomba Allaah wakati wote hii ni kipimo baada ya hajji kwani ikiwa hukubadilika katika 'Aqidah yako na tabia yako kwa ujumla itakuwa hajji yako ni matembezi tu na sio 'Mabruur'.
((Ee Mola Tukubalie hakika Wewe ni Mwenye kusikia na ni mjuzi))
“Aamiyn”

Allaah Atuwafiqishe na Atufanyie wepesi na ajaalie manufaa na kuyafanyia kazi yote na tufaidike nayo In sha Allaah. 

Wa Allaahu A’alam******************************************************

Maajabu Ya Zam Zam



Utafiti wa maji uliofanywa na Tariq Hussain,
Mhandisi wa kutoa chumvi katika maji
Imefasiriwa na Ummu Ummu Ayman

Tumekuja hapa tena kutekeleza Umrah, na nimekumbushwa na maajabu ya Zamzam.
Kisima cha Zamzam ni kisima ambacho Allaah amekichimbua huko Makkah kwa ajili ya mke wa Mtume Ibraahiym na kwa mtoto wake mkubwa Ismail, (amani iwe juu yao wote). Niruhusu nirudi nyuma kuona mambo yalianzaje. Katika mwaka 1971, Daktari wa kimisri aliandika katika European Press, barua inayosema kuwa maji ya Zamzam hayafai kwa matumizi ya kunywa.
Kwa haraka nilifikiria kuwa hii ilikuwa ni aina ya njama dhidi ya Uislam na kuwa kwa kuwa hoja zake ziliegemea katika dhana ya kuwa kwa kuwa Ka’abah ni pahala pafupi (chini ya usawa wa bahari) na ipo katikati ya mji wa Makkah, maji machafu ya mji yanayojikusanya katika mitaro yanaangukia katika kisima cha maji hayo (yaani Zamzam).
Kwa bahati njema, habari hii ilimfika  Mfalme Faysal ambae alikasirika sana na kuamua kupingana na maneno ya uchokozi ya Daktari huyo wa kimisri. Haraka aliamrisha Wizara ya Kilimo na Raslimali ya Maji kuchunguza na kupeleka sampuli za maji ya Zamzam katika maabara za Ulaya kwa ajili ya kuchunguza ubora wa maji hayo.
Wizara baaadae iliielekeza Jeddah Power and Desalination Plants kuifanya kazi hii. Hapo ndipo nilipoajiriwa kama mhandisi wa utoaji wa chumvi majini (mhandisi wa kemikali katika uzalishaji wa maji ya kunywa kutoka katika maji ya chumvi). Nilichaguliwa kuifanya kazi hii.
Kufikia hapo, nakumbuka kuwa sikuwa na fununu yoyote kuhusu kilivyo kisima chenye maji. Nilikwenda Makkah na kuripoti kwa viongozi wa wahusika ili kuelezea madhumuni ya ziara yangu. Walinitengea mtu maalum kunipa msaada wowote ule utaohitajika.
Tulipofika kisimani, ilikuwa vigumu kwa mimi kuamini kuwa, bwawa la maji kama kidimbwi kidogo, kama futi 18 kwa 14, ndio kisima chenye kutoa mamilioni ya magaloni ya maji kila mwaka kwa mahujaji tokea kilipoanza wakati wa Nabii Ibraahiym (‘Alayhis Salaam), karne nyingi zilizopita.
Nilianza uchunguzi wangu na kuchukua vipimo vya kisima hicho. Nilimtaka yule mtu anioenyeshe kina cha kisima hicho. Kwanza alikoga na kuzamia katika maji. Kisha akasimama sawa sawa. Niliona kuwa kina cha maji kimefikia kiasi cha usawa wa mabega yake. Urefu wake ulikuwa  kama futi tano na nchi 8. Kisha akaanza kwenda kutoka kona moja hadi nyengine ndani ya kisima (akiwa amesimama wakati wote kwani hakuruhusiwa kuzamisha kichwa chake ndani ya maji) akijaribu kutafuta paipu inayoingiza maji kisimani ili kuona maji hayo yanakotokea. Hata hivyo, mtu huyo aliripoti kuwa hakuweza kuipata paipu yoyote ndani ya kisima hicho.
Nikapata mawazo mengine. Maji yanaweza kutolewa kwa haraka kwa kutumia pampu kubwa iliyokuwa imewekwa kwa ajili ya kujaza tangi la maji ya Zamzam.  Kwa njia hii, kina cha maji kitapungua na kutuwezesha kupata sehemu yanayoingilia maji. Kwa mshangao, hakuna kilichoonekana wakati wa kuyavuta maji, lakini nilijua kuwa hii ndio njia pekee ya kuweza kuipata sehemu ya kuingilia maji katika kisima. Kwa hivyo niliamua kurejea tena njia hiyo. Lakini mara hii nilimuelekeza yule mtu atulie pahala pamoja na aangalie kwa uangalifu chochote kitachojitokeza ndani ya kisima ambacho si cha kawaida.
Baada ya muda, ghafla alinyanyua mkono wake na kusema kwa nguvu, Alhamdulillah! Nimepaona! Mchanga unacheza cheza chini ya miguu wakati maji yanachimbuka katika sehemu ya chini ya kisima”.
Kisha alikizunguka kisima wakati wa kuvutwa maji na akahisi vile vile katika kila sehemu ya chini ya kisima. Ukweli ni kuwa uchimbukaji wa maji katika kila pahala ulikuwa sawa sawa, kwa hivyo kufanya kina cha maji kiwe kimetulia. Baada ya kumaliza uangalizi wangu nilichukua sampuli za maji kwa ajili ya uchunguzi katika maabara za Ulaya. Kabla ya kuondoka Ka’abah, Niliwauliza wahusika kuhusu visima vyengine vya Makkah. Niliambiwa kuwa visima hivyo karibu vyote vimekauka.
Nilipofika ofisini kwangu Jeddah niliripoti ugunduzi wangu kwa mkuu wangu ambae alinisikiliza kwa hamu kubwa lakini akatoa maoni yake yasiyopendeza kuwa kisima cha Zamzam kumeungana chini kwa chini na Bahari Nyekundu. Itawezekana vipi wakati Makkah iliyo kilomita 75 mbali na bahari, visima vilivyopo kabla ya mji kwa kawaida huwa vikavu.
Matokeo ya sampuli (vielelezo) zilizopimwa katika maabara ya Ulaya na zile ambazo tulizozipima sisi katika maabara yetu yalionekana kuwa karibu ni sawa sawa. Tofauti baina ya maji ya Zamzam na maji ya visima vyengine (maji ya mjini) yalikuwa ni katika viwango vya chumvi za chokaa (calcium) na magnesi (magnesium). Viwango nya chumvi hizi vilikuwa ni vikubwa kidogo katika maji ya Zamzam. Hii inawezekana ikawa ni sababu ya maji haya huwaondoshea uchovu (kuwachangamsha) mahujaji. Lakini kilichojitokeza zaidi, ni kuwa maji hayo yalikuwa na floridi (fluorides) ambayo inaathiri vijidudu.
Zaidi ya hayo, maelezo ya maabara za Ulaya yalionyesha kuwa maji hayo yanafaa kwa kunywa. Kwa hivyo maneno yaliyowekwa na Daktari wa Kimisri yalishuhudiwa kuwa ni ya uongo.
Yaliporipotiwa mambo hayo kwa Mfalme Faysal alifurahi mno na akaamrisha tofauuti za kupingana kati ya ripoti hizo zitolewe katika jarida la European Press.
Kwa njia hiyo, imekuwa ni baraka kuwa uchunguzi huo ulifanyika ili kuonyesha kemikali zilizomo katika maji hayo. Kwa kweli, kadri unavyopekuwa zaidi, ndivyo maajabu yake yanavyojitokeza zaidi na unajikuta mwenyewe unaamini kikamilifu miujiza ya maji hayo ambayo Allaah Amejaalia kuwa zawadi kwa wacha Mungu wanaokuja katika ardhi yenye jangwa kutoka masafa ya mbali kwa ajili ya hija.
Niwache nifupishe baadhi ya maumbile ya maji ya Zamzam
·  Kisima hichi hakijawahi kukauka. Na badili yake daima kimekuwa kinatosheleza mahitaji ya maji.

·  Daima kiwango chake cha chumvi na ladha kinabaki sawa sawa tokea kimekuwepo.

·  Ubora wake kwa kunywa daima  umetambuliwa kimataifa kwa vile mahujaji kutoka duniani kote wamekuwa wakiitembelea Ka’abah kila mwaka kwa ajili ya Hijja na Umra, lakini hakuna alielalamika kuhusu ubora huo. Badili yake, wamekuwa daima wakiyafurahia maji hayo ambayo yanawaondoshea uchovu.

·  Maji huwa na ladha tofauti katika pahala tofauti. Kupendwa kwa maji ya Zamzam kumekuwa ni kwa kimataifa.

·  Maji haya hayajawahi kutibiwa kwa kemikali yoyote au kutiwa klorini kama ilivyo kawaida ya maji yanayopelekwa mijini. Kuota kwa njia ya kibaiolojia (biological growth) vimelea na majani ni kawaida katika visima karibu vyote. Hii inasababisha maji kuwa si mazuri (kwa kunywa) kutokana na kuota kwa mwani (algae) unaoharibu  ladha na harufu. Lakini katika kesi ya kisima cha Zamzam, hakuna dalili yoyote ya kuota kwa vitu hivyo.

·  Karne nyingi zilizopita, Bibi Hajra (‘Alayhas Salaam) alitafuta kwa mfadhaiko maji katika vilima vya Swafaa na Marwa ili kumpa mtoto wake aliekuwa ndio kwanza anazaliwa Nabii Isma’iyl (‘Alayhis Salaam). Alipokuwa anakimbia huku na kule kutafuta maji, mtoto wake alipiga piga miguu yake chini mchangani. Bwawa la maji likachimbuka, kwa rehma za Allaah, yakajifanya kuwa kisima ambacho kimekuja kuitwa Maji ya Zamzam.*********************************************

Hajj Ya Mtume (Swalla Allaahu ‘Alayhi Wa Aaalihi Wa Sallam)



(Kama Ilivyohadithiwa Na Jaabir Bin ‘Abdillaah (Radhiya Allaahu ‘Anhu)

Imetafsiriwa Na: Muhammad Faraj Saalim As-Sa’ay


Anasema Imaam Muslim:

“Nimehadithiwa na Abu Bakr bin Abi Shaybah na Is-haaq bin Ibraahiym, wote pamoja. Na kutoka kwa Haatim amesema kuwa Abu Bakr amesema:
'Nimehadithiwa na Haatim bin Ismaa’iyl Al-Madaniy, kutoka kwa Ja’afar bin Muhammad, kutoka kwa baba yake (Radhiya Allaahu ‘anhum) kuwa alisema:
“Tulimwendea Jaabir bin ‘Abdillaah (Radhiya Allaahu ‘anhu), akaanza kutuuliza majina yetu mmoja mmoja mpaka akaishia kwangu. Nikamwambia:
'Mimi ni Muhammad bin Aliy bin Husayn”. Akakivamia kichwa changu, kisha akanifungua kifungo changu cha juu kisha cha chini yake, kisha akauweka mkono wake kifuani pangu, na wakati huo nilikuwa bado kijana. Akaniambia;
“Marhaban (karibu) ewe mwana wa ndugu yangu. Uliza unalotaka kuuliza”.
Nikamuuliza, na wakati ule alikuwa kipofu, na wakati wa Swalah ulipowadia aliinuka huku akiikusanyakusanya nguo yake, kila akijifunika nayo upande mmoja wa bega lake, upande wa pili inaanguka kwa sababu ya udogo wake.
Akatuswalisha, kisha nikamwambia:
“Tuhadithie juu ya Hajj ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam)”

Jaabir (Radhiya Allaahu ‘anhu) akasema:
“Watu walipoarifiwa kuwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) atahiji mwaka huu, walianza kumiminka mjini Madiynah kwa wingi sana, kila mmoja akitamani aongozwe na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na afanye kama atakavyofanya.

(Ilipowadia siku ya safari) Tukaondoka naye mpaka tulipowasili Dhul Hulayfah (Abaar ‘Aliy - mikati ya watu wa Madiynah), Asmaa bint Umays akamzaa Muhammad bin Abi Bakr Asw-Swiddiyq (Radhiya Allaahu ‘anhu), akamtuma mtu kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kumuuliza nini afanye. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akamwambia:
“Oga, kisha weka kitambaa na utie nia ya Ihram (niyyah ya kuhiji)”.

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akaswali Msikitini kisha akampanda ngamia wake anayejulikana kwa jina la Al-Qaswaa, na alipokuwa katikati ya jangwa nikainua kichwa changu kutizama waliokuwa mbele ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), nikaona watu wengi sana, upeo wa macho yangu wakiwemo waliopanda wanyama na wanaokwenda kwa miguu, kisha nikatazama kuliani kwake, nikaona hivyo hivyo, kisha upande wake wa kushoto nikaona hivyo hivyo, na nyuma yake hivyo hivyo, na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akiwa pamoja nasi huku wahyi ukimteremkia, huku akituhadithia, na kila anachokifanya, sisi tulikuwa tukimfuata.
Kisha akaanza kusema;
“Labbayka Allahumma labbayka, labbayka laa shariyka laka labbayka. Innal hamda wa n’imata laka wal mulk, laa shariyka laka”.
Na watu wakawa wanasema kama anavyosema”.

Jaabir bin ‘Abdillaah (Radhiya Allaahu ‘anhu) akaendelea kusema:
“Hatukuwa tukitia niyyah nyingine isipokuwa nia ya Hajj, (hatukuwa tukijua aina nyingine za Hajj), hatukuwa tukijua juu ya ‘‘Umrah. Tukaendelea na Safari mpaka tulipoifikia Al-Ka’abah tukiwa pamoja naye, akaligusa jiwe jeusi kisha akaanza kutufu. Katika mizunguko mitatu ya mwanzo alikuwa akenda kwa kukazana, na katika minne iliyobaki akenda mwendo wa kawaida. Alipomaliza akaenda penye Maqaamu Ibraahiym ('Alayhis Salaam), akasoma:
“Wattakhidhuw mim-maqaami Ibraahiyma muswallaa” [Al-Baqarah: 125]
Na maana yake “Na mahali alipokuwa akisimama Ibraahiym pafanyeni pawe pa kuswalia.”

Akaelekea Qiblah na kuswali rakaa mbili mahali hapo, akasoma katika rakaa ya mwanzo (Alhamdu pamoja na) Qul yaa ayyuhal kaafiruun na katika rakaa ya pili akasoma (Alhamdu pamoja na) Qul Huwa Allaahu Ahad, kisha akarudi penye jiwe jeusi, akaligusa kisha akatokea mlangoni kuelekea Swafaa.

Alipokaribia Swafaa akasoma:
“Inna Swafaa wal Marwata min sha’aairi LLaahi” - Abdau bimaa bada-a Allaahu bihi”
Na maana yake ni:
“Hakika Swafaa na Marwah (Majabali mawili yanayofanyiwa ibada ya Saa'yi huko Makkah) ni katika alama za kuadhimisha Dini ya Allaah - Naanzia pale alipoanzia Allaah.
Akaanzia Swafaa, akaupanda mlima huo mpaka alipoweza kuiona Al Kaaba akaelekea Qiblah akasema:
“Laa ilaha illa Allaah - Allahu Akbar”,
Kisha akasema:
“La Ilaaha Illa Allaah, Wahdahu La shariyka Lahu, Lahul Mulku wa Lahul Hamdu, wa Huwa ‘alaa kulli shay-in Qadiyr. La Ilaaha Illa Allaah, Wahdahu, Anjaza wa’adahu, wa Naswara ‘abdahu, wa Hazamal ahzaaba Wahdah”.

Kisha akaomba du’aa, kisha akarudia kusema hivyo mara tatu, kisha akashuka kuelekea Marwah, alipofika katikati ya bonde akawa anakwenda mwendo wa kukazana, na alipolifikia jabali la Marwah akalipanda kwa mwendo wa kawaida, na alipolifika juu yake akasoma na kufanya kama alivyofanya alipokuwa juu ya Swafaa.

Akaendelea hivyo mpaka twawafu yake ilipomalizikia Marwah akasema:
“Lau kama amri niliyopewa (hivi sasa) ningelipewa kabla, nisingechukuwa pamoja nami mnyama na ningeijaalia (twawafu yangu na sa’ayi yangu) kuwa ‘Umrah, na kama yupo kati yenu asiyekuwa na mnyama basi avue nguo za Ihraam na aijaalie iwe ‘Umrah”.
Akainuka Suraaka bin Maalik bin Ja’athum (Radhiya Allaahu ‘anhu) akasema:
“Ee Mtume wa Allaah, (hukmu hii) ni kwa ajili ya mwaka huu tu au milele?”
Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akaviingiza vidole vyake vya mkono wa kulia ndani ya vidole vya mkono wa kushoto na kusema:
“‘Umrah na Hajj zishaingiliana” akasema hivyo mara mbili, kisha akasema; “La, bali milele”.

‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) akawasili kutoka nchi ya Yemen akiwa na ngamia wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam), akamkuta Faatwimah (Radhiya Allaahu ‘anha) amekwishavuwa nguo za Ihraam na kuvaa nguo za kawaida za rangi rangi na ametia wanja. Akamkataza, kwa ajili hiyo, lakini Faatwimah (Radhiya Allaahu ‘anha) akamwambia:
“Baba yangu ameniamrisha kufanya hivi”.
Akaenda kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) kumshtaki Faatwimah kwa vile alivyofanya (kuvua nguo za Ihraam na kupaka wanja) na kwa kule kusema kwake kuwa Baba yake ndiye aliyemuambia, akamjulisha kuwa yeye alimkataza kwa kufanya kwake vile.
Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akamjibu:
“Ni kweli, (na) wewe umetia niyyah gani ya kuhiji ulipokuwa unakuja?”
Akasema:
“Nilisema; 'Allahumma mimi natia niyyah ile ile aliotia Mtume wako”.
Akamwambia:
“Basi mimi ninaye mnyama, kwa hivyo tusivuwe (nguo za Ihraam)”.

Idadi ya wanyama aliokuja nao ‘Aliy (Radhiya Allaahu ‘anhu) kutoka Yemen ikichanganywa na idadi ya wanyama aliokuja nao Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) ikafikia ngamia mia moja.

Watu wote wakavua Ihraam zao na kukata nywele isipokuwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) na wachache waliokuja na wanyama wao.

Ilipofika siku ya Tarwiyah - siku ya tarehe 8 Dhul Hajj, watu wakaondoka kuelekea Minaa wakitia niyyah ya Hajj, na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akampanda mnyama wake na kuelekea huko pamoja nao. (Walipowasili Minaa), wakaswali Adhuhuri, Alasiri, Maghrib, ‘Ishaa na Alfajiri (Qaswran, kila Swalah katika wakati wake).

(Baada ya kuswali Alfajiri) Akasubiri kidogo mpaka jua lilipochomoza akaamrisha lisimamishwe hema mahali paitwapo Namirah, - karibu na ‘Arafah -. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akaondoka kuelekea Namirah na akapitiliza Muzdalifah bila ya kusimama penye Mash’arul Haraam, juu ya kuwa Ma-Quraysh walidhania atasimama hapo kama walivyokuwa wakifanya wakati wa Ujahilia.

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) hakusimama mpaka alipowasili Arafat, akaliona hema lishasimamishwa pale Namirah kama alivyoamrisha, akashuka na kupumzika hapo mpaka ulipoingia wakati wa Adhuhuri, akaamrisha aletwe ngamia wake Al-Qaswaa, akampanda na kwenda moja kwa moja mpaka alipofika katikati ya bonde la ‘Arafah akasimama na kuwahutubia watu akasema:
“Hakika ya damu zenu na mali zenu (ni tukufu sana kwa hivyo) ni haramu baina yenu (kumwaga damu zenu na kudhulumiana baina yenu) kama ulivyokuwa utukufu wa siku yenu hii, katika mwezi wenu huu, katika mji wenu huu, visasi vyenu vyote vya wakati wa ujahilia viko chini ya mguu wangu - nishavibatilisha - na kisasi cha mwanzo cha kumwaga damu yetu ninachokibatilisha ni kisasi cha (kumwaga) damu ya Ibn Rabi’ah bin Al-Haarith - alikuwa na mtoto anayenyonyeshwa katika kabila la Bani Sa’ad,akauliwa na watu wa kabila la Hudhayl - Na ribaa iliyokuwa ikichukuliwa wakati wa Ujahilia ishabatilika, na ribaa ya mwanzo ninayoibatilisha ni ribaa yetu, ribaa ya ‘Abbaas bin ‘Abdil Muttwalib, ishabatilika yote, na muogopeni Allaah katika wake zenu, kwani nyinyi mumewachukuwa kwa dhamana ya Allaah, na mkahalalishiwa tupu zao kwa neno la Allaah, na nyinyi mna haki zenu juu yao. Wasiwaingize nyumbani kwenu yeyote msiyempenda (awe mwanamume au mwanamke), na wakifanya hivyo, mnayo haki ya kuwapiga kipigo kisichoumiza. Na haki yao juu yenu ni kuwalisha na kuwavisha kwa wema. Na nimekuwachieni ambayo hamtopotea baada yake ikiwa mtashikamana nayo, Kitabu cha Allaah. Mkiulizwa juu yangu mtasema nini?”
Wakasema:
“Tutashuhudia kuwa umefikisha na umekamilisha na umenasihi.”
Akanyanyua kidole cha shahada akawa mara anakielekeza mbinguni mara anakielekeza kwa watu, akasema:
“Mola wangu shuhudia - (mara tatu)”.

Kisha akaadhini, akakimu na kuswali Swalah ya Adhuhuri, kisha akaqimu tena na kuswali Swalah ya Alasiri bila kuswali Sunnah baina yao. Kisha akampanda ngamia wake na kuelekea naye moja kwa moja mpaka mahali pa kusimama (katika uwanja wa Arafah), akamuelekeza ngamia wake Al-Qaswaa penye majabali na yeye akaelekea Qiblah.

Akasimama mahali hapo mpaka wakati wa Maghribi ulipoingia na umanjano wa jua kutoweka na juwa kuzama kabisa, ndipo alipoondoka akiwa amempakia Usaamah nyuma yake.

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akampanda ngamia wake Al-Qaswaa na kuianza safari ya kwenda Muzdalifah. Akawa anazikaza kamba za hatamu za ngamia wake na kumbana nazo ili asiweze kwenda mbio kwa ajili ya zahma ya watu. Akawa anaashiria watu kwa mkono wake wa kulia huku akiwaambia:
“Enyi watu! (nendeni kwa) utulivu (nendeni kwa) utulivu.”
Na kila anapolifikia jabali akawa anailegeza kamba ili mnyama wake aweze kupanda kwa wepesi. Akawa anafanya hivyo mpaka alipowasili Muzdalifah, akaswali hapo Swalah ya Maghribi na ‘Ishaa kwa Adhana moja na Iqaamah mbili, bila ya kusabbih baina ya Swalah hizo.

Kisha Mtume wa Allaah akapumzika mahala hapo mpaka Alfajiri ilipoingia, akaswali Alfajiri pale ilipombainikia kuwa wakati wa Swalah ya Alfajiri ushaingia, kwa Adhaana na Iqaamah.

Kisha akampanda Al-Qaswaa mpaka alipowasili Masha’arul Haraam - (jabali lililopo hapo hapo Muzdalifah), akaelekea Qiblah na kuomba du’aa huku akikabbir na kumtukuza na kumpwekesha Allaah. Akawa katika hali hiyo mpaka kulipopambazuka.

Kisha akaondoka na kuianza safari ya kuelekea Minaa kabla ya jua kupanda akiwa amempakia Al-Fadhwl bin ‘Abbaas aliyekuwa kijana mwenye nywele nzuri, mweupe, na mwenye sura nzuri. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) alipokuwa akiondoka naye, akapita mbele yao ngamia aliyebeba wanawake wawili, na Al-Fadhwl akawa anawaangalia wanawake hao. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akauweka mkono wake usoni pa Al-Fadhwl ili asiweze kuwatazama, lakini Al-Fadhwl aliugeuza uso wake upande wa pili na kuendelea kuwatazama, na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akaukamata uso wa Al-Fadhl na kuugeuza upande mwingine. Akaendelea na safari yake mpaka alipolifikia bonde la Muhsir akaongeza mwendo kidogo, kisha akapita njia ya kati inayopeleka moja kwa moja mpaka penye Jamaraat kubwa (nguzo watu wanaporusha vijiwe vidogo), na alipolifikia Jamarah (hilo) lililokuwa karibu na mti akalipiga kwa vijiwe saba huku akikabbir kila anaporusha jiwe.

Kisha akaondoka kuelekea mahali pa kuchinja, akachinja (ngamia) sitini na tatu kwa mkono wake, kisha akampa ‘Aliy achinje waliobaki, kisha akaamrisha nyama ikatwe katwe, ikatiwa ndani ya vyungu vya kupikia, ikapikwa, wakala katika nyama ile na kunywa supu yake.

Kisha Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam) akampanda ngamia wake na kuelekea penye Al-Ka’abah, akaswali Adhuhuri alipowasili Makkah.

Baada ya kuswali akawaendea watu wa kabila la Bani ‘Abd-l Muttwalib waliokuwa na jukumu la kuwahudumia watu katika kunywa maji ya Zamzam, akawaambia:
“Wanywesheni maji enyi watu wa kabila la Bani ‘Abdil Muttwalib, ingekuwa sikuogopeeni watu kukuchukulieni kazi hii ya kunywesha maji, basi ningelikusaidieni.”
 *********************************************

Umuhimu Wa Kukimbilia Kutekeleza Nguzo Ya Hajj


Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):
((وَلِلّهِ عَلَى النَّاسِ حِجُّ الْبَيْتِ مَنِ اسْتَطَاعَ إِلَيْهِ سَبِيلاً وَمَن كَفَرَ فَإِنَّ الله غَنِيٌّ عَنِ الْعَالَمِينَ))

((Na kwa ajili ya Allaah imewajibikia watu wahiji kwenye Nyumba hiyo, kwa yule awezae njia ya kwendea. Na atakayekanusha basi Allaah si mhitaji kwa walimwengu)) [Al-'Imraan: 96-97].

Na kauli ya Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

((بني الإسلام على خمس شهادة أَنْ لا إلهَ إلا اللهُ وأَنَّ محمِّداً رسولُ الله وإقام الصلاة ، وإيتاء الزكاة، وصوم رمضان، وحج البيت)) متفق عليه

((Uislamu umejengeka kwa matano; Kushuhudia kwamba hakuna Mola apasaye kuabudiwa isipokuwa Allaah, na Muhammad ni Mjumbe wa Allaah, kusimamisha Swalah, kutoa Zakaah, kufunga Ramadhaan, na kuhijii katika Nyumba (tukufu))) [Al-Bukhaariy na Muslim]


Tunatambua kutokana na kauli hizo za utangulizi kuwa kutekeleza ibada ya Hijjah ni fardh kwa kila mwenye uwezo. Hivyo asiyeharakisha kutekeleza ibada hii atakuwa amemuasi Mola wake Mtukufu na Mjumbe Wake (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na itakuwa ni dhambi kubwa kwake ikiwa kuacha huko ni kwa makusudi na hali alikuwa ana uwezo wa mali, siha n.k., sababu atakuwa amekanusha amri ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) kama Anavyosema:


((وَمَا كَانَ لِمُؤْمِنٍ وَلَا مُؤْمِنَةٍ إِذَا قَضَى اللَّهُ وَرَسُولُهُ أَمْرًا أَن يَكُونَ لَهُمُ الْخِيَرَةُ مِنْ أَمْرِهِمْ وَمَن يَعْصِ اللَّهَ وَرَسُولَهُ فَقَدْ ضَلَّ ضَلَالًا مُّبِينًا))

((Haiwi kwa Muumini mwanamume wala Muumini mwanamke kuwa na khiari katika jambo, Allaah na Mtume Wake wanapokata shauri katika jambo lao. Na mwenye kumuasi Allaah na Mtume Wake basi hakika amepotea upotofu ulio wazi)) [Al-Ahzaab: 36].


Kwa Nini Muislam Aharakishe Kutekeleza Hajj?

Huenda Akafikwa Na Masaibu:

Muislamu mwenye uwezo wa fedha na siha inampasa afanye hima kutimiza fardhi hii kabla ya kufikwa na masaibu kwani huenda ukawa humiliki tena siku za mbele.

Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ametuhimiza na kutuonya hayo:  


((مَنْ أَرَادَ الْحَجَّ فَلْيَتَعَجَّلْ)) . رواه الإمام أحمد وأبو داود وابن ماجه. وفي رواية أحمد وابن ماجه: (( فَإِنَّهُ قَدْ يَمْرَضُ الْمَرِيضُ ، وَتَعْرِضُ الْحَاجَةُ)) حسنه الألباني في صحيح ابن ماجه  

 ((Mwenye kutaka kufanya Hijjah basi aharakize)). [Imaam Ahmad, Abu Daawuud na Ibn Maajah] na katika riwaaya ya Ahmad na Ibn Maajah ((Kwani huenda akapata maradhi au akafikwa na haja)). [Kaipa daraja ya hasan Shaykh Al-Albaani katika Swahiyh-Ibn Maajah]

Vile vile amesema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)

((تعجلوا إلى الحج  (يعني الفريضة)  (( فإن أحدكم لا يدري ما يعرض له)) أخرجه الإمام أحمد رحمه الله وحسَّنه الألباني في إرواء الغليل.

((Harakizeni Hajj, (yaani kutekeleza fardhi ya Hajj) ((kwani hajui mmoja wenu nini kitamsibu)). [Imaam Ahmad na kaipa daraja ya hasan Shaykh Al-Albaaniy katika Irwaaul-Ghaliyl]


Hatuna Dhamana Na Umri Mrefu

Waislamu wengi hawaifanyii hima ibada hii na aghalabu ya sababu ni:

Wengine huona kuwa ni bado vijana hivyo wanasubiri wawe na umri mkubwa ndio watimize. Hao wajiulize; je, wana uhakika gani kuwa wataruzukiwa umri mrefu? Bali wana dhamana gani kama wataishi hata mwaka mmoja zaidi? Au mwezi mmoja zaidi? Au wiki moja zaidi? Au hata siku moja zaidi? Hawasomi kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):

(( وَمَا تَدْرِي نَفْسٌ مَّاذَا تَكْسِبُ غَدًا وَمَا تَدْرِي نَفْسٌ بِأَيِّ أَرْضٍ تَمُوتُ إِنَّ اللَّهَ عَلِيمٌ خَبِيرٌ))  

((Na haijui nafsi yeyote itachuma nini kesho. Wala nafsi yeyote haijui itafia nchi gani. Hakika Allaah Ndiye Mwenye kujua, Mwenye khabari)) [Luqmaan: 34].

Wengine wameshughulika na anasa za dunia na kujisahau kabisa kama huenda wakaondoka duniani wakiwa katika hali hizo za mapenzi ya dunia huku wameacha kutenda yaliyo muhimu kama ibada hii ya fardhi. Nafsi inayojidhulumu kama hivi hujuta wakati wa kutolewa roho yake, na hutamani arudi atende yale aliyoyakosa kutenda lakini kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):

((حَتَّى إِذَا جَاء أَحَدَهُمُ الْمَوْتُ قَالَ رَبِّ ارْجِعُونِ))

(( لَعَلِّي أَعْمَلُ صَالِحًا فِيمَا تَرَكْتُ كَلَّا إِنَّهَا كَلِمَةٌ هُوَ قَائِلُهَا وَمِن وَرَائِهِم بَرْزَخٌ إِلَى  يَوْمِ يُبْعَثُونَ))
((Mpaka yanapomfikia mmoja wao mauti, husema: Mola wangu Mlezi! Nirudishe))
((Ili nitende mema sasa badala ya yale niliyo yaacha. Wapi! Hii ni kauli aisemayo yeye tu. Na nyuma yao kipo kizuizi mpaka siku watapo fufuliwa)) [Al-Mu-minuun: 99-100].

Ni ‘Amali Bora Kabisa

  سئل النبي صلى الله عليه وسلم أي العمل أفضل؟ قال: ((إيمان بالله ورسوله)) قيل: ثم ماذا؟ قال: ((الجهاد في سبيل الله))" قيل ثم ماذا؟ قال: ((حج مبرور)) متفق عليه

Aliulizwa Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) Ipi amali njema kabisa? Akasema: ((Kumuamini Allaah na Mjumbe Wake)) Akaulizwa: "Kisha nini"? Akasema: ((Jihaad katika Njia ya Allaah)) Akaulizwa: "Kisha nini"? Aakasema: ((Hajj yenye kukubaliwa)). [Al-Bukhaariy na Muslim].


Hufutiwa Madhambi Yote

عن أبي هريرة رضي الله عنه  قال سمعت رسول الله صلى الله عليه وسلم يقول: ((من حج، فلم يرفث ولم يفسق، رجع كيوم ولدته أمه)) متفق عليه

Kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu 'anhu) ambaye amesema: "Nimemsikia Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: ((Atakayefanya Hajj, kisha asiseme maneno machafu wala asitende vitendo vichafu atarudi akiwa kama siku aliyozaliwa na mama yake)) [Al-Bukhaariy na Muslim].


Jazaa Yake Ni Pepo

عن أبي هريرة رضي الله عنه أن رسول الله صلى الله عليه وسلم قال: "((العمرة إلى العمرة كفارة لما بينهما، والحج المبرور ليس له جزاء إلا الجنة)) متفق عليه  

Kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu 'anhu) kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: (('Umrah hadi 'Umrah ni kafara (kufutiwa dhambi) baina yao, na Hajjul-Mabruur (Hajj yenye kukubaliwa) haina jazaa isipokuwa ni Pepo)) [Al-Bukhaariy na Muslim].

Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Awajaalie ndugu zetu wote Waislamu uwezo wa kutekeleza nguzo hii muhimu na Awalipe wote wanaojaaliwa kuitekeleza Pepo Yake Na'iym Aliyotuahidi. Aaamiyn.
***********************

Makosa Wanayofanya Mahujaji Mara Kwa Mara


 
Imetayarishwa na www.alhidaaya.com
 
MAKOSA YANAYOHUSU IHRAAM
Mahujaji wengine wanavuka kituo kilichoteuliwa kwa ajili ya ihraam katika njia za msafara wao bila ya kuwa katika hali ya ihraam au bila ya kuwa katika ihraam hapo. Wanaendelea hadi wanafika Jiddah au sehemu nyingine katika mipaka ya vituo ambako huko ndio wanaingia  katika hali ya ihraam.
Hivi ni kinyume na  amri ya Mjume wa Allah  (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ambayo inaamrisha kuwa kila Hujaji anapaswa aingie kwenye ihraam katika kituo kilichoko katika njia ya msafara wake.
Inapomtokea mtu hivyo, ni lazima arudi katika kituo chake cha  ihraam ili aingie katika ihraam. Au itambidi afanye kafara kwa kuchinja kondoo atakapokuwa Makkah na kuigawa nyama yote kuwalisha  masikini.
Hii inawahusu Mahujaji wote, wanaopita kituo wakiwa wamesafiri kwa njia ya angani, baharini au nchi kavu.
Ikiwa mtu hakupitia vituo vitano vilivyoteuliwa kwa ajili ya ihraam katika kila pande ya njia ya msafara, basi ni lazima aingie katika ihraam akiwa katika sehemu iliyo karibu na kituo cha ihraam kilichopo njiani kwake.

MAKOSA YANAYOHUSU TWAWAAF
1.       Kuanza twawaaf katika chanzo kingine kisichokuwa sehemu ya Hajarul-Aswad na hali ni fardhi kuanzia twawaaf hapo.
2.       Kufanya twawaaf ndani ya Hijr Ismaa'iyl.  Hii itamaanisha kwamba ni kuzungua sehemu tu ya Ka'abah na sio Ka'abah yote kwa vile Hijr Ismaa'iyl ni sehemu mojawapo ya Ka'abah yenyewe. Kufanya hivyo itakuwa imeachwa kufanywa twawaaf, na hivyo itakuwa twawaaf haikukamilika mzunguko wake. Twawaaf kama hii haifai.
3.       Kufanya ramal (yaani kupiga hatua ndogo ndogo za haraka) katika twawaaf zote saba na hali ramal inatakikana kufanywa katika mizunguko mitatu tu ya mwanzo ya twawaaful-quduum. 
4.       Kusukumana na watu na kusabisha zahma, kuwaumiza watu kutaka kulifikia Hajarul-Aswad ili kulibusu. Vitendo kama hivi vinaleta madhara kwa Waislamu na haturuhusiwi kufanya hivyo.
Itambulike kuwa twawaaf inabakia kuwa sahihi bila ya kulibusu Hajarul-Aswad. Ikiwa mtu hawezi kulifikia  au kulibusu Hajarul-Aswad, inamtosheleza Hujaji anapofika sambamba nalo kuashiria tu kwa mkono na kusema 'Allahu Akbar' japokuwa yuko mbali nalo.
5.       Hujaji kufuta au kusugua mkono wake katika Hajarul-Aswad akitegemea kupata baraka. Hili ni jambo lisilokuwa na dalili katika sheria ya Kiislam, hivyo ni bid'ah (uzushi). Sunnah ni kuligusa tu au kulibusu inapokuweko uwezekano wa kufanya hivyo bila ya taabu yoyote.
6.       Kugusa pembe nne za Ka'abah au kuta zake, kusugua na kujipangusa nayo kwa kutegemea kupata baraka. Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) hakugusa sehemu yoyote ya Ka'abah isipokuwa Hajarul-Aswad na Ruknul-Yaman.   
7.       Kusoma du'aa zilizotajwa kuwa ni maalum kwa kila twawaaf moja, na utakuta kuna vijitabu vidogo vidogo vyauzwa huko Makkah vyenye du'aa maalum kwa kila twawaaf, du'aa hizo za kwenye hivyo vijitabu hazina ushahidi wala asli katika mafunzo ya Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) isipokuwa chache sana. Ni bora mtu aombe yale yaliyothibiti na pia yale anayoyahitajia yeye zaidi kuliko kukariri du'aa za kwenye hivyo vijitabu ambazo hawaelewi hata maana zake. Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) hakueleza bayana du'aa yoyote isipokuwa ni kusema 'Allahu Akbar' anapofikia Hajarul-Aswad na kila anapomaliza twawaaf moja baina ya Ruknul-Yaman na Hajarul-Aswad akisoma:
رَبَّنَا آتِنَا فِي الدُّنْيَا حَسَنَةً وَفِي الآخِرَةِ حَسَنَةً وَقِنَا عَذَابَ النَّارِ
Rabbanaa Aatinaa Fid-Duniyaa Hasanataw-Wafil- Aakiharati Hasanataw-Waqinaa 'Adhaaban-Naar.
((Mola wetu Mlezi, tupe duniani mema, na Akhera mema, na utulinde na adhabu ya Moto)) [Al-Baqarah:201]
Sehemu nyingine katika mzunguko wa twawaaf, anaweza kusoma Aaya za Qur-aan, du'aa zilizothibitika katika Sunnah, Kumtukuza, Kumsifu, Kumpwekesha, Kumshukuru Allah, Kuomba maghfira, kumswalia    Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) n.k .  
8.         Kupandisha sauti kupita sauti za wengine aidha anapoongoza watu katika hizo du'aa ambazo watu wamejipangia au anapomfuata anayemuongoza. Kufanya hivyo kunasababisha kubabaisha mahujaji wengine ambao wanasoma du'aa zao pole pole, wasiweze kupata khushuu katika ibada yao wanapofanya twawaaf.
9.        Kujilazimisha kuswali Maqaam Ibraahiym wakati kuna zahma za watu. Hii ni kinyume na Sunnah, pia husababisha maudhi na misongomano ambayo huishia kuumizana na Mahujaji wengine. Inatosheleza kuswali Rakaa mbili baada ya kumaliza twawaaf mahali popote katika Masjidil-Haraam. 

MAKOSA YANAYOHUSU SA'Y
1.       Kwenye kupanda  kilima cha Swafaa na Marwah, baadhi ya mahujaji wanaelekea Ka'abah na kuiashiria kwa mikono wakisema 'Allahu Akbar' kama vile wanavyosema takbira ya Swalah. Kuashiria hivyo ni makosa kwa sababu Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alinyanyua mikono yake tu kuomba du'aa. Hapo unaweza kumtukuza Allaah (Subhaanahu kwa Ta'ala), kuomba du'aa yoyote ile upendayo huku umeelekea Ka'abah. Inapendekezeka kusoma dhikr ambayo Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliisoma katika Swafaa na Marwa nayo ni:

 لا إِلهَ إلاَّ  اللهُ وَحْدَهُ  لا شَرِيكَ لَهُ، لَهُ المُلْكُ وَلَهُ الحَمْدُ وهُوَ عَلى كُلِّ شَيءٍ قَديرٌ،
 لا إِلَهَ إلا اللهُ وَحْدَهُ أَنْجَزَ وَعْدَهُ، وَنَصَرَ عَبْدَهُ وَهَزَمَ الأَحْزَابَ وَحْدَهُ
Laa Ilaaha Illa-Allaah Wahdahu Laa Shariyka Laah, Lahul-Mulku Walahul-Hamd Wa Huwa 'Alaa Kulli Shay-in Qadiyr.  Laa Ilaaha Illa-Allaah Wahdahu, Anjaza Wa'dahu Wanaswara 'Abdahu Wahazamal-Ahzaaba Wahdahu))
   ((Hapana Mola Apasae kuabudiwa kwa haki ila Allah, hali ya kuwa peke Yake, wala Hana mshirika Wake, ni Wake Ufalme na ni Zake sifa njema Naye juu ya kila kitu ni Muweza.  Hapana Mola apasae kuabudiwa kwa haki ila Allah hali ya kuwa peke Yake, Ametekeleza ahadi Yake, na Amemnusuru mja Wake, na Amevishinda vikosi peke Yake))

2.     Kuchapuza mwendo katika masafa yote baina ya vilima viwili. Sunnah ni kuchapuza mwendo baina ya milingoti miwili ya kijani na kutembea mwendo wa wakawaida kwengine kote.

 MAKOSA YANAYOTENDEKA MINAA
1.    Mahujaji kupoteza muda wao katika mahema kwa kupiga soga badala ya kufanya dhikr au badala ya kuelimishana hapo mambo ya dini na hasa yanayohusu utekelezaji sahihi wa ibada hii ya fardhi. Mahujaji wengi kabisa wanafika huko kutekeleza fardhi hii wakiwa hawana elimu ya kutosha ya jinsi ya kuitekeleza ibada hii. Kwa hiyo kuelimishana ni jambo litakaloleta faida kubwa badala ya kupoteza muda kwa mambo yasiyofaa.
       Wengine wanafanya mambo ya bid-ah kama kusoma uradi kwa pamoja, na kusoma adhkaar zisizokuwa zenye dalili kutoka katika mafunzo ya Sunnah.
           
MAKOSA KATIKA KISIMAMO CHA 'ARAFAH
1.          Baadhi ya mahujaji wanapiga kambi nje ya maeneno ya 'Arafah na kubakia hapo hadi jua kuzama, kisha wanaelekea Muzdalifah bila ya kusimama 'Arafah kama inavyopasa. Hili ni kosa kubwa ambalo linabatilisha Hijja yao kwani kusimama 'Arafah ni kilele cha Hajj na pia ni fardhi kubakia ndani ya eneo la 'Arafah na si nje ya eneo lake.
2.          Kuondoka 'Arafah kabla ya jua kuzama hairuhusiwi kwa sababu Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alibakia 'Arafah hadi jua kuzama kabisa.
3.          Kujilazimisha katika zahma ya watu kupanda mlima wa 'Arafah hairuhusiwi, kwa sababu inasababisha madhara na madhara kwa Mahujaji wengine. Eneo lote la 'Arafah linahesabiwa kuwa ni kisimamo cha'Arafah, na si kupanda mlima wa 'Arafah wala kuswali katika huo mlima au karibu yake kuwa ndio idhaniwe kuwa mtu amepata  kisimamo cha 'Arafah.
4.          Kuomba du'aa akiwa anaelelekea mlima wa 'Arafah ni makosa kwa sababu Sunnah ni kuelekea Qiblah wakati wa kuomba du'aa.
5.          Kulundika chungu ya mchanga au vijiwe siku ya 'Arafah katika sehemu fulani, jambo ambao haliko katika sheria ya Allah.


MAKOSA KATIKA ENEO LA MUZDALIFAH

1.     Baadhi ya Mahujaji wanapofika tu Muzdalifah na kabla ya kuswali Swalah za Magharibi na 'Ishaa huanza kukusanya vijiwe vya kurusha katika nguzo za huko Minaa. 
Mawe hukusanywa popote katika maeneo ya al-Haram   Inajulikana kwamba Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) hakuamrisha mawe ya Jamaratul-'Aqabah yaokotwe Muzdalifah. Maswahaba walimuokotea yeye mawe asubuhi baada ya kuondoka Muzdalifah na kuingia Minaa. Aliokotewa mawe yaliyobakia yote kutoka Minaa pia.
2.     Baadhi ya Mahujaji huyaosha mawe. Sio pendekezo kufanya hivyo wala sio Sunnah.

MAKOSA KATIKA SEHEMU ZA KURUSHIA MAWE
Baadhi ya Mahujaji wanadhania kwamba kurusha mawe katika nguzo za Jamarah ni kumpiga shaytwaan, hivyo wanarusha mawe kwa nguvu na ghadhabu. Kurusha mawe kuna maana zifuatazo:
1.     Imekusudiwa kuwa ni njia ya kumkubuka Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala), ni jambo la kiibada.

2.     Wengine wanarusha mawe makubwa, viatu au mbao. Kufanya hivyo kote ni kuzidisha mambo ya dini ambayo Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ameharamisha. Vile vile ni kusababisha madhara ya Mahujaji wengine kwani mtu anaweza kurusha jiwe kubwa kwa mbali likampiga Hujaji aliye mbele yake badala ya kupiga nguzo.  Vijiwe vidogo vyenye ukubwa wa harage au kunde au choroko au punje za mahindi ndio bora zaidi kuvitumia.

3.     Kusababisha zahma, kusukumana na kugombana na wengine katika maeneo hayo ya nguzo hairuhusiwi. Inavyopasa ni kuwa na upole na kurusha vijiwe bila ya kumjeruhi mtu mwingine.

4.     Kurusha vijiwe vyote kwa mara moja ni makosa. Maulamaa wamesema kwamba hii itahesabika kuwa ni kama kurusha kijiwe kimoja. Sharia imetaja kurusha kijiwe kimoja baada ya kimoja na huku Hujaji anasema 'Allahu Akbar' kila kijiwe kimoja kinaporushwa.

5.     Kumuwakilisha mtu kurusha mawe, kwa sababu tu ya khofu ya zahma au tabu na mashaka, na hali Hujaji mwenyewe anao uwezo wa kufanya mwenyewe ibada hii hairuhusiwi. Wagonjwa tu na wale walio dhaifu ndio wanaruhusiwa kumuwakilisha mtu kufanya kitendo hiki.

 MAKOSA KATIKA KUZURU KABURI LA MTUME (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)

1.     Kugusa na kusugua mikono katika kuta na nondo za chuma, kufunga nyuzi katika mihimili yake na vitendo vingine vya namna hiyo wakati wa kuzuru kaburi la Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kwa kutegemea kupata baraka. Hivyo ni bid'ah. Baraka zinapatikana kwa kufuata amri za Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) na Mjumbe Wake (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na si kufuata mambo ya kuzushwa yasiyo na maana wala manufaa.

2.     Kwenda katika mapango ya Mlima wa Uhud au mapango ya mlima wa Hiraa au Thawr karibu na Makkah na kutundika vitambara au kuomba du'aa huko. Haya hayamo katika mafunzo ya kutekeleza fardhi hii. Na yote hayo ni kujitakia mashaka na tabu kwani ni mambo ya bid'ah katika dini na wala hayana msingi katika Sheria.

3.     Vile vile kuzuru sehemu nyingine kwa kudhania kuwa sehemu hizo ni athari za mabakio ya Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam). Mfano sehemu ambayo ngamia wake alikaa, au kisima cha 'Uthmaan na kukusanya udongo sehemu hizo kwa kutegemea kupata baraka, yote ni mambo ya bid'ah.

4.     Kuwaita waliokufa wakati wa kuzuru makaburi ya Al-Baqi'i au makaburi ya mashuhadaa wa Uhud na kurusha sarafu ili kutegemea kupata baraka za sehemu waliozikiwa watu ni makosa makubwa kabisa bali ni shirki kama walivyosema Maulamaa. Ni dhahiri pia katika Qur-aan na Sunnah ya Mjumbe Wake (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kwamba aina zote za ibada ziwe kwa ajili ya Allaah Pekee. Hairuhusiwi kumuomba mwingine au kuchinja, kuweka nadhiri au aina yoyote ya ibada isipokuwa ziwe kwa ajili ya Allah kwani Anasema:
((وَمَا أُمِرُوا إِلَّا لِيَعْبُدُوا اللَّهَ مُخْلِصِينَ لَهُ الدِّينَ حُنَفَاء))  
((Nao hawakuamrishwa kitu ila wamuabudu Allah kwa kumtakasia Dini)) [Al-Bayyinah:5]
Vile vile Anasema:
((وَأَنَّ الْمَسَاجِدَ لِلَّهِ فَلَا تَدْعُوا مَعَ اللَّهِ أَحَدًا))
((Na hakika misikiti ni ya Allah, basi msimuabudu yeyote pamoja na Allah)) [Al-Jinn: 18]
Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Awazidishie Waislamu elimu ya dini, na Atuepushe katika makosa, kuvuka mipaka ya sheria Yake na kufuata mambo ya bid'ah, hakika Yeye ni Mwenye kusikia na Mwenye kujibu du'aa zetu. Aamiyn*********************************

Fadhila Za Siku Ya 'Arafah Na Yawmun-Nahr (Siku Ya Kuchinja)




‘Arafah ni jabali ambalo alisimama Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kuwahutubia Maswahaba alipotekeleza Hijja ya kuaga. Na hapo ndipo wanaposimama Mahujaji kutimiza kilele cha ‘Ibaadah hii ya fardhi. Kusimama hapo ndio nguzo mojawapo kuu ya Hijjah bila ya kuweko hapo mwenye kuhiji atakuwa hakutimiza hijja yake kutokana na dalili  ifuatayo:

عن عبد الرحمن بن يعمر قال: قال رسول الله صلى الله عليه وسلم:  ((الْحَجُّ عَرَفَة ، مَنْ جَاءَ قَبْلَ طُلُوعِ الْفَجْرِ مِنْ لَيْلَةِ جَمْعٍ فَقَدْ أَدْرَكَ الْحَجّ))  صحيح الجامع   

Kutoka kwa ‘Abdur-Rahmaan bin Ya’mur ambaye amesema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): ((Al-Hajj ni ‘Arafah, atakayekuja kabla kutoka Alfajiri usiku wa kujumuika atakuwa ameipata Hajj)) [Swahiyh Al-Jaami’].


Fadhila Za Siku ya ‘Arafah:


1-Ni Siku Iliyokamilika Dini Yetu  

قال رجل من اليهود لعمر : يا أمير المؤمنين ، لو أن علينا نزلت هذه الآية : ((اليوم أكملت لكم دينكم وأتممت عليكم نعمتي ورضيت لكم الإسلام دينا)) لاتخذنا ذلك اليوم عيدا ، فقال عمر: "إني لأعلم أي يوم نزلت هذه الآية ، نزلت يوم عرفة ، في يوم جمعة"  البخاري

Kutoka kwa ‘Umar bin Al-Khattwaab (Radhiya Allaahu ‘anhu) kwamba Myahudi mmoja alimwambia: “Ewe Amiri wa Waumini, lau ingeliteremka kwetu sisi Aayah hii ((Leo Nimekukamilishieni Dini yenu na Nimekutimzieni Neema Zangu kwenu na Nimekuridhieni Uislamu kuwa ni Diyn yenu)) [Al-Maaidah (5: 3] tungeliifanya ‘Iyd siku hiyo. Akasema ‘Umar: “Hakika naijua siku gani imeteremka Aayah hii. Imeteremka Siku ya ‘Arafah siku ya Ijumaa” [Al-Bukhaariy)


Na ukamilifu wa dini siku hiyo ni kwa vile Waislamu hawakupata kutekeleza Hajj kabla ya hapo ya Kiislamu. Na kukamilika dini yao ni kukamilisha nguzo za Kiislamu zote.  


2-Kufunga Swawm ni kufutiwa madhambi ya miaka miwili:

Ni fadhila kubwa kwetu kujitakasa na madhambi tunayoyachuma kila siku kwani binaadamu daima ni mkosa.


عَنْ أَبِي قَتَادَةَ رضي الله عنه أن النَّبِيَّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ :  ((صِيَامُ يَوْمِ عَرَفَةَ أَحْتَسِبُ عَلَى اللَّهِ أَنْ يُكَفِّرَ السَّنَةَ الَّتِي قَبْلَهُ وَالسَّنَةَ الَّتِي بَعْدَهُ )) أخرجه مسلم

Imetoka kwa Abu Qataadah (Radhiya Allaahu 'anhu) ambaye amesema: Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kasema: “Swawm ya 'Arafah nataraji (kwa Allaah) kufuta madhambi ya mwaka uliopita na wa baada yake.” [Muslim]

Umuhimu huo wa kufunga na msisitizo ni kwa wasiohiji, na walio katika Hajj wao hakuna msisitizo huo kwa dalili ifuatayo:

عن ميمونة بنت الحارث: أن الناس شكوا في صيام النبي صلى الله عليه وسلم يوم عرفة ، فأرسلت إليه بحلاب ، وهو واقف في الموقف ، فشرب منه والناس ينظرون" البخاري

Kutoka kwa Maymuunah bint Al-Haarith (Radhiya Allaahu ‘anhaa) kwamba watu walitia shaka na Swawm ya Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa  aalihi wa sallam) [kama alifunga] Siku ya ‘Arafah, nikampelekea maziwa, naye akiwa amesimama akayanywa na huku watu wanamtazama.”  [Al-Bukhaariy]



3-Ni Siku Bora Kabisa Ambayo Wataokolewa Waja Kutokana Na Moto; Wataghufuriwa Madhambi Yao



عن  جابر  رضي الله عنه  عن النبي صلى الله عليه وسلم قال: ((مَا مِنْ يَوْمٍ أَفْضَلُ عِنْدَ اللَّهِ مِنْ يَوْمِ عَرَفَةَ، يَنْزِلُ اللَّهُ تَعَالَى إلَى سَمَاءِ الدُّنْيَا فَيُبَاهِي بِأَهْلِ الْأَرْضِ أَهْلَ السَّمَاءِ)) وروى ابن حبان
وفي رواية: ((إنَّ اللَّهَ يُبَاهِي بِأَهْلِ عَرَفَةَ مَلَائِكَتَهُ، فَيَقُولُ: يَا مَلَائِكَتِي، اُنْظُرُوا إلَى عِبَادِي، قَدْ أَتَوْنِي شُعْثا غُبْرا ضَاحِينَ))

Kutoka kwa Jaabir (Radhiya Allaahu ‘anhu) kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa  aalihi wa sallam) amesema: “Hakuna siku iliyo bora kabisa mbele ya Allaah kama siku ya ‘Arafah. Anateremka Allaah Ta’ala mbingu ya dunia (ya kwanza) kisha Anawafakhiri watu  ardhi  kwa watu wa mbingu.”


Na katika riwaaya nyingine: “Hakika Allaah Anawafakhiri watu ‘Arafah kwa Malaika Wake. Husema Husema Ee Malaika wangu, watazameni waja Wangu wamenijia wakiwa timtimu wamejaa vumbi …”

Pia,

 عن عائشة  رضي الله عنها عن النبي صلى الله عليه وسلم: ((ما من يوم أكثر من أن يعتق الله فيه عبيدا من النار من يوم عرفة ، وأنه ليدنو ، ثم يباهي بهم الملائكة فيقول : ما أراد هؤلاء ؟ اشهدوا ملائكتي أني قد غفرت لهم )) صحيح الترغيب

Kutoka kwa ‘Aaishah (Radhiya Allaahu ‘anhaa) kutoka kwa Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): “Hakuna siku Anayoacha Allaah kwa wingi huru waja kutokana na moto kama siku ya ‘Arafah. Na huwa karibu kisha Anajigamba kwao kwa Malaika na Husema: Wametaka nini hawa? Shuhudieni Malaika wangu kwamba hakika Mimi Nimewaghufuria)) [Swahiyh At-Targhiyb]
  

عن جابر  رضي الله عنه عن النبي صلى الله عليه وسلم-(( ما من أيام عند الله أفضل من عشر ذي الحجة قال فقال رجل يا رسول الله هن أفضل أم عدتهن جهادا في سبيل الله قال: (( هن أفضل من عدتهن جهادا في سبيل الله وما من يوم أفضل عند الله من يوم عرفة ينزل الله تبارك وتعالى إلى السماء الدنيا فيباهي بأهل الأرض أهل السماء فيقول انظروا إلى عبادي جاءوني شعثا غبرا ضاحين جاءوا من كل فج عميق يرجون رحمتي ولم يروا عذابي فلم ير يوم أكثر عتيقا من النار من يوم عرفة))   الترغيب والترهيب - إسناده صحيح أو حسن 

Kutoka kwa Jaabir (Radhiya Allaahu ‘anhu) kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Hakuna Siku iliyo bora kabisa kama siku kumi za Dhul-Hijjah, akasema mtu: “Ee Mjumbe wa Allaah, hizo ni bora au Jihaadi katika njia ya Allaah? Akasema: “Hizo ni bora kuliko Jihaad katika njia ya Allaah, na hakuna siku bora kabisa mbele ya Allaah, kama siku ya ‘Arafah, Anateremka Allaah Tabaaraka wa Ta’ala katika mbingu ya dunia kisha Anawafakhiri watu wa ardhini kwa watu wa mbinguni kisha Anasema: Tazameni waja Wangu wamenijia timtimu wamejaa vumbi wamekuja kutoka kila pembe ya mbali wanataraji Rehma Yangu na wala hawajaona adhabu Yangu. Na wala hakuona siku inayoachwa huru shingo kutokana na moto kama siku ya ‘Arafah.” [At-Targhiyb wat-Tarhiyb – Isnaad yake Swahiyh au Hasan]
  
  
4.    Siku Ya Kutakabaliwa Du’aa

Amesema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa  aalihi wa sallam):

 ((خير الدعاء دعاء يوم عرفة، وخير ما قلت أنا والنبيون من قبلي: لا إله إلا الله وحده لا شريك له، له الملك وله الحمد وهو على كل شيء قدير)) روى الترمذي
  
“Du’aa bora kabisa ni du’aa katika siku ya 'Arafah, na yaliyo bora kabisa niliyosema mimi na Mitume kabla yangu ni: 'Laa Ilaaha Illa Allaah Wah-dahu Laa Shariyka Lahu, Lahul-Mulku Wa-Lahul-hamdu Wa Huwa 'Alaa Kulli Shay-in Qadiyr – Hapana Mola apasaye kuabudiwa kwa haki ila Allaah, Pekee Hana mshirika, ufalme wote ni Wake, na Sifa njema zote ni Zake, Naye ni Mweza wa kila kitu daima.” [At-Tirmidhiy]




6-     Siku Ambayo Allaah Ameiapia

Allaah Ameiapia siku hii ya ‘Arafah ambayo inajulikana kwa ‘Siku ya Kushuhudiwa’. Hii kutokana na kauli Yake Subhaanahu wa Ta’ala:
بِسْمِ اللّهِ الرَّحْمَنِ الرَّحِيمِ  ((وَالسَّمَاء ذَاتِ الْبُرُوجِ))  (( وَالْيَوْمِ الْمَوْعُودِ))   ((وَشَاهِدٍ وَمَشْهُودٍ))
((Naapa kwa mbingu yenye Buruji!))  ((Na kwa siku iliyoahidiwa!)) ((Na kwa shahidi na kinachoshuhudiwa!)) [Al-Buruuj 85: 1-3]

Imetoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ‘anhu) kwamba Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa alihi wa sallam) amesema: “Siku ya kuahidiwa ni siku ya kufufuliwa. Siku ya kushuhudiwa ni siku ya ‘Arafah, na Siku ya kinachoshuhudiwa ni Siku ya Ijumaa)) [At-Tirmidhiy na imepewa daraja ya Swahiyh na Shaykh Al-Albaaniy]

7-Siku Ambayo Allaah Amechukua Fungamano (ahadi) Kutoka Kizazi Cha Aadam

Imesimuliwa kwamba Ibn ‘Abbaas (Radhiya Allaahu ‘anhumaa) amesema: Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa alihi wa sallam) amesema: “Allaah Amechukua fungamano kutoka mgongo wa Aadam katika Na’maan yaani ‘Arafah. Akalete mbele mgongo wake kizazi chake chote na akawatandaza mbele Yake.. Kisha Akawakabali kuwauliza:
 ((أَلَسْتَ بِرَبِّكُمْ قَالُواْ بَلَى شَهِدْنَا أَن تَقُولُواْ يَوْمَ الْقِيَامَةِ إِنَّا كُنَّا عَنْ هَذَا غَافِلِينَ)) (( أَوْ تَقُولُواْ إِنَّمَا أَشْرَكَ آبَاؤُنَا مِن قَبْلُ وَكُنَّا ذُرِّيَّةً مِّن بَعْدِهِمْ أَفَتُهْلِكُنَا بِمَا فَعَلَ الْمُبْطِلُونَ))
((Je, Mimi si Mola wenu? Wakasema: Kwani! Tumeshuhudia. Msije mkasema Siku ya Qiyaamah sisi tulikuwa tumeghafilika na hayo)) ((Au mkasema: Hakika baba zetu ndio walioshirikisha kabla yetu, na sisi ni dhuriya zao tu baada yao. Basi Utatuangamiza kwa sababu ya waliyoyafanya wapotovu?)) [Al-A’araaf 7: 172-173] [Imesimuliwa na Ahmad na imepewa daraja ya Swahiyh na Shaykh Al-Albaaniy]


Kutokana na fadhila hizo, ndio ikawa ni siku tukufu kabisa na siku ambayo ruknu ya Hajj kuu inatimizwa na bila ya mtu kusimama ‘Arafah inakuwa hakutekeleza Hajj.

Fadhila Za Yawmun-Nahr – Siku ya Kuchinja:
Siku kuu ya ‘Iydul-Adhw-haa na ndio inajulikana pia kwa Yawmun-Nahr.

Kasema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): 

((إن أعظم الأيام عند الله يوم النحر، ثم يوم الق))  أبي داود

“Siku iliyo tukufu kabisa kwa Allaah ni siku ya kuchinja, kisha siku ya kutulia”  (yaani siku ya kukaa Mina)  [Abu Daawuud]
Sababu ya kuchinja ni kufuata Sunnah ya baba yetu Nabii ‘Ibraahiym (‘Alayhis Salaam) alipotaka kumchinja mwanawe Ismaa’iyl na Allaah Akamteremshia badala yake kafara ya mnyama.

No comments: