Tuesday 25 August 2015

 
Mola wetu Mtukufu Amemuumba mwanaadamu katika umbo bora lisilomithilika na kiumbe chochote. Naye ameumbwa kwa kutumia udongo uliopulizwa roho itokayo kwa Mola Mlezi.
 
Akamjaalia mwanaadamu ni mwenye kupata shida, mitihani, mtenda dhambi na mwenye kupata maradhi. Hakusita hapo Mola wetu Mtukufu, bali Akajaalia mlango wa pili wa kutokea kwenye mashaka ya dunia; Akajaalia kuwepo starehe, utulivu, toba na afya. Basi ni kwa neema zipi mwanaadamu anaweza kumlipa Mola wake!?
 
Tutambue kwamba hii roho tuliyokuwa nayo yatosha kuwa ni sababu ya kushukuru neema za Mola Mlezi kwa vitendo na kauli. Tusisahau wapi tulipotoka na wapi tunaelekea, hatukuwa chochote miaka 100 iliyopita. Basi ni nani kati yetu alikuwa na uhakika kwamba atadhihiri duniani kwa jina na umbo lake kabla ya kuzaliwa? Kuwa na adabu kwa kumcha Mola wako!
 
Muislamu yupo juu ya mgongo wa ardhi akiruzukiwa kila chenye manufaa na yeye, ni mwenye kula akapata njia ya kutolea uchafu, na siku uchafu unaposhindwa kutoka ndani ya tumbo ndio unaelewa umuhimu wa neema ya kuyeyusha chakula kwenye mwili. Ameumba kila kitu kwenye kiwango maalumu, kwani tumbo likiyeyusha kupita kiwango, mwanaadamu ataugua maradhi ya tumbo la kumuendesha. Hivyo, kumbuka na yazingatie maneno ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala):
{{Na mkihesabu neema za Allaah hamtaweza kupata idadi yake. Hakika Allaah ni Mwingi wa kusamehe (na) Mwingi wa kurehemu.}} [An-Nahl: 18]
 
Basi elewa ndugu yangu, kwamba sisi si chochote si lolote zaidi ya tone la manii lililoengwa engwa hadi likafikia miezi tisa likaweza kutoka kwa sura ya mwanaadamu. Ndani ya tumbo, Mola wetu Mlezi Alitulinda na wala hatukuhitaji askari, jeshi, polisi, ultimate security au mwengineye. Ukatoka kwa ukenya wa kilio cha juu ukiomba msaada kwa mama yako. Ukafikia baleghe ukaweza kuoa/kuolewa na sasa kwa Qadar ya Mola unaweza nawe kupata mtoto. Aliyekuwa mbabe kati yetu azihesabu neema ngapi zimepita baina ya kuzaliwa kwake hadi hivi sasa, kisha aangalie ni kwa kiwango gani ataweza kuzishukuru neema hizo. SubhaanaLlaah! Yuko umbali gani mwanaadamu kwa kuzitilia maanani neema za Mola wake?
 
Ugeuze uso wako, uangalie mbingu ilivyotanda na ardhi ilivyotandikwa, kisha useme kwamba Mola wako amekutupa. Rizki zako Akazimimina kutoka mbinguni na Akazichimbua kutoka ardhini. Ni kipi basi katika chakula chako kitokacho nje ya mfumo huu? Basi kwa Kiburi Chake Mola Mlezi Anastahiki kuyaambia makundi ya wanaadamu na majini:
{{Enyi jamii ya majini na watu! Kama mtaweza kupenya katika mbingu na ardhi (ili mkimbie Nisikupateni), basi penyeni (Nikuoneni)! Hamtapenya ila kwa nguvu (Zangu. Nikikupeni nguvu hizo mtaweza).}} [Ar-Rahmaan: 33]
 
Tumcheni Mola wetu kwa kila kitu, kwa dogo na kubwa, kwa tunayoyajua na tusiyoyajua. Tutende mema kabla ya kutufika yale yasiyoweza kuhimili miili yetu. Wahenga wanatuambia: "Kijua ndi hichi usipouanika utaula mbichi."
 
 
 
Uchungaji wa viungo vya Muislamu katika maisha haya umekuwa ni wa chini usio na maana yoyote. Mkono unaiba, mguu unampeleka baa au kuzini, na ulimi unadiriki kutoa kiapo cha uongo.
 
Ulimi ni kiungo kimoja ambacho chatumiwa vibaya mno takriban na wanaadamu wote, na ndani yake kuna kundi kubwa la Waislamu ambao hawajali yale yanayotoka ndani ya vinywa vyao.
 
Tutambue kwamba, kiapo juu ya viumbe ni haki ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kuviapia. Ni kwa mfano pale Anaposema: Ninaapa kwa Siku ya Qiyaamah, Ninaapa kwa Jua na kadhalika. Mwanaadamu yeyote hana ruhusa ya kutoa kiapo kama hicho.
 
Kwa mujibu wa mafundisho ya Mtume wetu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kiapo cha Muislamu kinaelekezwa kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala). Na nini maana ya kiapo? Kiapo ni kuweka dhamana ya lile unalosema kwa Yule Unayemwapia. Kwamba hayo unayoyaapia ni ya kweli unahitaji kusadikiwa na wanaadamu wenzio. Basi ole wake yule ambaye anaweka kwa Muumba wake kiapo cha uongo.
 
Hivyo, kiapo ni chenye kuchungwa mno na wala sio kukifanya kuwa ni dhikri ya ulimi ukataka kila kitu kukifanyia kiapo hadi kuwa ni sababu ya kutumbukia kwenye dimbwi la moto. Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anatuambia tusimtii yule mwenye kuapa kila wakati:
{{Wala usimtii kila muapaji sana, aliye dhalili.}} [Suratul-Qalam: 10]
 
Kitu ambacho kimejaa ndani ya maisha yetu Waislamu ni viapo visivyokuwa na kichwa wala mguu. Na kila wanapokumbushwa wao wanaufanyia kazi ule msemo: "Kelele za mlango hazimughasi mwenye nyumba". Wanakuwa hawajali wala hawakubali maneno ya Qur-aan au Sunnah ya Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam).
 
 
Mtume wetu amekataza mno Muislamu kula kiapo ovyo ovyo. Kinyume chake Muislamu anakula kiapo cha uongo katika biashara ingawa Mtume wetu amesema kwamba Allaah Hatamuangalia (kwa jicho la huruma) mtu namna hiyo Siku ya Qiyaamah. [Imesimuliwa na Abu Dharr na kupokelewa na Muslim].
 
Lililo kubwa ndani ya jamii zetu ni kufikishana mbele ya vyombo vya sheria kwa namna za udanganyifu, utapeli na uongo mtupu. Muislamu anadiriki kuweka kiapo cha uongo kwa Mola wake ili apate mali ya mwengine bila ya halali. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesimuliwa akisema kama ilivyopokewa na Ummu Salamah (Radhiya Allaahu ‘Anha):
 
((Mimi ni binaadamu tu na nyinyi mnaleta migogoro yenu kwangu mimi, mukiwa wenye fasaha katika viapo vyenu kuliko wengine, ili ya kwamba nitoe hukumu kwa niaba yenu kwa mujibu wa ninayoyasikia kutoka kwenu. Hivyo, vyovyote nitakavyoamua kwa yeyote, ambapo kwa haki ni ya ndugu yake, asichukue kwani simpatii chochote ila kipande cha moto.))
[Imepokewa na Al-Bukhaariy].
 
Tunawanasihi wale waliochukua viapo vya uongo wakamilikishwa mali kwa njia za haramu wazirejeshe amana hizo haraka iwezekanavyo. Ya Ar-Rahmaan! Na wapo miongoni mwa viumbe Vyako waliokula kiapo kwa kudhulumu mayatima na wakala kiapo kwa lengo la kuzini na wake za watu. Umetakasika! Shingo zao zipo mikononi Mwako!
 
Ya Allaah! Tunategemea kwako, na tunageuka kuja Kwako, na Kwako tu ndiko marejeo yetu. Basi tunakuomba Mola wetu! Tutimizie nuru yetu, na Utughufirie, hakika Wewe ni Mwenye uweza juu ya kila kitu.
 

Toa Swadaqah Kwa Ajili Ya Allaah

 
Naaswir Haamid
 
 
Ihsaan ni kinyume cha ufisadi, na miongoni mwa Ihsaan ni kufanya wema bila ya kujali mipaka ya Kaskazi wala Kusi, na kutoa kwa ajili ya Allaah ni wema na Ihsaan kwa mwanaadamu.
 
Hakuna shaka yoyote kwamba Swadaqah ni katika tabia njema, na iwapo tutafungua kurasa za Siyrah za wema waliotangulia, tutaona kwamba walikuwa wakikithiri mno kwenye kutoa Swadaqah. Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anasema:
{{Chukua Swadaqah katika mali zao, uwasafishe na kuwatakasa kwa ajili ya hizo (Swadaqah zao).}} [At-Tawbah: 103]
 
Kupitia Tamko hilo hapo juu, tunafahamu kwamba kumbe kuisafisha nafsi kutokana na takataka za upungufu na kuiinua jamii mpaka kuifikisha kwenye daraja tukufu kabisa, ndio hekima ya juu. Ni kwa ajili hii ndio Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alipanua wigo katika kuelezea maana ya neno “Swadaqah” ambayo Muislamu anatakiwa kuitoa, akasema:
((Tabasamu lako usoni kwa nduguyo (Muislamu mwenzio) ni Swadaqah, kuamrisha kwako mema na kukataza kwako maovu ni Swadaqah. Na kumuongoza kwako njia mtu katika ardhi (nchi) ya upotevu, hilo kwako ni Swadaqah. Na kuondosha kwako njiani udhia, mwiba na mfupa, hilo kwako (nalo) ni Swadaqah. Na kumtekea kwako maji nduguyo, kwako ni Swadaqah na kumsaidia kwako mtu dhaifu wa uoni kuongoza njia, (hilo nalo) kwako ni Swadaqah)). [Al-Bukhaariy]
 
Swadaqah huanza kwa kuuzoesha mkono kutoa kila mara bila ya kinyongo wala manuuniko. Mkono una dhima kuu ya kukulingania kutoa Swadaqah katika vile ulivyoruzukiwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kama Alivyosema:
{{Yule anayetoa (Zakaah, Swadaqah na vinginevyo) na kumcha Allaah. Na kusadiki jambo jema (akalifuata). Tutamsahilishia njia ya kwenda Peponi.}} [Al-Layl: 5-7]
 
Hiyo ndio faida na jazaa ya aliyeutumia vyema mkono wake katika kutoa Swadaqah. Akautumia mkono wake katika kutoa vile Alivyoruzukiwa na Allaah Ar-Razzaaq, katika kuisadia jamii na kuupeleka mbele Uislamu.
 
Ni vyema ukakumbuka kwamba kutoa katika mambo ya khayr ni katika kuishukuru neema ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala). Ambako hakumaanishi ila kuzidishiwa neema, tusome kwa mazingatio:
{{Na (kumbukeni) Alipotangaza Mola wenu (kuwa): "Kama mkishukuru, Nitakuzidishieni; na kama mkikufuru, (jueni) kuwa adhabu Yangu ni kali sana.}} [Ibraahiym: 7]
 
"Mtenda wema hutendea nafsi yake na mtenda ovu humrejea mwenyewe". Hivyo elewa kamba kuishukuru neema kikweli kweli na kuitumia vile inavyostahiki sio tu kusema au kuandika kwenye milango kwa mbwembwe: ‘AlhamduliLlaah’ au ‘Hadha Min Fadhli Rabiy’! Na ni ubaya ulioje kuzitumia neema hizi kinyume na vile Alivyoamrisha Ar-Razzaaq.
Dunia ni tamu na kawaida ya mwanaadamu kupenda mazuri mno. Hujitahidi kadiri ya juhudi zake kukusanya yale ayaonayo kuwa ni yenye kufurahisha nafsi yake. Hutafuta yale yenye laghai na anasa - 'material world'.
 
Hilo halina shaka na hata Qur-aan na Sunnah yatuthibitishia kwamba dunia imeumbwa kuunganishwa na matamanio ya mwanaadamu. Lakini sio yote ambayo Muislamu anatakiwa kuyatilia mkazo kwa kuyavamia. Ndio lengo la kuwepo halali na haramu ndani ya Uislamu ili kumtofautisha mwanaadamu na Muislamu.
 
Waislamu walio wengi kabisa wanatamka shahaadah ya kwamba Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) ni Mmoja na Ndiye Apaswaye kuabudiwa pamoja na kutiiwa Mtume Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam). Kikomo cha wengi kinamalizia hapa kwenye kauli tu. Matendo yao yanakuwa kinyume na kauli hii. Hivyo, hufanya ibada kwa kudanganya macho ya waumini, kwani wanatenda mbele ya kadamnasi, wanapokuwa peke yao huingia kwenye hiyo 'material world' kwa mapana na marefu. Hiyo sio iymaan inayopigiwa mfano na Mola Mlezi:
 
{{Ambao wanamuogopa Mola wao (hata) wanapokuwa faraghani, na pia hukiogopa Qiyaamah.}} [21:49]
 
Taariykh yatufunza kwamba Waislamu hapo kale walilelewa kwenye Tawhiyd ya kumuamini Allaah pamoja na Malaika, Mitume, Vitabu, Siku ya Mwisho, Qadar kheri na shari. Kwa wakati wa sasa ni Kitabu cha Qur-aan pekee ndicho kilicho mbele ya macho yetu. Vilivyobaki vyote vinabaki kuwa nyuma ya pazia 'ghayb'.
 
Imesimuliwa kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ‘Anhu): amesema Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kwamba:
"Iymaan ni kumuamini Allaah, na Malaika Wake, na Vitabu Vyake, na Kukutana Kwake (Siku ya Qiyaamah), na Mitume Wake na kuamini ufufuo wa Siku ya Mwisho." (Imepokewa na Shaykhaan)
 
Kukosa kuamini moja ya nguzo za iymaan, kunapelekea kutoamini ghayb. Hivyo, kuanguka kwa iymaan ya ghayb kutasababisha kuondoka iymaan ya kwamba Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Yupo.
 
Ni ghayb hii inayomfanya mwanaadamu na hata Muislamu kutotilia mkazo kuutafuta ukweli halisi wa Uislamu, ghayb ndiko kunakomfanya Muislamu kutotenda mema kwa lengo la kupata ridhaa ya Allaah. Thawabu wala dhambi hazioni mtu, Malaika wanaoandika mema na maovu nani anayewaona? Haya yote yapo kwenye ghayb. Muislamu anatakiwa kuamini hii ghayb bila ya mjadala. Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Anatuambia:
 
{{Tendeni mambo (mazuri). Allaah Atayaona mambo yenu hayo na Mtume Wake na Waislamu. Na mtarudishwa kwa Mjuzi wa siri na dhahiri; Naye Atakwambieni (yote) mliyokuwa mkiyatenda.}} [9:105]
 
Apambanue Muislamu juu ya kukosa kwake iymaan ya ghayb na kuirudisha nyuma akili kabla ya kuwepo kwake; yeye alikuwa ni nani? Nani aliyemhifadhi ndani ya tumbo la mama kwa miezi tisa? Hivyo, ghayb ni wajibu kuiamini na kwamba yapo mambo nyuma ya macho yetu yanatokea au yapo tayari kutokea.
 
Kukosekana kwa iymaan ya ghayb ndani ya nafsi ya Muislamu ndio kwamfanya awache himma ya kutenda mema. Ni sababu hii inayowafanya vijana walio wengi kujishughulisha mno na ratiba za mipira inayokula muda wa Waislamu. Nao kina dada kutilia mkazo urembo, mikusanyiko ya haramu na kutembea kwao utupu kunatokana na kukosa kwao kuamini ghayb.
 
Basi na aangalie Muislamu alivyoumbwa, chakula chake kinavyoyayushwa na kugaiwa sehemu mbali mbali. Vitamini, damu, madini, sukari, chumvi, mafuta na vyengineo; vyote vinapelekwa na kuhifadhiwa sehemu zake maalum. Atupe jicho lake kwa kuangalia linapotoka na kuzama jua, tofauti ya usiku na mchana, hali ya uzima na ugonjwa, maisha na mauti na mengineyo:
 
{{Naye ndiye Aliyeziumba mbingu na ardhi kwa haki. Na wakati Anaposema (kuliambia jambo): "Kuwa," basi huwa… Mjuzi wa ya siri na dhahiri…}} [6:73]
 
Basi ni mengi yaliyopo Mkononi Mwako yaa Allaah! Namna tutakavyojifunza katu hatutafikia chembe ya 'ilmu Yako. Hivyo, tunatamka kama ambavyo Umetufunza:
 
{{Wewe Umetakasika na kuwa na mshirika. Hainijuzii mimi kusema ambayo si haki yangu. Kama ningalisema bila shaka Ungalijua; Unayajua yaliyomo nafsini mwangu, lakini mimi siyajui yaliyomo nafsini Mwako; hakika Wewe Ndiye Ujuaye mambo ya ghayb.}} [5:116]

Wasiya Wa Pili Wa Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) – Swalaah Ya Adhw-Dhwuhaa.

Imetajwa pia katika Hadiyth ya Abu Ad-Dardaai kwamba Rasuli wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amemuusia naye mambo matatu kama aliyomuusia Abu Hurayrah (Radhwiya Allaahu ‘anhu), nayo ni: Swiyaam (kufunga) siku tatu, kuswali Swalaah ya adhw-dhwuhaa na kuswali Swalaah ya Witr kabla ya kulala,
وعَنْ أَبِي الدَّرْدَاءِ رضي الله عنه قَالَ : "أَوْصَانِي حَبِيبِي صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ بِثَلَاثٍ لَنْ أَدَعَهُنَّ مَا عِشْتُ : بِصِيَامِ ثَلَاثَةِ أَيَّامٍ مِنْ كُلِّ شَهْرٍ، وَصَلَاةِ الضُّحَى  وَبِأَنْ لَا أَنَامَ حَتَّى أُوتِرَ"   رواه مسلم  
Imepokelewa kutoka kwa Abu Ad-Dardaai (Radhwiya Allaahu ‘anhu) kwamba: “Ameniusia mpenzi wangu Swalla Allaahu ‘alayhi wa sallam [mambo] matatu nisiyaache maishani mwangu; Swiyaam (kufunga) siku tatu kila mwezi na Swalaah ya Adhw-Dhwuhaa na nisilale mpaka niswali Witr” [Muslim]

Swalaah ya Adhw-Dhwuhaa – Fadhila zake, idadi ya raka’ah zake na wakati wake:

Ukumbusho Wa Swiyaam (Funga) za Ayyaamul-biydhw (Masiku meupe) Dhul-Qa'dah 1436H

SWIYAAM (FUNGA) SIKU TATU KILA MWEZI THAWABU ZAKE NI SAWA NA THAWABU ZA SWIYAAM YA MWAKA!
Tunapenda kuwakumbusha Swiyaam (funga) za Ayyaamul-biydhw (masiku meupe) ambayo ni tarehe 13, 14, 15 katika kila mwezi wa Kiislaam (Hijriyyah). Masiku hayo mwezi huu wa Dhul-Qa’dah 1436H, yataangukia tarehe 28, 29, 30 August (Ijumaa, Jumamosi, Jumapili). Bonyeza 'Endelea' upate fadhila kadhaa za Ayyaamul-biydhw na fadhila za Swiyaam siku tatu kila mwezi, pamoja na fadhila za Swiyaam kwa ujumla.  Soma  na utekeleze ili ufaidike na ujichumie thawabu tele In Shaa Allaah.  Na hakuna tawfiyq isipokuwa ya Allaah ‘Azza wa Jalla, Kwake tunatawakali na Kwake tunarudia kutubia.

Nasiha Za Minasaba Mbali Mbali

Tumeingia Katika Miezi Mitukufu Inatupasa Kuitakasa Kwa Kuacha Maovu Na Kuzidisha Mema

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):
((إِنَّ عِدَّةَ الشُّهُورِ عِندَ اللّهِ اثْنَا عَشَرَ شَهْرًا فِي كِتَابِ اللّهِ يَوْمَ خَلَقَ السَّمَاوَات وَالأَرْضَ مِنْهَا أَرْبَعَةٌ حُرُمٌ ذَلِكَ الدِّينُ الْقَيِّمُ فَلاَ تَظْلِمُواْ فِيهِنَّ أَنفُسَكُم))

((Hakika idadi ya miezi kwa Allaah ni miezi kumi na mbili katika hukumu ya Allaah, tangu Alipoumba mbingu na ardhi. Katika hiyo iko minne mitakatifu. Hiyo ndiyo Dini iliyo sawa. Basi msidhulumu nafsi zenu humo)) [At-Tawbah: 36].

Miezi minne hiyo imetajwa katika Hadiyth ifuatayo:
  عَنْ أَبَى بَكْرَة أَنَّ رَسُول اللَّه - صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ - قَالَ فِي حَجَّة الْوَدَاع : ((إِنَّ الزَّمَان قَدْ اِسْتَدَارَ كَهَيْئَتِهِ يَوْم خَلَقَ اللَّه السَّمَوَات وَالْأَرْض السَّنَة اِثْنَا عَشَر شَهْرًا مِنْهَا أَرْبَعَة حُرُم : ثَلَاث مُتَوَالِيَات ذُو الْقَعْدَة وَذُو الْحِجَّة وَالْمُحَرَّم وَرَجَب مُضَر الَّذِي بَيْن جُمَادَى وَشَعْبَان)) صَحِيح الْبُخَارِيّ

491- Hakuna Mjinga Mkubwa Katika Dini Kama Huyu! - ´Allaamah al-Luhaydaan