Islam Tanzania

Alichokifanya Nyerere baada ya uhuru Kilichofuata baada ya kupatikana uhuru ilikuwa ni kukamatwa, kuwekwa kizuizini na kuhamishwa kwa masheikh na Waislamu wengine waliodhaniwa kuwa wanapinga utawala wa Nyerere.
Mashuhuri miongoni mwao walikuwa: Abdillah Schneider Plantan, Sheikh Abdulkarim Abdulwahid, Maalim Popo Saleh, Suleiman Masudi Mnonji, Ali Migeyo, Mufti Sheikh Hassan bin Amir, Sharff Hussein Badawiy, Shariff Mwinyibaba na Shariff Adnan
Wengine ni Bilali Rehani Waikela, Sheikh Jumanne Bias, Maalim Matar, Abdalah Mwamba, Sheikh Hashim Haji Abdallah, Sheikh Nurdin Hussein, Salum Abdallah Popo, Sheikh Mzee Ali Comoriam, Sheikh Al Amin Maftah, Rajab Kiguu cha Mbuzi na wengine wengi.
Lakini ukweli ulikuwa kwamba si wote katika wale waliokamatwa na kuwekwa kizuizini walijihusisha na siasa. Baadhi yao walikamatwa kwa sababu tu walikuwa wakishirikiana na wale waliodhaniwa ni wapinzani wa Nyerere.
Maalim Matar na Shariff Adnan walifungwa jela kwa sababu tu walihusika na msikiti wa Badawiy mjini Dar es Salaam ambako Sheikh Hassan bin Amir, wakati huo akichukuliwa kuwa ndiyo roho ya waumini wa Tanganyika, alikuwa ikiendesha madrasa yake kila magharibi pale msikitini.
Shariff Hussein na nduguye Mwinyibaba walihamishiwa Kenya, walikotoka si kwa sababu walikuwa wamejishughulisha katika harakati za kuipinga serikali, ila lakini kwa sababu walikuwa waangalizi wa msikiti wa Badawiy.
Sheikh Mzee Ali Comorian alitiwa kizuizini kwa sababu kila mara alikuwa akifuatana na Sheikh Hassan bin Amir kama vile alikuwa kivuli cha sheikh. Huenda kile kilichomfanya Nyerere kuwatia kizuizini masheikh na wengine kuhamishwa ni kufuata ule msemo wa Biblia usemao, 'yule ambae hayuko nasi basi ni dhidi yetu'.
Jinsi siasa na za Tanzania zilivyobadilika na jinsi Nyerere alivyoanza kuonesha uadui dhidi ya Waislamu kulimsikitisha sana Abdulwahid. Alishindwa kuelewa uhasama huu ulikuwa unatoka wapi. Alihisi kuwa anahusika na yale yaliyokuwa yanawapata Waislamu. Mawazo haya yalimzonga kama jinamizi. Kwa ufahamu wake alikuwa akidhani matatizo yote ya udini walikuwa wameyashinda toka miaka ya 1950. Mwaka 1953 Abdulwahid akiwa Muislamu na akiungwa mkono na Al Jamiatul Islamiyya aligombea kiti cha urais wa TAA na Nyerere, Mkatoliki.
Abdulwahid alishindwa uchaguzi ule. Waislamu hawakuuchukulia uchaguzi ule kama uchaguzi kati ya Muislamu na Mkristo. Kilichotazamwa ni uwezo wa wagombea.
Nyerere alikuwa amemzidi Abdulwahid na kwa ajili hii alichaguliwa kuiongoza TAA. Abdulwahid alikumbuka ugomvi wa Sheikh Suleiman Takadir wakati ule Mwenyekiti wa Baraza La Wazee wa TANU. Sheikh Takadir aliwaonya Waislamu wachukue tahadhari kwani Nyerere atakuja kuwapendelea Wakristo wenzake pale atakaposhika madaraka. Kama walivyofanya Waislamu wengi, Abdulwahid alimuunga mkono Nyerere na kumpinga Sheikh Takadir.
Wakati ule Abdulwahid aliamini kama Waislamu wengi walivyoamini kuwa Sheikh Takadir alikuwa anataka kuleta siasa za kibaguzi ambazo alikuwa anaziegemeza katika dini. Abdulwahid aliona udini aliokuwa anataka kuuleta Sheikh Takadir lilikuwa jambo ambalo lingeiletea hatari Tanganyika.
Abdulwahid alikufa mwaka 1968 wakati nchi ikiwa imegubikwa na hasama za chinichini kati ya Waislam dhidi ya serikali ya Nyerere ambae sasa alikuwa amehodhi madaraka yote katika serikali.
Umoja wa kitaifa, moja ya maadili ambayo yeye(Abdulwahid ) aliyapigania katika maisha yake yote katika siasa ulikuwa unahatarishwa. Halikadhalika umoja wa Waislamu ulikuwa unaelekea kuvunjika. Kulikuwepo na kuwekwa kizuizini kwa masheikh chini ya Preventive Dentation Act of 1962.
Baadhi ya masheikh waliotiwa gerezani walikuwa watu waliomuunga yeye mwenyewe mkono wakati anaunda TANU. Baadhi yao aliwashawishi kumuunga mkono Nyerere na TANU katika kile kipindi kigumu cha harakati za kudai uhuru. Mwanakamati wa Kamati Ndogo ya Siasa ya TAA, Mufti Sheikh Hassan bin Amir, kiongozi wa ngazi ya juu kabisa kwa Waislamu alikuwa amekamatwa na kuondolewa nchini na kurudishwa kwao Zanzibar kwa amri ya Nyerere. Sababu iliyotolewa ya kukamatwa kwa Sheikh Hassan bin Amir ilikuwa alikuwa ati 'akipanga njama ya kupindua serikali'.
Sheikh Hassan bin Amir alikuwa kati ya Waislamu wachache ambao walithubutu kusimama kidete dhidi ya serikali na kutoa mawazo yake kuhusu jinsi serikali ilivyokuwa ikiwakandamiza Waislam. Kabla hajafa Abdulwahid alikuwa akifikiwa na habari kuwa Nyerere alikuwa alikuwa akiendesha kampeni makini sana ndani ya chama kuwafuta Waislamu ndani ya TANU.
Abdulwahid alikuwa anafahamu matokeo ya kuvunjika kwa umoja wa Waislam. Yeye alikuwa anajua vyema nguvu ya umoja wa Waislamu wakati walipokuwa wanapigania uhuru wa Tanganyika.
Abdulwahid halikadhalika alikuwa anafahamu nguvu ya wale waliokuwa nyuma na njama zile za kuwagawa Waislamu katika makundi hasimu. Vilevile alikuwa anatambua hofu na watu wote waliokuwa nyuma ya njama zile.
Alifahamu kuwa wale aliowapokea na kuwatia katika harakati za kudai uhuru sasa walikua na hofu na Uislam. Kama Uislamu ulitumika kuwaondoa wakoloni Uislam hautashindwa kuwatoa wao madarakani. Uislam ikiwa itkadi ya kupinga ukoloni sasa ilikuwa ni tishio kwa Ukristo katika Tanzania huru.
Kabla hajafariki dunia Abdulwahid alifanya mazungumzo na Nyerere. Mazungumzo haya baina ya Abdulwahid na Nyerere yalifanyika katika miezi ya mwisho ya mwaka 1968 wakati mashekhe na Waislamu mashuhuri wanasombwa na kutupwa gerezani. Abdulwahid na Nyerere walikuwa wametoka mbali. Watu hawa walikuwa marafiki wa zamani. Huenda kama isingelikuwa kwa msaada wa Abdulwahid historia ya TANU na ya Nyerere mwenyewe zingechukua mkondo tofauti.
Mazungumzo haya yalikuwa muhimu kwa Abdulwahid kwa sababu kwa kiasi fulani alihisi anahusika na yale yaliyokuwa yakiwasibu Waislamu, wale kutoka Dar es Salaam. Taarifa za Waislamu kukamatwa usiku na kuwekwa kizuizini zilikuwa zikimfikia karibu kila siku. Abdulwahid hakuweza kujifanya kuwa haathiriki na matokeo yale. Baadhi ya watu ambao Nyerere alikuwa anawatupa gerezani walikuwa watu ambao yeye Abdulwahid binafsi walimuunga mkono wakati anaanza siasa na watu ambao aliwashawishi wamkubali Nyerere wakati wa kuundwa TANU.
Abdulwahid alimwambia Nyerere huenda yeye akawa hana hisia wala uhusiano wowote na watu ambao yeye anatia sahihi wakamatwe na kutupwa gerezani. Lakini kwake yeye hao ni jamaa zake anaokutananao ama msikitini au mitaani. Yeye kama mtu anayeishi miongoni mwa Waislamu na zile familia zao alikuwa anaelewa majonzi yao.
Abdulwahid alimwambia Nyerere kwamba watu wale wanajua kuwa yeye, Abdulwahid ndiye aliyesamsaidia Nyerere wakati akiwa mgeni mjini Dar es Salaam, watu wakamjua na kumkubali na hivyo kuja kuweza kufika hapo alipofika.
Abdulwahid alimwambia Nyerere kuwa ndugu na jamaa za wafungwa wale wanamjia wakimbembeleza amsihi Nyerere awatoe ndugu zao jela. Abdulwahid alimwambia Nyerere kwamba kule kuwatia watu kizuizini ni uonevu kwa sababu wale watu hawana uwezo wa kupindua serikali yake.
Kwa sauti ya masikitiko Abdulwahid alimaliza maelezo yake kwa kumwambia Nyerere 'Naondoka hapa nikiwa nataka kuamini kuwa wewe Julius Nyerere, leo hujatugeuka.' Kwa maneno hayo Abdulwahid aliaga na kuondoka.
Alichosikia Nyerere kuhusu Abdulwahid baada ya maneno yale ilikuwa taarifa ya kifo chake jioni moja Jumamosi tarehe 12 Oktoba, 1968. Mkewe Mama Maria Nyerere, alizirai aliposikia habari zile za msiba. Alikuwa Abdulwahid ndiye aliyewapokea yeye na mume wake mara ya kwanza walipokuja Dar es Salaam.
Mazishi ya Abdulwahid Sykes yalifanyika siku ya Jumapili tarehe 13 Okrtoba. Mazishi yake yalikuwa makubwa yasiyo kifani. Ukitoa mazishi ya mwaka 1950 ya Sheikh Idrissa bin Saad, muasisi na Khalifa wa Tariqa Askariya na mazishi ya Sheikh Kaluta Amri Abeid mwaka 1963, Dar es Salaam ilikuwa haijapata kushuhudia mazishi kama hayo. Gerezani yote ambako Abdulwahid aliishi katika utoto wake na mahali ambapo alianza harakati zake dhidi ya Waingereza ilikuwa kama vile imesimama hakuna kinachoendelea ila maziko ya Abdulwahid. Hii ilikuwa pamoja na sehemu nyingine zilizozunguka Kariakoo kama Misheni Kota na Kisutu.
Gerezani kwa hakika ilikuwa na mwito wa pekee. Ilikuwa ni kutoka Gerezani ndipo walipotoka wanaharakati wa mwanzo waliounda TANU ukimtoa John Rupia. Siku hiyo Gerezani ilikuwa imekuja kumzika shujaa wao. Watu walianza kukusanyika nyumbani kwa mama yake, Abdulwahid Bibi Mluguru bint Mussa mapema asubuhi ambako maiti ilipokuwa imepelekwa. Ilipofika adhuhuri ikawa kama vile Dar es Salaam nzima imekusanywa pale. Chifu wa Unyanyembe Abdallah Said Fundikira, ambae Abdulwahid alisomanae darasa moja katika shule ya serikali mjini Dar es Salam katika miaka ya 1930 na mtu ambae walikwenda wote kuhiji Maka alikuja Dar es Salaam kwa ndege kutokea Nairobi kuja kuhudhuria mazishi.
Inasemekana Nyerere hakutaka kuja kwenye mazishi ya Abdulwahid kwa kuwa wakati ule ndiyo kulikuwa na lile tatizo la EAMWS na masheikh walikuwa wakikamatwa nyakati za usiku na kutupwa jela. Usalama wa Taifa unasemekana ulimshauri Nyerere kwa usalama wake kutohudhuria mazishi yale kwa sababu mazishi ya Abdulwahid yatahudhuriwa na Waislamu wengi. Chuki za Waislamu dhidi ya Nyerere kwa wakati ule zilikuwa juu sana.
Rashid Kawawa aliyekuwa Makamo wa Rais alipopata habari zile kuwa Nyerere hatofika mazishini haraka alimwendea Nyerere na kumwabia kuwa kabla hajachukua uamuzi wa kutokwenda yeye atakwenda kuangalia hali ya mambo yalivyo pale msibani kisha atarudi kumpa habari kamili.
Aliporudi kwa Nyerere Kawawa alimwambia Nyerere kuwa umma uliokuja kumzika Abdulwahid haujapata kuonekana. Chifu Fundikira amekuja kutoka Nairobi kuja kumzika Abdulwahid. Watu wa Dar es Salaam hawatamwelewa kama yeye Nyerere yupo Dar es Salaam na ashindwe kwenda kwenye mazishi yake. Watu wa Dar es Salaam wengi wao wanakumbuka kwa mara ya kwanza kumuona Nyerere akiwa amefuatana na Abdulwahid na wanafahamu hisani aliyomfanyia Nyerere. Nyerere aliona busara ya Kawawa na palepale ikatoka amri kuwa ulinzi katika mazishi ya Abdulwahid uimarishwe na Nyerere atakwenda kumzika rafiki yake aliyempokea na kumuunga mkono wakati ule wa kipindi kigumu cha kuasisi TANU.
Rais Nyerere akawa mmoja wa watu waliokwenda kuomboleza kifo cha Abdulwahid. Akitembea kwa miguu Nyerere alilifuata jeneza la Abdulahid nyuma kutoka Mtaa wa Lindi, Gerezani hadi Msikiti wa Kitumbini maiti ilipokwenda kuswaliwa swala ya jeneza kama ilivyo ada ya Kiislamu.
Pale Kitumbini, Nyerere alisimama nje ya msikiti pamoja na Wakristo na wananchi wengine kungojea maiti ilitolewe nje. Mfanyabiashara mmoja wa Kiasia kuona rais amesimama wima, kwa ajili ya heshima alileta kiti na kumuwekea Nyerere akae. Nyerere alikataa kukaa na akawa amesimama pamoja na watu wengine. Kutoka Kitumbini msafara wa maziko ulielekea makaburi ya Kisutu kwa ajili ya mazishi.
Chifu Fundikira alikuwa mmoja wa watu walioingia kaburini kuupokea mwili wa Abdulwahid. Wakati huu wote wakielekea makaburini, Nyerere alikuwa nyuma ya jeneza kichwa chake amekiinamisha na kila wakati alionekana akifuta macho yake na kitambaa.
Nyerere alikuwa analia. Ilikuwa mwaka 1952 Abdulwahid alipofahamiana na Nyerere na yeye Abdulwahid akamjulisha kwa watu mashuhuri wa Dar es Salaam ­ Mufti Sheikh Hassan bin Amir, Sheikh Suleiman Takadir, Mwinjuma Mwinyikambi, Mohamed Jumbe Tambaza, Omar Londo, Rajab Diwani, Mshume Kiyate, Bibi Tatu bint Mzee, Bibi Asha Ngoma, Bibi Titi Mohamed, Bibi Hawa bint Maftah, Bibi Khadija bint Kamba, Said Chamwenyewe na wengi wengine. Ilikuwa na kutokana na msaada wa Abdulwahid na Waislam hawa ndiyo uliomuwezesha Nyerere kuwa katika siasa na kuchukua uongozi wa nchi miaka tisa baadae.
Hakuna aliyeweza kukisia ni mawazo gani yalikuwa yanapita katika fikra za Nyerere. Lakini ni wazi kuwa alikuwa akimfikiria Abdulwahid na jinsi pamoja walivyoweza kuanzisha harakati za kudai uhuru wa Tanganyika. Ilikuwa miaka kumi na tano iliyopita katika Ukumbi wa Arnatouglo, si mbali na pale alipokuwa, Nyerere aligombea urais wa TAA na rais aliyekuwa madarakani, Abdulwahid Sykes. Abdulwahid akiwa na umri wa miaka thelathini na Nyerere akiwa na miaka thelathini na mbili.
***
Tarehe 27 Aprili, 1985 Julius Kambarage Nyerere, sasa akijulikana kama Baba wa Taifa,294 katika sherehe kubwa katika viwanja vya Ikulu, alitoa jumla ya medali 3979 kwa Watanzania waliochangia katika maendeleo ya taifa. Kati ya wale ambao walipewa medali hizo alikuwa Sheikh Abdallah Chaurembo.
Wazalendo waliotajwa ndani ya kitabu hiki ambao walipigania uhuru wa Tanganyika, hakuna hata mmoja wao aliyekuwa katika orodha ile ya heshima. Baada ya siku chache kupita, Nyerere kama mtu aliyegutuka alimualika Dossa Aziz Ikulu. Dossa Aziz, wakati wa kudai uhuru wa Tanganyika alikuwa mtu maarufu, mwenye nafasi, na kujiweza sana. Sasa Dossa baada ya miaka kupita hakuwa akifahamika tena na ule umaarufu na utajiri wake ulikuwa umetoweka. Alikuwa akiishi maisha ya kawaida kijijini Mlandege, maili chache nje ya Dar es Salaam. Katika sherehe ya faragha Nyerere alimtunukia medali Dossa Aziz, rafiki yake wa zamani. 295
Ule Mkutano wa Tabora ulikuwa umeacha kovu lake katika historia ya uhuru wa Tanganyika. Huenda kama si yale masharti ya uchaguzi wa kura tatu, historia ya TANU na kwa hakika ile ya ukoloni Tanganyika isingekuwa hivi ilivyo sasa. Yamkini kusingekuwepo na mgawanyiko katika TANU wala Zuberi Mtemvu asingeunda ANC, na Mashado Plantan - AMNUT; wala suala la udini katika siasa za Tanganyika lisingewekwa katika agenda, jambo ambalo kwa miongo mitatu baada ya uhuru ngurumo zake bado zinasikika na zinatishia utengemano na uthabiti wa nchi. Waislam wanamlaumu Nyerere na Wakristo waliokabidhiwa madaraka ya kutawala nchi kwa msaada mkubwa wa Waislam. Waislam wanadai kuwa wamesalitiwa. Kwa hivi sasa Waislam wako katika mwelekeo wa kujitambua kwa mara ya pili na historia yao yenye mengi sana. Wanaamini majibu ya baadhi ya matatizo yao ya hivi sasa yamo katika historia yao ya zamani.
***
Mjini Dar es Salaam katika msikiti wa Kitumbini hawli husomwa kila mwaka katika mwezi wa Oktoba kumkumbuka Abdulwahid Kleist Sykes. Hii ni hafla ya kifamilia ikihudhuriwa hasa na wana-ndugu. Ukiachia mbali ule wajibu wa Waislam kurehemiana kama ilivyo kawaida katika Uislam, Abdulwahid hufanyiwa hafla hii pale msikitini kwa sababu nyingine. Katika umri wake mfupi, Abdulwahid alikuwa akiswali pale msikitini na katika msikiti ule ndipo aliposwaliwa swala yake ya mwisho kabla ya kupelekwa kuzikwa. Abdulwahid alikuwa mtu mashuhuri katika jamii ya Waislam Dar es Salaam. Alifanya shughuli nyingi chini ya Al Jamiatul Islamiyya. Halikadhalika alikuwa katibu baadae rais wa TAA. Ingawa historia ya Tanzania bado haijamtambua mchango wake ni wazi kuwa Abdulwahid ndiye aliyekuwa bongo katika kuasisi TANU chama ambacho kilikuja kuwaunganisha wananchi wa Tanganyika katika kudai uhuru wao kwa Waingereza.
Marika ya Abdulwahid bado wa hai na baadhi yao wanaswali pale msikitini. Huwa wanafurahishwa na kumbukumbu hii ya kumrehemu mwenzao. Karibu walio wengi ni maveterani wa TANU ya miaka ya 1950. Hivi sasa wao ni wazee na kwa uchungu hawana haja na siasa. Ukiacha ndugu wa marehemu Abdulwahid (sasa hivi wanajumuika na wajukuu zake), marafiki wa karibu na wanachama wa zamani wa TANU, hakuna hata mtu mmoja katika Chama cha Mapinduzi (chama kilichorithi nafasi ya TANU) anaemkumbuka. Jina la Abdulwahid halitajwi kabisa katika historia ya kudai uhuru wa Tanganyika au katika historia ya kuasisi TANU. Juu ya haya yote Abdulwahid ndiye aliyewasha cheche za kuanzisha harakati za kudai uhuru wa Tanganyika.
Jopo la wana-historia wa Chama Cha Mapinduzi waliopewa jukumu la kutafiti na kuandika historia rasmi ya TANU, hakuna hata sehemu moja waliyotaja jina la Abdulwahid katika kitabu kizima.296 Dhana inayojaribiwa kuenezwa katika kitabu kile ni kuwa kabla ya kutokea kwa Julius Nyerere mwezi Aprili, 1953, alipochaguliwa kuwa rais wa TAA, chama hicho hakikuwa na mwelekeo wowote wa siasa. Kitu cha ajabu ni kuwa kitabu hicho wala hakielezi huo urais wa TAA, Nyerere aliupataje au aliuchukua kutoka kwa kiongozi gani wa wakati ule. Kitendo hiki kimeondoa hadhi na heshima ya wazalendo wengi waliopigania nchi hii na halikadhalika kimeiondolea TAA heshima ya kuitwa chama cha siasa. Wanahistoria wazalendo pamoja na wanasiasa wa sasa hawataki kabisa kuipa TAA hadhi ya chama cha siasa. Kambona aliiita African Association chama cha majadiliano:
Sasa inakaribia mwaka mmoja toka iundwe Tanganyika African National Union na katika kipindi hiki chama kimekua kikipata nguvu siku hadi siku, wakati mwingine chini ya upinzani mkubwa. Kama mnavyofahamu chama hiki ni badala ya Tanganyika African Union ambayo ilikuwa sawasawa na chama cha majadiliano.297
Ulotu anaieleza TAA kuwa ilikuwa chama cha ustawi wa jamii.298 Wengine wameieleza TAA kama taasisi ya jamii: Nyerere (1976), 299 halikadhalika Japhet na Seaton (1966).300 TAA wakati mwingine inaelezwa kuwa ilikuwa chama cha vuguvugu za upinzani dhidi ya ukoloni, lakini upinzani wake haukuwa dhahiri: Kaniki (1974), 301 Nyerere (1953) 302 aliieleza TAA kama chama cha vuguvugu la siasa lakini si za dhahiri. Julius Nyerere alipohutubia Baraza la Udhamini la Umoja wa Mataifa, New York, tarehe 7 Machi, 1955 alisema:
Tanganyika African National Union kwa mtazamo mmoja ni chama kipya, lakini kwa mtazamo mwingine ni chama kikongwe. TANU imechukua nafasi ya Tanganyika African Association ambayo ilianzishwa mwaka 1929, kama chama cha kijamii. Tanganyika African National Union, chama kilichochukua nafasi ya African Association miezi kumi iliyopita ni chama kipya kwa maana ni chama cha siasa, wakati TAA ilikuwa chama cha siasa nusunusu.
Wasomi wengine wameishusha TAA kufikia daraja la kuwa klabu: Mwenegoha (1976) anaandika: 'Mwaka 1954, baada ya miaka ishirini na tano ya kutoweza kufanya lolote, Nyerere aliigeuza TAA kutola chama cha kijamii kuwa chama cha siasa chenye kuogopwa kilichoitwa Tanganyika African National Union'. 303
Abdulwahid ambae alitoa mchango wa pekee katika kuunda TANU alikuwa anaiona TAA kama chama cha siasa (1951). 304 Katika kundi la waandishi na wasomi walioandika kuhusu African Association kisha wakabadili mawazo yao kuhusu nini hasa chama kile kilikuwa, ni Nyerere na Hatch ndiyo waliobadili misimamo yao ya awali. Nyerere alipoandika barua kwa Gavana wa Tanganyika, Edward Twining tarehe 10 Agosti, 1953 alieleza kuwa TAA ni chama cha siasa. 305
Lakini baadae alibadili msimamo na kusema kuwa TAA kilikuwa chama cha starehe. Kauli hii ilitawala hotuba za Nyerere na maandishi yake kwa kipindi kirefu. Katika miaka ya hivi karibuni amesikika akisema kuwa TAA kilikuwa 'chama cha siasa kisichokuwa na katiba ya siasa'. Hatch (1976) ameieleza TAA kama chama cha starehe 306 sehemu moja na chama cha siasa sehemu nyingine.307 John Kabudi ameieleza African Association kama 'chama cha watu binafsi wananchi kilichokuwa na mwelekeo wa kitaifa'.308 Ieleweke kuwa hata viongozi wa TAA hawathaminiwi kama wanasiasa. Kaniki, kwa kukosa neno la kuwatambulisha waasisi wa TAA, amewaita wanasiasa na kuwawekea quatation mark:
Nyerere, kabla ya hapo akiwa hajulikani na 'wanasiasa' wengi katika Tanganyika, alikuwa mwalimu katika shule ya Mtakatifu Francis, Pugu, jirani na Dar es Salaam, na alikuwa amechaguliwa rais wa (TAA) mwaka uliopita.309
Kwa mtazamo huo wa Kaniki mzalendo kama Abdulwahid Sykes hakuwa mwanasiasa, ila Nyerere ndiye mwanasiasa. Iliffe (1968)310 alidokeza kuwa historia ya TANU iliyokuwa imeandikwa hadi wakati ule ilikuwa haijakamilika na katika uchambuzi wake alisema kuwa African Association kutokana na mwelekeo na wanachama wake ilikuwa ni chama cha siasa. Kandoro na Japhet, 311 waasisi wa TANU walipata umaarufu wakati Abdulwahid akiwa rais wa TAA mwaka 1952. Hawa walikuwa ndiyo waasisi pekee ambao walifanya kazi na Abdulwahid wakati wa Mgogoro wa Ardhi ya Wameru. Safari ya Kirilo kuja Dar es Salaam na kule kumweka Seaton kama mwanasheria kushughulikia mgogoro ule, kazi yote hiyo ilifanywa na Abdulwahid na uongozi a TAA wa wakati ule. Ilikuwa Abdulwahid ndiye aliyemhangaikia Kirilo kupata pasi ya kusafiria baada ya kunyimwa pasi kule Arusha. Kirilo na Seaton na halikadhalika Kandoro wamenadika kumbukumbu zao kuhusu ukoloni, lakini cha ajabu na kusikitisha ni kuwa hakuna hata sehemu moja waandishi hawa wametaja mchango wa Abdulwahid hata kwa kuparazia tu. Waandishi hawa wamejaribu kumtumbukiza Nyerere kama kiongozi aliyehusika katika Mgogoro wa Ardhi ya Wameru, wakati yeye hata kuwapo nchini wakati ule hakuwapo. Ukweli ni kuwa wakati mgogoro wa ule ulipofikishwa mbele ya Baraza la Udhamini la Umoja wa Mataifa, New York, Nyerere alikuwa masomoni Chuo Kikuu cha Edinburgh Uskochi akisomea shahada ya pili. Mwandishi aliyejipambanua na hawa wote kwa kutomtaja Abdulwahid ni mama wa Kiingereza Judith Listowel (1965) 312 ambae ingawa amemtaja kijuujuu, ameandika kwenye kitabu chake kuwa Abdulwahid alikuwa mmoja wa waasisi wa TANU.
Katika miaka hii ya karibuni kumejitokeza hamu ya kutaka kuielewa historia ya siasa katika Tanzania na jina la Abdulwahid limekuwa likijitokeza mara kwa mara katika majarida, 313 magazeti, 314 magazeti ya kimataifa, 315 na katika vitabu. 316 Maandiko yote haya yanamtazama Abdulwahid kwa sura tofauti. Yapo yanasema kuwa yeye ndiye alikuwa kinara katika kuunda TANU na kumtia Nyerere katika siasa. Katika maandiko haya Abdulwahid anaelezwa kama mzalendo na mwanamapinduzi. Tandon anamweleza Abdulwahid na wazalendo wengine katika Afrika ya Mashariki kama Chege Kibachia, Makham Singh, Fred Kubai, James Kivu, I.K. Musazi, Erika Fiah na Gama Pinto kama 'viongozi maveterani wa watu wa Afrika ya Mashariki ambao wanahistoria wetu wa sasa wamewasahau'. 317 Wapo waandishi wanaomuona Abdulwahid kama 'kabaila uchwara' kutokana na kuwa alikuwa mtoto wa mfanyabiashara Mwafrika tajiri, Kleist Sykes.
Profesa Shivji anamtuhumu Abdulwahid kwa kushirikiana na wakoloni na anamchukulia kama kabaila uchwara ambae yeye mwenyewe hatoki katika tabaka la wafanyakazi. Akitafakari nafasi ya Abdulwahid kama kiongozi wa makuli katika bandari ya Dar es Salaam wakati wa ukoloni Shivji ansema:
serikali ilipenyeza uongozi wa makabaila uchwara katika chama. Mwezi February 1948 Abdul Sykes, mtoto wa mfanya biashara Mwafrika maarufu, aliombwa na serikali awe katibu wa chama cha makuli. Abdul Sykes hakuwa akifanyakazi bandarini wala hakuwa anatoka katika tabaka la wafanyakazi.318
Hapa Shivji alikuwa anaeleza jinsi Abdulwahid alivyochaguliwa kuwa katibu mkuu wa kwanza katika historia ya vyama vya wafanyakazi Tanganyika. Kwa kutoijua vyema historia ya maisha ya Abdulwahid na vilevile kwa hamaki za misimamo ya mrengo wa kushoto ya Ki-Marx, Shivji ametumia vipimo visivyo sawa katika kumchambua Abdulwahid. Engels anasema bepari uchwara ni 'tabaka la makabaila wa kisasa ambao wanahodhi njia zote za uzalishaji mali za jamii na vilevile wanawaajiri na kuwalipa'.319 Hata hivyo Sklar anasema kuwa dhana hiyo sasa imebadilika kwa hiyo hata ile maana yake ya awali imebadilika:
Hivi sasa neno hilo linatumiwa na wafuasi wa Marx kuieleza tabaka lililo juu katika jamii ambazo linafuata soko huria na kuachia kuhodhiwa kwa mali kama matokeo ya mali binafsi katika uzalishaji wake.320
Kama Shivji angeliyajua maisha ya Abdulwahid ni wazi kuwa angetumia kipimo kingine kabisa katika kumweleza. Lakini kwa kuwa kilichotumika ni kipimo kisicho sawa, matokeo yake hayakuweza kuwa barabara. Hakuna biashara ya Mwafrika wakati wa ukoloni inaweza kuitwa biashara ya bepari na katika mkumbo wa kujumuishwa katika dhana ya ubepari, kama ubepari ulivyokuwa ukifahamika huko Ulaya. Haya ndiyo matatizo yanayoikumba historia ya Abdulwahid na kwa kweli historia nzima ya taifa la Tanganyika.
Katika wale walioasisi TANU, ni wale tu aliokuwa makao makuu ya TAA ndiyo wanaoweza kueleza historia ya kweli ya chama hiki. Hawa ni John Rupia, Dossa Aziz, Tewa Said Tewa, Julius Nyerere, Dome Budohi, Abdulwahid na Ally Sykes. Hawa ndugu wawili, Abdulwahid na Ally, wao ni baba yao ndiye aliyekuwa muasisi wa African Association akiwa kama katibu wake wa kwanza hapo mwaka wa 1929. Majalada ya akina Sykes kuhusu African Association na TANU yana habari muhimu sana kwa mtafiti kuhusu historia ya ukoloni na juhudi walizofanya waasisi wa taifa la Tanganyika katika kujikomboa. Majalada haya yana habari muhimu na za kutosha kuhusu Nyerere na jinsi alivyopokelewa Dar es Salaam na akina Sykes na jinsi alivyoingizwa katika siasa. Inastaajabisha kuwa kumbukumbu hizi zenye habari muhimu sana kuhusu Nyerere na TANU hazikuguswa kabisa wakati watafiti wa historia ya TANU walipokuwa wakifanya utafiti wao. Inastaajabisha vilevile kuwa, si Ally wala mdogo wake, Abbas ndugu wawili walio hai baada ya kifo cha kaka yaoAbdulwahid, walifanyiwa mahojiano yoyote na watafiti wale.
Katika miaka ya mwishoni ya 1960, John Iliffe akiwa Idara ya Historia ya Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam, alipoanza utafiti wake wa historia ya Tanzania, aliweza kukusanya habari nyingi sana na muhimu kutoka kwa mmoja wa wanafunzi wake, Aisha Daisy Sykes, binti wa Abdulwahid. Ingawa Daisy alimfahamisha Iliffe kuwa habari zile alizokuwa akiandika katika semina kuhusu historia ya Tanganyika alikuwa akizipata kutoka kwa baba yake, inastaajabisha kuwa, Iliffe japo kuwa alikua muhihataji sana wa kutaka kujua historia ya Tanganyika, hakuchukua tabu ya kuonana na Abdulwahid ili apate habari zile moja kwa moja kutoka kinywani kwake.
Iliffe hata hivyo kwa kujua hazina ya historia iliyokuwa katika kumbukumbu za akina Sykes, alimtia hima Daisy aandike historia ya maisha ya babu yake, Kleist Sykes. Utafiti huu Daisy aliufanya kwa ufanisi mkubwa. 321
Baba yake alipofariki dunia mwaka wa 1968, Daisy kutokana na mafanikio ya kuandika habari za babu yake sasa akataka kufanya utafiti na kuandika maisha ya marehemu baba yake. Daisy aliamua kufanya hivyo kwa uchungu alipokuja kugundua kuwa historia ilikuwa haimtendei haki baba yake. Daisy alihisi ilikuwa ni wajibu wake kuueleza ulimwengu baba yake alikuwa nani na nini mchango wake katika kuikomboa Tanganyika kutoka ukoloni wa Waingereza. Hiki alikiona kitu muhimu ili kuiweka sawa historia ambayo kwa makusudi ilikuwa inapotoshwa. Daisy alikuwa na majalada na shajara zote za baba yake. Iliffe kwa sababu ambazo kwa wakati ule Daisy hakuweza kuzitambua, alimkataza asifanye hivyo kwa kuwa wakati wa kuandika historia ya baba yake ulikuwa bado. Iliffe alimwambia Daisy afanye subira hadi hapo baadae. Ni wazi kuwa Iliffe alikuwa akijua kuwa Abdulwahid alikuwa mtu muhimu na wa kuaminika katika historia ya TANU; na kuwa utafiti wowote katika maisha yake kungesaidia sana kuielewa historia ya Tanzania. Kutokana na msimamo huu wa Iliffe Daisy hakujaaliwa tena kuandika maisha ya baba yake.
Historia ya TANU siku zote imekuwa ikitawaliwa na mambo kama haya. Mwaka wa 1962 Ally Sykes alijaribu kuandika historia ya TANU katika gazeti la Mambo Leo. Mhariri wa gazeti lile M.J. Sichwale alimuandikia Ally Sykes kumfahamisha kuwa hawezi kuchapisha makala yake kwa kuwa mwandishi hana utaalamu na somo aliloliandikia.322
TAA ilipogeuzwa kuwa TANU, wanaharakati wa TAA, labda kwa kuanza kuhisi kuwa historia yao ilikuwa inataka kupotoshwa na wale waliokuja katika siasa na TANU, walikuwa na fikra za kuandika historia ya TANU. Mwalimu Kihere, mmoja wa viongozi wa TAA Tanga, alipata wakati fulani kumwambia Abdulwahid na Ally Sykes, Dossa Aziz na John Rupia kuwa ingekuwa vyema historia ya siasa katika Tanganyika ikaandikwa na kuhifadhiwa wakati wao wangali hai kuepusha kuingizwa uongo ndani yake na kupindisha ukweli na hao watakaokuja hapo baadae baada ya wao kutoweka. Bahati mbaya wazo hili halikupewa uzito iliostahili na hadi Mwalimu Kihere, Abdulwahid na John Rupia, Stephen Mhando na Hassan Suleiman wanafariki dunia, hakuna hata mmoja katika wale wakongwe wa siasa alikuwa wameandika kitu chochote.
Hassan Suleiman anawalaumu wanahistoria kwa kukosekana kuandikwa historia ya kweli ya uhuru wa Tanganyika kwa kuwapuuza wazalendo wengine na badala yake kuandika historia ya Tanganyika kwa kuegemeza historia hiyo kwa Nyerere. Kabla hajafariki, Hassan Suleiman alichukua nyaraka zake zote binafsi za African Association wakati alipokuwa kiongozi na kuzikabidhi kwa Katibu Mkuu wa CCM wakati ule Rashid Kawawa katika sherehe mahsusi iliyofanyika Makao Makuu ya CCM, Dodoma.
Kwa mara ya kwanza historia ya TANU ilitaka kuandikwa na Abdulwahid mwenyewe. Baada ya kupatikana kwa uhuru mwaka 1961 na TANU ilipokuwa sasa inataka kujiimarisha kama chama cha umma, inasemekana Nyerere wakati ule Waziri Mkuu alimuomba Abdulwahid aandike historia ya harakati ya Waafrika wa Tanganyika dhidi ya ukoloni wa Waingereza. Hii kwa hakika ndiyo historia ya TANU. Dr Wilbert Kleruu ambae ndiyo kwanza alikuwa ametoka masomoni Marekani alichaguliwa na TANU asaidiane na Abdulwahid katika utafiti na uandishi wa historia ile.
Abdulwahid alirudi kwenye ofisi za TANU makao makuu; kwenye ofisi yake ya zamani aliyokuwa akiitumia kama rais wa TAA. Nyaraka zake binafsi, za baba yake nyingine kuanzia mwaka wa 1929 wakati wa enzi za African Association zililetwa pale kwa utafiti kama ushahidi wa yale yaliyopitika zama hizo. Maelezo ya Abdulwahid katika kuanzishwa kwa Africa Association inasemekana hayakumpendeza Nyerere, kwa kuwa mwanzo wa harakati dhidi ya ukoloni jina la baba yake Abdulwahid ­ Kleist Sykes, lilikuwa likitawala. Halikadhalika ilipofika kueleza namna TAA ilivyokujabadilishwa kuwa TANU watoto wake wote watatu Abdulwahid, Ally na Abbas wakiongozwa na kaka yao mkubwa Abdulwahid halikadhalika likawa linatawala harakati zile. Historia hii inasemekana haikumpendeza Nyerere na baadhi ya viongozi wa TANU. Haukupita muda Abdulwahid akatambua kuwa viongozi wapya walioshika nafasi katika TANU kwa kweli hawakuwa na nia hasa ya kutafiti na kuandika historia ya Tanganyika bali nia na azma yao ilikuwa na kumjenga Nyerere na kumkuza kwa sifa ambazo hazikumstahili. Abdulwahid alipong'amua hili haraka akajitoa katika kazi ile. Hata hivyo Dr Kleruu aliendelea na utafiti na akaandika historia ya TANU. Historia hii iansemekana ilifuta mchango mzima wa akina Sykes katika kuunda TAA na baadae TANU. Hata hivyo baada ya kazi hii kukamilika haikuchapishwa na ikabaki katika maktaba ya TANU, Mtaa wa Lumumba, Dar es Salaam. Lakini baadae kazi ile ilitoweka na ikachapishwa baada ya 'mwandishi' kufanya mabadiko kadhaa katika mswada ule ili usitambulike chanzo chake. Hata hivyo TANU iligundua kuwa ile ilikuwa historia yao iliyoandikwa na Dr. Kleruu na wakafanya bidii kuzuia isichapishwe. Kimya kimya TANU ikafanya juhudi ya kuzuia kitabu hicho kisitoke toleo la pili. Lakini hili halikuwezekana na kitabu hicho kimechapishwa sasa mara kadhaa. Uandishi wa kitabu kile haukutofautiana sana na kitabu cha TANU kilichotoka mwaka 1981 kilichoandikwa na Chuo cha TANU cha Kivukoni.
Hata hivyo kuna kasoro katika kitabu hicho ambacho 'mwandishi' alishindwa kugundua na kuweza kujikinga asijulikane kama kile kitabu hakikuandikwa na kalamu yake. 'Mwandishi' kama tunavyoweza kumwita, akiandika katika nafsi ya kwanza, anaeleza kuwa amekiandika kitabi kile mwaka wa 1964. Katika maelezo hayo 'mwandishi' anatoa habari ambazo msomaji makini anahisi kuwa 'mwandishi' alikuwa marika sawa na anawafahamu vyema wale wazalendo anaoandika habari zao. Lakini mwandishi anasahau kuwa mwaka 1964 wakati yeye anadai alikuwa akiandika habari hizo yeye alikuwa mvulana mdogo na asingeweza kuwajua vile wale wazalendo na habari zilizotokea miaka ya 1950 wala asingeweza kuwa na ubongo wa kutafakari mambo kama yale. Sasa swali linakuja. Huyu aliyeandika habari zile ni nani hasa? Kutokana na maelezo ambayo kitabu hiki kimeeleza ni wazi aliyeandika habari zile hawezi kuwa Dr Kleruu kwa sababu Kleruu katika kipindi kile, hakuwapo katika harakati zile za kuunda TANU. Ni mtu mmoja tu ndiye anaeweza kuwa na habari zile na kuwa na ufahamu wa mambo yalivyokuwa miaka ile. Huyu atakuwa ni marehemu Abdulwahid akiandika mwaka 1964. 'Mwandishi' kwa ujinga amenakili kutoka kwenye maandishi ya Abdulwahid ambayo yalikuwa yamehifadhiwa katika Maktaba ya TANU, Dar es Salaam. Na huyu 'mwandishi' wala hakunakili maandishi yale mwaka 1964, bali miaka mingi baada ya kifo cha Abdulwahid kutokea.
Abdulwahid alipobaini kuwa historia ya Tanganyika inaweza kuwa chanzo cha husda na hasama kati yake na Nyerere na viongozi wengine wa TANU, akaamua kutosema chochote kuhusu hilo ingawa kabla hajafa alikubali mwaliko wa Chama Cha Historia Cha Tanzania (Historical Association of Tanzania) (HAT). Imeshindikana kujua Abdulwahid alizungumza kuhusu nini katika mwaliko ule, lakini inasemekana moja ya maswali aliyoulizwa ilikuwa kuwa kama si kweli Nyerere ndiye aliyekipa chama uhai kuanzia mwaka wa 1954. Katika kujibu swali hili Abdulwahid alilirudisha swali lile kwa wasikilizajiwake kwa kutoa mfano wa John Glenn, Mmarekani wa kwanza kwenda angani kuzunguka dunia. Abdulwahid aliwauliza wasikilizaji wake, 'Nani apewe sifa, wanasayansi wa Kimarekani waliotengeneza roketi ile au John Glenn aliyekuwa rubani wa chombo?'
Mwaka 1962 Judith Listowel alipokuja Tanganyika kufanya utafiti kabla hajaandika kitabu chake The Making of Tanganyika, alitaka sana kufanya mahojiano na Abdulwahid. Kwa kujua matatizo yaliyokuwa yanakabili historia ya Tanganyika mara ya kwanza ilipojaribiwa kuandikwa, Abdulwahid alijaribu sana kumkwepa Listowel. Listowel alipokuja kumkamata Abdulwahid nyumbani kwake Magomeni Mikumi, yeye hakupenda kueleza mchango wake wala wa baba yake katika kuaisisi African Association na TANU. Kwa kweli katika mahojiano yake Listowel hakupata chochote cha maana sana. Hata hivyo Listowel aliweza kuelezwa na Abdulwahid jinsi TANU ilivyokuja kuasisiwa. Listowel alikuja kuandika katika kitabu chake kuwa: 'Abdul Sykes, kaka yake Ally, alisema kuwa ilibidi waamshe fikra za siasa za wananchi ili kiundwe chama cha siasa'.323 Kutokana na mazungumzo haya na Abdulwahid, Listowel alimwandikia Ally Sykes: 'Nimependezwa sana na kaka yako na ningefurahi kama ningepata wasaa wa kuwa na mazungumzo na yeye zaidi'.324 Akiwa London Listowel alimuandikia Ally Sykes mara kadhaa akitaka ufafanuzi kuhusu mambo mengi muhimu katika historia ya Tanganyika.
Abdulwahid alipofariki Wizara ya Habari ilitoa taarifa ikieleza kuwa Rais Nyerere amehudhuria maziko ya Abdulwahid Sykes.325 Kingine kinachostaajabisha ni kuwa taarifa ile ilitoa maelezo machache ya uajiriwa wake katika serikali na kuacha maelezo muhimu ya Abdulwahid katika siasa. Ilikuwa Mwingereza, Brendon Grimshaw, mhariri wa Tanganyika Standard, ndiye aliyempa Abdulwahid heshima na hadhi anayostahili baada ya kifo chake kwa kuchapisha taa'zia ambayo ilimweleza Abdulwahid kama: 'mmoja wa wapangaji wa vuguvugu la kudai uhuru na mmoja wa watu waliomsaidi Nyerere kuingia katika siasa '
Taa'zia ile ilitoa sifa kemkem kwa ukoo wa Sykes katika kuleta maendeleo ya siasa Tanganyika kwa kusema kuwa, 'msukumo mkubwa wa Waafrika wa Tanganyika kupata chama cha siasa chenye nguvu ulitokana na juhudi za ukoo wa Sykes'.326 Inasemekana taa'zia hii iliyompa marehemu Abdulwahid heshima na sifa za uzalendo wa hali ya juu iliwaudhi baadhi ya viongozi katika TANU. Viongozi hao wakawa wakisikika wakisema kuwa Ally na Abbas Sykes walikuwa wanajaribu kumtukuza kaka yao. Hali hii ilijitokeza tena wakati CCM ilipokuwa ikitafiti historia yake. Hassan Upeka,327 mmoja katika wasaidizi wa utafiti ule alipeleka katika jopo lile la utafiti na uandishi wa historia ya TANU, mahojiano aliyofanya na Abdulwahid miaka mingi iliyopita kuhusu historia ya TANU. Hassan Upeka alifahamishwa kuwa historia inayoandikwa haimhusu Abdulwahid Sykes. Wakati Abdulwahid anafariki dunia, Abbas alikuwa Councellor katika Ubalozi wa Tanzania Canada na Ally Sykes alikuwa amejiuzulu kazi na kushughulika na biashara. Ally Sykes alikuwa amelazimika kujiuzulu kazi kwa shinikizo kutoka serikalini kwa kuwa alikuwa ameshindwa kufuata masharti ya uongozi yaliyomtaka kiongozi asiwe na mali wala asifanye biashara.
Mwaka wa 1974 Rais Julius Nyerere aliwatwisha Chuo Cha Kivukoni jukumu la kuandika historia ya TANU. Chuo hiki kilianzishwa kama shule ya kuwasomesha makada wa TANU katika mambo ya itikadi, propaganda na uhamasishaji umma wakiiga mfano wa Ruskin College ya Uingereza. Chuo Cha Kivukoni kwa ajili hii kisingeweza kufanya utafiti huru wala kuandika historia sahihi ya TANU. Mwaka 1976, katika mkutano wa kumi na sita wa TANU Nyerere alisisitiza tena kuandikwa kwa historia rasmi ya TANU. Lakini historia rasmi ziku zote zimekuwa za kupotosha kama anavyoeleza Maslov:
Kuwafuta watu waliopita ni kasoro nyingine katika maandishi yanayohusu historia ya Chama Cha Kikomunisti cha Urusi. Katika vitabu na makala za utafiti, kama vile ni sheria, watu walio muhimu katika historia huwa wanaorodheshwa katika katika 'orodha' na baadhi yao hawatajwi kabisa.328
Historia ya Chama Cha Kikomunisti cha Urusi haina tofauti na historia ya TANU. Mwaka 1985, Rais Nyerere alipokuwa anamtunukia digrii ya heshima Basil Davidson, alitoa changamoto kwa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam kuandika historia ya kweli ya Tanzania. Mwaka 1988, katika sherehe ya kuadhimisha miaka thelathini ya Azimio la Tabora, Nyerere aliwasifu wanachama wa mwanzo wa TANU ambao walijiunga na chama kati ya mwaka 1954 na mwaka 1958. Nyerere alisema: 'Hicho kilikuwa kipindi kigumu sana katika historia ya Chama chetu na ni watu wachache sana walikuwa na ujasiri wa kujiunga na chama na kukifanyika kazi'. 329 Jambo la kustaajabisha katika kauli ya Nyerere ni kuwa wakati yeye anawasifu watu waliojiunga na TANU katika ya mwaka wa 1954 na 1958 yeye binafsi hajawaenzi wale ambao siyo tu walijiunga na TANU bali ndiyo waasisi wa TANU yenyewe. Kwa hali hii inakuwa vigumu kuamini kama kauli yake ilikuwa inatoka kwenye dhati ya nafsi yake.
Katika kuunga mkono kauli ya Nyerere kuhusu kuwakumbuka mashujaa wa uhuru wa Tanganyika, na kwa kutaka kuitikia ile changamoto yake ya kutaka historia ya kweli ya TANU iandikwe kama alivyosema mwaka wa 1974 na 1985, mwandishi wa kitabi hiki alichapisha makala katika Africa Events 330 ambayo Abdulwahid na wazalendo wengine wa TANU zilielezwa habari zao. Katika makala yale mwandishi alifanya jambo ambalo kabla yake lilikuwa halijafanywa na mwandishi yeyote. Mwandishi alisema kuwa Waislamu ndiyo walikuwa mstari wa mbale katika kupigania uhuru. Wakati ule ilikuwa mwiko kabisa kunasibisha Uislam au Waislamu na harakati za kudai uhuru. Mwandishi alipewa kemeo kali kutoka kwa mwanahistoria wa CCM, Dr Mayanja Kiwanuka,331 kiongozi wa jopo lililoandika Historia ya Chama Cha TANU 1954-1977, kitabu kinachoeleza historia rasmi ya Chama. Mwanahistoria wa Chama Cha Mapinduzi alikuwa na haya ya kusema dhidi ya mwandishi:
"Makala inadai kuwa ingawa Waislam Tanzania walitoa mchango muhimu katika harakati za kudai uhuru, zipo juhudi za makusudi za kufifilisha mchango wao. Kutokana na hayo, makala nzima ina ngano ili kuipa nguvu fikra zake, zaidi kwa kutaja majina ya wazalendo wa TANU ambao imetokea kuwa ni Waislam Ukuu wa TANU, na hasa ukuu wa kiongozi-muasisi wake, Mwalimu Nyerere, ni kuwa, baada ya muda mfupi tu toka kuasisiwa (TANU), ikaweza kuwaunganisha watu katika vuguvugu la utaifa lenye nguvu, lau kama watu hao walikuwa tofauti kwa kabila, utamaduni na dini zao Nia ya Said ni kupandiza chuki, kwa bei yoyote ile, ukweli kwake yeye si kitu muhimu.332
Hizi ndizo fikra za Kiwanuka, ambae aliaminiwa na CCM kusimamia utafiti na uandishi wa historia mahsusi ya TANU. Kilichomkera ni kusema kuwa Waislamu ndiyo waliokuwa mstari wa mbele katika kudai uhuru wa Tanganyika. Kwa ajili ya kuwataja Waislam, makala ya utafiti ikawa sawasawa na ngano, yaani hadithi. Mwandishi akatuhumiwa kusema uongo. Kiwanuka hakuweza kuuepuka msimamo wa Chama wa kutia mkazo katika kumsifu mtu mmoja, Nyerere peke yake katika kuasisi TANU - 'Ukuu wa TANU, na hasa ukuu wa kiongozi-muasisi wake, Mwalimu Nyerere ' Wakati akiandika maneno haya Kiwanuka alikuwa Katibu Msaidizi katika Idara ya Propaganda na Uhamasishaji Umma katika Chama Cha Mapinduzi. Mwandishi alijibu mashambulizi ya Kiwanuka kwa kueleza kuwa yote aliyoyaandika ni matokeo ya utafiti.333 Kufuatia majibu haya Kiwanuka aliandika fedhuli kwa kumuita mwandishi 'mwanahistoria asiye kuwa na kimo' na akamtisha mwandishi kwa kuapa kuwa endapo atajaribu kuibadisha historia ya Tanzania atamwandama yeye na ndugu zake.334 Baada ya mjadala huu baina ya mwandishi na Kiwanuka, watu wengi walijitokeza kumuunga mkono mwandishi na huo ndiyo ukuwa mwisho wa ubishi. Kingine cha kustaajabisha ni kuwa anaeiweka historia kwa kufanya utafiti na kuiandika sawa, ndiyo anayetishwa na wale waliopotosha historia wanaachiwa waendelee kuipotosha historia na kuifanyia fisadi kadri watakavyo. Kiwanuka akiwa mwanafunzi Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam, aliandika tasnifu kuhusu uhusiano wa Waislam na Wakristo Tanzania. Tasnifu hii ni muhimu kwa kila mwanafunzi wa historia ya uhuru wa Tanzania, hasa miaka kumi ya mwanzo baada ya uhuru. 335
Kutokana na makala za mwandishi zilizokuwa zinaitafsiri upya historia ya Tanzania kwa kuuweka mbele Uislam kama itikadi ya kupinga dhulma ya aina yoyote pamoja ukoloni, Fr. Peter Smith, mtaalamu wa uhusiano kati ya Waislam na Wakristo katika Kanisa Katoliki, katika juhudi za kupinga ukweli huo, alijibu kwa makala mbili.336 Katika makala moja alisema:
Kuna historia mpya zinazoandikwa hivi sasa zinazojaribu kuonyesha kuwa vuguvugu la mwanzo kuiunga mkono TANU lilikuwa vuguvugu la Kiislam. Ukweli ni kuwa Waislam walihusika, halikadhalika Wakristo ­ vuguvugu lilikuwa la utaifa, ingawa halikuwa la kupinga dini, lilikuwa ni vuguvugu la kisekula.337 (tafsiri yangu).
Father Smith wa Kanisa Katoliki na CCM inaelekea wote wana mawazo sawa katika utata huu wa historia ya Waislam na uhuru wa Tanganyika.338 Wote wawili, Kiwanuka, mwanahistoria wa CCM na Padri Smith, mtaalamu wa Uislam katika Kanisa Katoliki wanatoa mawazo yao binafsi. Hawaangalii historia unadhihirisha ukweli gani. Hakuna anaekataa kuwa Wakristo walikuwepo. Ukweli ni kuwa majina ya Kikristo yapo katika historia ya uhuru wa Tanganyika. Lakini walikuwa ni wachezaji wa pembeni si katikati ya jukwaa. Kitabu hiki kimeonyesha nafasi ya Waislam na Uislam katika kupambana na ukoloni, mchango wao katika kuunda TANU, kukipa chama wanachama na katika kuutumia Uislam wenyewe kama itikadi ya mapambano. Baraza la Wazee wa TANU Jimbo la Dar es Salaam chini ya mwenyekiti wake wa kwanza Sheikh Suleiman Takadir lilikuwa na wajumbe mia mmoja na sabini na tatu, wote Waislam.339
Kutokana na Kiwanuka, mwandishi katika kumbukumbu ya miaka ishirini toka Abdulwahid afariki dunia, aliamua kuandika historia fupi ya maisha yake.340 Abdulwahid ili kukomesha upinzani wote kwa wakati ule na hapo baadae kuhusu nafasi ya Abdulwahid katika kuasisi TANU na kudai uhuru wa Tanganyika. Makala hii ilifuatiwa na kumbukumbu iliyotolewa na watoto wake katika gazeti la CCM - Uhuru, na gazeti la serikali ­ Daily News. 341 Wahariri wa magazeti ya Chama na serikali waliposoma wasifu wa Abdulwahid tayari wakawa wameshatatizwa na habari zilizokuwa katika kumbukumbu ile. Tatizo kubwa lilikuwa habari zilizoandikwa katika kumbukumbu ile zilizokuwa zinahusisha jina la Abdulwahid na matukio muhimu katika historia ya Tanganyika. Mhariri wa Daily News, Reginald Mhango, alimpigia simu mtoto wa Abdulwahid, Kleist na kumweleza kuwa hatoweza kuchapisha kumbukumbu ile hadi amepata idhini kutoka Dodoma, Makao Makuu ya Chama Cha Mapinduzi. Hakijulikani kilichofanyika lakini kwa bahati nzuri kumbukumbu zote mbili zilichapishwa na kutokea katika magazeti yote, ya chama na serikali siku ya pili yake.
Mwaka a 1986, miaka miwili kabla, baada ya takriban miaka ishirini na tano ya ukimya, Ally Sykes alikubali kufanya majadiliano na mwandishi wa Kiingereza Paula Park. Park akachapisha majadiliano aliyofanya na Ally Sykes kuhusu ukoo wa Sykes na mchango wao katika historia ya uhuru wa Tanganyika.342 Makala ile iliposomwa Ally Sykes akawa anapata simu kutoka kwa marafiki zake na kwa wafanyabiashara wenzake wakitaka uhakika kama yale yaliyoandikwa katika gazeti lile kweli yeye ameyasema. Haukupita muda mrefu, maofisa wa Idara ya Uhamiaji walimtembelea Park na kumuomba aondoke nchini.
Hivi ndivyo mambo yalivyo na mwandishi amekuwa akiulizwa maswali mengi na watu mbalimbali kuhusu ukweli ya yale aliyokuwa akiyaandika katika mchango wa Abdulwahid katika uhuru wa Tanganyika. Wasiwasi huu umekuwapo lau kama mwandishi amefanya rejea nyingi na za kutosha kutoka magazeti ya zamani, vitabu,majarida na kumbukumbu zingine za wakati wa ukoloni. Juu ya wasiwasi wote uliokuwapo hakuthubutu kujitokeza yeyote kupinga yake mwandishi aliyoandika kuhusu historia ya Abdulwahid katika TANU na uhuru wa Tanganyika. Hata mwanahistoria wa CCM hakunyanyua kalamu yake. Hali hii ya CCM kuikataa historia yake na wakati huo huo ikidai kuwa haijaweza kuihifadhi historia yake inatoa mvuto fulani kwa watafiti kutaka kujua kulikoni. Ukweli wa kuwa CCM imeandika historia yake lakini hapo hapo imeonekana upo upungufu mkubwa unaweka wazi suala la utafiti ufanywe na watafiti huru ili ukweli upate kujitokeza. Somo la historia ya uhuru wa Tanganyika bado lipo wazi kwa utafiti zaidi.
Ni kitu gani kimesababisha haya yote. Huu ukweli unafichwa ni mpango maalum wa viongozi walioingia TANU katika siku zamwisho za mapambano kuanzia mwaka 1958 baada ya Mkutano wa Tabora ? Kwa nini jina la Abdulwahid na majina ya wazalendo wengine yamefutwa katika historia? Hao wanaofanya hivi wanataka wapate nini na kwa manufaa ya nani? Unapoingia mlango mkuu wa Makao Makuu ya CCM Dodoma huwezi kukosa kuiona picha kubwa sana iliyotundikwa juu ya ukuta ikitazama mlango. Picha hii ni ile picha ya waaasisi wa TANU iliyopigwa tarehe 7 Julai, 1954 na mpiga picha maarufu wa wakati ule Gomez. Abdulwahid anaonekana akiwa amevaa miwani ya jua akiwa amesimama kushoto kwa Dossa Aziz; wote wamevaa suti na tai. Abdulwahid anaiangalia kamera. Rais mstaafu Julius Kambarage Nyerere amevaa kaptura na soksi ndefu hadi magotini amekalia benchi mkono wa kushoto wa John Rupia. Aliyesimama nyuma ya Nyerere, Saadani Abdu Kandoro. Picha hii ndiyo kumbukumbu ya Abdulwahid iliyobaki katika Chama. Jina lake litaandikwa katika orodha ya jumla pale inapobidi kuorodheshwa majina ya wale waasisi kumi na saba wa TANU.
Haiwezekani kabisa mtafiti akafanya utafiti kuhusu TANU na asimtaje Abduwahid. Haiwezekani kabisa akatajwa Abdulwahid na ikaachwa kutajwa Al Jamiatul Islamiyya. Haiwezekani kabisa ikatajwa Al Jamiatul Islamiyya na ikaachwa kutajwa TANU na kinyume chake ni hivyo hivyo. Haiwezekani akasifiwa Abdulwahid kwa yale yote aliyoifanyia nchi yake na baba yake asitajwe pamojanae. Hakuna mtafiti yeyote atakaeweza kuandika maisha ya Nyerere na akaacha kumtaja Abdulwahid na wale waliokuwanao wakati ule na jinsi walivyomsaidia kufika pale alipofika. Wengi wanahofu kuwa katika kufanya hivyo ni sawa na kutonesha kidonda kutoka kwa jamii ya Waislam. Ingawa Waislam ndiyo walioleta uhuru wa Tanganyika, manufaa ya uhuru ni madogo sana kwao. Ni vyema kama simanzi katika kumbukizi hizi zikabaki zimesahaulika. Njia iliyobaki kuziacha ziwe zimesahaulika ni kujaribu kufuta historia ya uhuru wa Tanganyika.

No comments: