Saturday 11 April 2015

Nani Aliyepanga Surah, Aayah Na Nani Aliyetoa Majina ya Surah?

SWALI:
Swali La Kwanza: 
Asslaam aleykum,
Ni nani aliezipanga sura za Qur-an katika mpango tunaouona sasa. Ni kwa nini na kuna hikma gani. Ikiwa Suratul Baqra imeteremshwa Madina kwa nini iwe ya pili katika msahafu na isiwe ya 86, kwani za mwanzo zilianza kuteremshwa Makkah?
Swali La Pili:
Shekh, naomba tafadhali maelezo nani aliyetoa majina ya sura za qurani?  Vipi zimepangwa aya ikiwa Qurani imeteremshwa kidogo kidogo kuanzia iqra hadi aya za mwisho kabla kufa Mtume maana naona imeanza Alhamdu na kumalizikia Qul-audhu. 
 

JIBU:
Sifa zote njema Anastahiki Allaah Aliyetukuka Mola Mlezi wa walimwengu wote, Swalah na salamu zimshukie kipenzi chetu Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na Swahaba zake (Radhiya Allaahu ‘anhum) na watangu wema mpaka Siku ya Mwisho.
Shukrani zetu za dhati kwa swali lako kuhusu upangaji wa surah za Qur-aan. Ni jambo linaloeleweka kuwa hakuna jambo lolote la Uislamu isipokuwa lina hekima kubwa ni sawa tunazijua hizo hekima au la.
 
Mpangilio wa Qur-aan na majina yake yamepangwa na Yeye Mwenyewe Allaah Mwenye hekima na busara kubwa. Tufahamu kuwa Qur-aan yote ilikuwa imehifadhiwa na Allaah Aliyetukuka katika sehemu inayoitwa Lawhul Mahfuudh na kisha kuteremshwa yote usiku wa al-Qadr katika mwezi wa Ramadhaan hadi wingu wa duniani. Kutoka hapo Jibriyl ('Alayhis Salaam) akawa ni mwenye kupatiwa amri na Aliyetukuka kumteremshia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu 'Alayhi wa aalihi wa sallam) kidogo kidogo kwa miaka 23 kulingana na mahitajio.
 
Kila ilipokuwa inateremshwa Surah au baadhi ya Aayah Jibriyl ('Alayhis Salaam) kwa maagizo kutoka kwa Allaah Aliyetukuka alikuwa akimuamuru Mtume (Swalla Allaahu 'Alayhi wa aalihi wa sallam) aiweke mahali kadhaa na jina la Surah liwe kadhaa. Baada ya kuhama Madiynah, Jibriyl alikuwa akija kila Ramadhaan kumsikiliza Mtume (Swalla Allaahu 'Alayhi wa aalihi wa sallam) kisomo cha Qur-aan. Na ule mwaka aliokufa, Jibriyl alikuja mara mbili na mara ya mwisho Zayd bin Thaabit (Radhiya Allaahu 'anhu) alikuwepo.
Hivyo, alivyoaga dunia (Swalla Allaahu 'Alayhi wa aalihi wa sallam), Maswahaba (Radhiya Allaahu 'anhum) waliandika Qur-aan kama walivyofundishwa na kuagiziwa na Mtume (Swalla Allaahu 'Alayhi wa aalihi wa sallam). Hata wale waandishi wa Mtume (Swalla Allaahu 'Alayhi wa aalihi wa sallam) walikuwa wakipatiwa maagizo hayo.
Ama kuhusu Suratul Baqarah kuwa ni ya 86 si kweli na huenda kuwa ndugu yetu akawa amekosea katika ubinaadamu wake. Na hilo si la ajabu. Hakika ni kuwa Suratul Baqarah ni Surah ya 87 kuteremshwa na ya kwanza kuteremka Madiynah. Surah ya mwisho kuteremshwa Makkah ilikuwa ni ya 86 nayo ni Suratul Mutwaffifiyn (83).
 
Na Allaah Anajua zaidi
 

No comments: